Zekaria 4:1-14

  • Maono ya 5: Kinara cha taa na mizeituni miwili (1-14)

    • “Si kwa nguvu, bali kwa roho yangu” (6)

    • Usidharau siku inayoanza kwa mambo madogo (10)

4  Malaika aliyekuwa akizungumza nami akarudi na kuniamsha, kama mtu anavyoamshwa kutoka usingizini.  Kisha akaniuliza: “Unaona nini?” Nikamjibu: “Tazama! ninaona kinara cha taa cha dhahabu tupu,+ na juu yake kuna bakuli. Kina taa saba juu yake,+ naam, saba, na taa hizo zilizo juu yake zina mirija saba.  Na kando yake kuna mizeituni miwili,+ mmoja upande wa kulia wa bakuli na mwingine upande wa kushoto.”  Kisha nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Bwana wangu, vitu hivi vinamaanisha nini?”  Kwa hiyo malaika aliyekuwa akizungumza nami akaniuliza: “Hujui maana ya vitu hivi?” Nikamjibu: “Sijui, bwana wangu.”  Ndipo akaniambia: “Hili ndilo neno la Yehova kwa Zerubabeli: ‘“Si kwa jeshi, wala si kwa nguvu,+ bali kwa roho yangu,”+ asema Yehova wa majeshi.  Wewe ni nani, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli+ utakuwa nchi tambarare.*+ Naye ataleta nje jiwe la juu kabisa la hekalu huku watu wakishangilia: “Ni zuri ajabu! Ni zuri ajabu!”’”  Neno la Yehova likanijia tena, likisema:  “Mikono ya Zerubabeli imeweka msingi wa nyumba hii,+ na mikono yake mwenyewe itaikamilisha.+ Nanyi mtalazimika kujua kwamba Yehova wa majeshi amenituma kwenu. 10  Kwa maana ni nani ameidharau siku inayoanza kwa mambo madogo?*+ Kwa maana watashangilia na kuona timazi* mkononi mwa Zerubabeli. Na haya macho saba ni macho ya Yehova, ambayo yanazunguka duniani kote.”+ 11  Kisha nikamuuliza: “Mizeituni hii miwili iliyo upande wa kulia na wa kushoto wa kinara cha taa inamaanisha nini?”+ 12  Nikamuuliza mara ya pili: “Mafungu haya mawili ya matawi ya mizeituni* yanayomimina mafuta ya dhahabu kupitia mirija miwili ya dhahabu yanamaanisha nini?” 13  Basi akaniuliza: “Hujui maana ya vitu hivi?” Nikamjibu: “Sijui, bwana wangu.” 14  Akasema: “Hawa ndio wale watiwa-mafuta wawili wanaosimama kando ya Bwana wa dunia yote.”+

Maelezo ya Chini

Au “uwanda.”
Tnn., “vitu vidogo.”
Tnn., “jiwe, mkebe.”
Yaani, matawi yaliyojaa zeituni.