MAKALA YA 3

WIMBO 124 Washikamanifu Sikuzote

Yehova Atakusaidia Wakati wa Hali Ngumu

Yehova Atakusaidia Wakati wa Hali Ngumu

“[Yehova] ndiye tegemeo imara la nyakati zako.”​—ISA. 33:6.

JAMBO KUU

Tunaweza kufanya nini ili tunufaike na msaada wa Yehova wakati wa hali ngumu?

1-2. Ni changamoto gani ambazo huenda watumishi waaminifu wa Yehova wakakabili?

 MATUKIO mabaya sana yanaweza kubadili kabisa maisha yetu. Kwa mfano, ndugu mwaminifu anayeitwa Luis a aligunduliwa kuwa na kansa mbaya sana. Daktari alimwambia kwamba alikuwa na miezi michache tu ya kuishi. Monika na mume wake walimtumikia Yehova pamoja kwa bidii. Kisha siku moja, Monika aligundua kwamba mume wake, ambaye alikuwa mzee wa kutaniko, alikuwa akifanya dhambi kwa siri kwa miaka mingi. Dada mseja anayeitwa Olivia, alilazimika kuhama nyumba yake kwa sababu kimbunga kikubwa kilikuwa kinakaribia kukumba eneo lao. Aliporudi, aliona nyumba yake ilikuwa imeharibiwa vibaya sana na kimbunga hicho. Maisha ya Luis, Monika, na Olivia yalibadilika kabisa bila kutarajia. Umewahi kupatwa na tukio fulani ambalo lilibadili kabisa maisha yako bila kutarajia?

2 Ingawa sisi ni watumishi waaminifu wa Yehova, tunakabili hali ngumu na magonjwa kama watu wengine. Huenda pia tukahitaji kuvumilia upinzani au mateso kutoka kwa watu wanaowachukia watu wa Mungu. Ingawa Yehova hatukingi tusipatwe na hali hizo ngumu, anaahidi kutusaidia. (Isa. 41:10) Kwa msaada wake tunaweza kudumisha shangwe yetu, kufanya maamuzi mazuri, na kuendelea kuwa waaminifu licha ya kukabili hali ngumu. Katika makala hii, tutazungumzia njia nne ambazo Yehova anatumia, ili kutusaidia kuvumilia tunapokabili hali ngumu maishani. Pia, tutachunguza tunachohitaji kufanya ili tunufaike na msaada anaotupatia.

YEHOVA ATAKULINDA

3. Tunapokabili tukio baya sana, huenda isiwe rahisi kufanya mambo gani?

3 Changamoto. Tunapopatwa na matukio mabaya sana, huenda isiwe rahisi kufikiri kwa njia nzuri na kufanya maamuzi. Kwa nini? Huenda tukawa na maumivu makali moyoni. Huenda akili yetu ikalemewa na mahangaiko. Tunaweza kuhisi kana kwamba tupo kwenye eneo lenye ukungu mzito na hatujui tuelekee wapi. Ona jinsi dada wawili waliotajwa awali walivyohisi walipokabili majaribu. Olivia anasema hivi: “Kimbunga kilipoharibu kabisa nyumba yangu, sikujua jambo la kufanya, na hali hiyo ilinilemea sana.” Monika anasema hivi kuhusu usaliti wa mume wake: “Nilivunjika moyo sana. Nilihisi maumivu makali kana kwamba mtu ameuchoma moyo wangu. Haikuwa rahisi kufanya shughuli za kila siku maishani. Jambo ambalo niliamini halingenipata lilikuwa limenipata.” Yehova anaahidi kutusaidiaje tunapolemewa na mahangaiko?

4. Kulingana na Wafilipi 4:6, 7, Yehova anatuahidi nini?

4 Yehova anatusaidiaje? Anaahidi kutupatia kile ambacho Biblia inakiita “amani ya Mungu.” (Soma Wafilipi 4:6, 7.) Amani ya Mungu inarejelea utulivu na amani ya akilini na moyoni tunayopata kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Amani hiyo ‘inazidi uelewaji wote’; inastaajabisha sana kuliko tunavyoweza kuwazia. Kwa mfano, umewahi kuhisi umepata utulivu sana baada ya kusali kwa bidii kwa Yehova? Utulivu huo ni “amani ya Mungu.”

5. Amani ya Mungu inalindaje mioyo na akili zetu?

5 Mstari huohuo unasema kwamba amani ya Mungu “itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” Neno la awali lililotafsiriwa “linda” lilitumiwa jeshini na lilikuwa likirejelea kikosi cha wanajeshi kilichopewa kazi ya kulinda jiji ili lisishambuliwe. Wakaaji wa jiji lililolindwa walilala bila wasiwasi, wakijua kwamba wanajeshi walikuwa wakilinda malango ya jiji. Katika maana hiyohiyo, amani ya Mungu inapoilinda mioyo na akili zetu, tunahisi utulivu tukijua kwamba tuko salama. (Zab. 4:8) Kama ilivyokuwa kwa Hana, hata kama hali yetu haibadiliki papo hapo, bado tunaweza kuwa na kiasi fulani cha amani. (1 Sam. 1:16-18) Na tunapokuwa na utulivu, mara nyingi inakuwa rahisi zaidi kufikiri kwa njia nzuri na kufanya maamuzi ya hekima.

Sali hadi uhisi “amani ya Mungu” ikilinda moyo na akili yako (Tazama fungu la 4-6)



6. Tunaweza kufanya nini ili amani ya Mungu itunufaishe? (Tazama pia picha.)

6 Tunachohitaji kufanya. Kama wakaaji wa jiji walivyowaomba walinzi wawalinde, tunaweza kumwomba Yehova atulinde tunapopata matatizo. Jinsi gani? Sali hadi uhisi umepata amani ya Mungu. (Luka 11:9; 1 The. 5:17) Luis, aliyetajwa awali, anaeleza jinsi yeye na mke wake, Ana, walivyoweza kukabiliana na hali ngumu walipogundua kwamba Luis ana miezi michache tu ya kuishi. Alisema hivi: “Katika wakati kama huu, ni vigumu sana kufanya maamuzi kuhusu jinsi ya kutunza afya na mambo mengine. Lakini kusali kumekuwa jambo muhimu sana linalotupatia amani katika kipindi hiki kigumu.” Luis na mke wake walisali kwa Yehova kwa bidii na kwa kurudia-rudia wakimwomba awapatie amani ya akili, utulivu wa moyoni, na hekima ili wafanye maamuzi mazuri. Na Yehova aliwasaidia. Ikiwa unakabili hali ngumu, dumu katika sala, nawe utajionea amani ya Mungu ikilinda akili na moyo wako.​—Rom. 12:12.

YEHOVA ATAKUIMARISHA

7. Huenda tukahisije tunapokabili hali ngumu?

7 Changamoto. Tunapopatwa na hali ngumu, huenda tukahisi, tukafikiri, au kutenda kwa njia tofauti na ile tuliyozoea. Huenda tukahisi kama meli inayosukumwa huku na huku na mawimbi katika bahari yenye dhoruba. Ana, aliyetajwa awali, alisema kwamba baada ya kifo cha Luis alikuwa na hisia nyingi tofauti-tofauti. Alisema hivi: “Niliposhuka moyo, nilianza kujisikitikia. Pia nilikasirika kwa sababu hakuwepo.” Zaidi ya hayo, Ana alihisi upweke na alilemewa na hisia kwa sababu alihitaji kufanya maamuzi kuhusu mambo ambayo Luis aliyashughulikia vizuri. Nyakati nyingine, alihisi kana kwamba yuko katika bahari yenye dhoruba. Yehova anatusaidiaje hisia kama hizo zinapotulemea?

8. Kama inavyotajwa katika Isaya 33:6, Yehova anatuhakikishia nini?

8 Yehova anatusaidiaje? Anatuhakikishia kwamba atatuimarisha. (Soma Isaya 33:6.) Meli inapokabiliwa na dhoruba, inaweza kuyumbayumba kwa njia ya hatari. Ili zisiyumbeyumbe, meli nyingi zimewekewa vifaa vya pekee vinavyoisaidia meli itulie na iwe imara. Vifaa hivyo vya pekee vinaisaidia meli isiyumbe sana na kufanya safari iwe salama na yenye kustarehesha. Hata hivyo, mifumo hiyo ya kuimarisha meli hufanya kazi vizuri zaidi ikiwa meli inasonga mbele. Vivyo hivyo, Yehova atatuimarisha tunaposonga mbele kwa uaminifu wakati wa majaribu.

Jiimarishe kwa msaada wa vifaa vya utafiti (Tazama fungu la 8-9)



9. Vifaa vyetu vya utafiti vinawezaje kutusaidia kudumisha usawaziko wetu? (Tazama pia picha.)

9 Tunachohitaji kufanya. Unapolemewa na hisia kali, jitahidi kadiri uwezavyo kudumisha ratiba yako ya kiroho. Bila shaka, huenda usiweze kutimiza mambo mengi kama zamani, lakini kumbuka kwamba Yehova ana usawaziko. (Linganisha Luka 21:1-4.) Katika ratiba yako ya mambo ya kiroho, tenga wakati kwa ajili ya kujifunza kibinafsi na kutafakari. Kwa nini? Kupitia tengenezo lake, Yehova ametupatia habari nyingi nzuri zinazotegemea Maandiko ambazo zinatusaidia kudumisha usawaziko. Ili kupata habari unayohitaji, unaweza kutumia vifaa vya utafiti vinavyopatikana katika lugha yenu, kama vile programu ya JW Library®, Fahirisi, na Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Monika, aliyetajwa awali, alisema kwamba alitumia vifaa vya utafiti mara tu alipoanza kuhisi maumivu makali ya kihisia. Kwa mfano, alifanya utafiti kuhusu neno “hasira.” Wakati mwingine alifanya utafiti kuhusu “usaliti” au “ushikamanifu.” Kisha, angesoma mpaka ahisi vizuri. Alisema hivi: “Nilipoanza kufanya utafiti nilikuwa na wasiwasi sana lakini kadiri nilivyoendelea kusoma, ndivyo nilivyohisi kana kwamba Yehova ananikumbatia. Nilipoendelea kusoma nilitambua kwamba Yehova alielewa hisia zangu mbalimbali na alikuwa akinisaidia.” Msaada kama huo kutoka kwa Yehova unaweza kukusaidia wewe pia udumishe usawaziko hadi utakapopata utulivu.​—Zab. 119:143, 144.

YEHOVA ATAKUTEGEMEZA

10. Tunaweza kuhisije baada ya kupitia hali ngumu sana?  

10 Changamoto. Baada ya kupitia hali ngumu sana, huenda pindi fulani tukahisi tukiwa dhaifu kimwili na kihisia. Tunaweza kuhisi kama mwanariadha aliyejeruhiwa ambaye alikuwa na kasi sana lakini sasa anachechemea anapotembea. Huenda tukashindwa kutimiza mambo ambayo zamani tulifanya kwa urahisi, au huenda tukakosa kichocheo cha kufanya mambo ambayo awali tulifurahia. Kama Eliya, tunaweza kushindwa hata kuamka na kutamani kuendelea kulala tu. (1 Fal. 19:5-7) Yehova anaahidi kufanya nini tunapokuwa dhaifu?

11. Ni njia gani nyingine ambayo Yehova hutumia ili kutusaidia? (Zaburi 94:18)

11 Yehova anatusaidiaje? Anaahidi kututegemeza. (Soma Zaburi 94:18.) Kama ambavyo mwanariadha aliyejeruhiwa anavyohitaji msaada ili kutembea, huenda sisi pia tukahitaji msaada ili kuendelea na utendaji wetu katika utumishi wa Yehova. Katika hali kama hizo, Yehova anatuhakikishia hivi: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika kwa nguvu mkono wako wa kulia, Mimi ninayekuambia, ‘Usiogope. Nitakusaidia.’ ” (Isa. 41:13) Mfalme Daudi alipata msaada huo kutoka kwa Yehova. Alipokabili majaribu na maadui, alimwambia hivi Yehova: “Mkono wako wa kuume hunitegemeza.” (Zab. 18:35) Lakini Yehova anatutegemezaje?

Kubali utegemezo wa familia, marafiki, na wazee wa kutaniko (Tazama fungu la 11-13)



12. Huenda Yehova akatumia akina nani kutusaidia tunapokuwa dhaifu?

12 Mara nyingi Yehova anatutegemeza kwa kuwachochea wengine watusaidie. Kwa mfano, Daudi alipokuwa dhaifu, Yonathani, rafiki yake, alimtembelea ili kumwimarisha na kumtia moyo. (1 Sam. 23:16, 17) Vivyo hivyo, Yehova alimchagua Elisha ili amsaidie Eliya kwa njia hususa. (1 Fal. 19:16, 21; 2 Fal. 2:2) Leo, Yehova anaweza kutumia familia, marafiki, au wazee wa kutaniko ili kututegemeza. Hata hivyo, ikiwa tumeumizwa, huenda tukawa na mwelekeo wa kujitenga na wengine. Na tukataka tu kuwa peke yetu. Ni jambo la kawaida kuhisi hivyo. Tunaweza kufanya nini ili tupate utegemezo wa Yehova?

13. Tunahitaji kufanya nini ili tunufaike na utegemezo wa Yehova? (Tazama pia picha.)

13 Tunachohitaji kufanya. Epuka kujitenga na wengine. Tunapojitenga na wengine, mara nyingi tunajikazia fikira sisi wenyewe na matatizo tunayokabili. Njia hiyo ya kufikiri inaweza kuathiri maamuzi yetu. (Met. 18:1) Bila shaka, sisi sote tunahitaji wakati wa kuwa peke yetu, hasa tunapokabili hali ngumu sana. Hata hivyo, tukijitenga na wengine kwa muda mrefu, huenda tukawa tunakataa njia ambayo Yehova anatumia ili kututegemeza. Unapokabili hali ngumu, kubali msaada wa familia, marafiki, na wazee wa kutaniko, ingawa huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Waone kuwa njia ya Yehova ya kukutegemeza.​—Met. 17:17; Isa. 32:1, 2.

YEHOVA ATAKUFARIJI

14. Ni hali gani zinazoweza kutuogopesha?

14 Changamoto. Huenda tukapitia hali zinazofanya tuogope. Katika Biblia, watumishi waaminifu wa Mungu wameeleza kuhusu pindi walizotaabika na kuogopa kwa sababu ya maadui au matatizo mengine. (Zab. 18:4; 55:1, 5) Vivyo hivyo, tunaweza kukabili upinzani shuleni, kazini, kutoka kwa watu wa familia, au serikali. Huenda hata tukaogopa kwamba tutakufa kwa sababu ya matatizo ya afya. Katika pindi hizo, huenda tukahisi kama mtoto mdogo asiye na msaada. Yehova anatusaidiaje katika hali kama hizo?

15. Zaburi 94:19 inatupatia uhakikisho gani?

15 Yehova anatusaidiaje? Anatufariji na kutubembeleza. (Soma Zaburi 94:19.) Huenda zaburi hii ikatufanya tufikirie kuhusu msichana mdogo anayeogopa na kushindwa kulala kwa sababu ya mngurumo mkubwa wa radi. Tunaweza kuwazia baba yake akimchukua na kumbeba kwenye mikono yake hadi msichana huyo anapolala. Ingawa radi zinaendelea kupiga, msichana huyo anafarijika na kuhisi akiwa salama kwenye mikono ya baba yake. Tunapokabili majaribu yenye kuogopesha, huenda tukahitaji Baba yetu wa mbinguni atubebe kwa njia ya mfano hadi hisia hizo kali zitakapokwisha. Tunawezaje kupata faraja kama hiyo kutoka kwa Yehova?

Mruhusu Baba yako wa mbinguni akufariji kupitia Maandiko (Tazama fungu la 15-16)



16. Tunaweza kufanya nini ili tunufaike na faraja ambayo Yehova anatoa? (Tazama pia picha.)

16 Tunachohitaji kufanya. Tumia wakati kwa ukawaida pamoja na Yehova​—kwa kusali na kusoma Neno lake. (Zab. 77:1, 12-14) Kisha unapokuwa chini ya mkazo, ni wazi kwamba utafikiria kumwendea kwanza Baba yako wa mbinguni. Mweleze Yehova mambo yanayokuogopesha na kukuhangaisha. Mruhusu azungumze nawe na kukufariji kupitia Maandiko. (Zab. 119:28) Huenda ukaona kwamba sehemu fulani hususa za Biblia zinaweza kukufariji hasa unapoogopa. Kwa mfano, unaweza kupata faraja katika kitabu cha Ayubu, Zaburi, Methali, na pia maneno ya Yesu yanayopatikana katika Mathayo sura ya 6. Kadiri unavyosali kwa Yehova na kusoma Neno lake, ndivyo utakavyohisi faraja yake.

17. Tunaweza kuwa na uhakika gani?

17 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuwa pamoja nasi tunapopitia hali ngumu maishani. Kamwe hatutakuwa peke yetu. (Zab. 23:4; 94:14) Yehova anaahidi kutulinda, kutuimarisha, kututegemeza, na kutufariji. Isaya 26:3 inasema hivi kumhusu Yehova: “Utawalinda wale wanaokutegemea kikamili; utawapa amani inayodumu, kwa sababu wanakutumaini wewe.” Kwa hiyo, mtumaini Yehova, na utumie njia anazoandaa ili kukusaidia. Ukifanya hivyo, utapata nguvu tena hata wakati wa hali ngumu.

UNGEJIBUJE?

  • Ni wakati gani ambao huenda tukahitaji hasa msaada wa Yehova?

  • Tunapokabili hali ngumu, Yehova hutumia njia gani nne kutusaidia?

  • Tunaweza kufanya nini ili tunufaike na msaada wa Yehova?

WIMBO 12 Mungu Mkuu, Yehova

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.