MAKALA YA 20

WIMBO 67 “Lihubiri Neno”

Acheni Upendo Uwachochee Kuendelea Kuhubiri!

Acheni Upendo Uwachochee Kuendelea Kuhubiri!

“Katika mataifa yote, lazima habari njema ihubiriwe kwanza.”MARKO 13:10.

JAMBO KUU

Jinsi upendo unavyotuchochea kufanya kazi ya kuhubiri kwa bidii na kwa nafsi yote.

1. Tulijifunza nini katika mkutano wa kila mwaka wa 2023?

 KWENYE mkutano wa kila mwaka wa 2023, a tulipata marekebisho yenye kusisimua katika uelewaji wetu kuhusu baadhi ya mambo tunayoamini na kulikuwa na matangazo yenye kusisimua kuhusu huduma yetu. Kwa mfano, tulijifunza kwamba huenda baadhi ya watu watapata nafasi ya kuwa upande wa watu wa Yehova hata baada ya Babiloni Mkubwa kuharibiwa. Pia, tulitangaziwa kwamba kuanzia Novemba 2023, wahubiri wa Ufalme hawatahitaji kuripoti utendaji wao wote wanaofanya katika huduma. Je, mabadiliko hayo yanafanya huduma yetu isiwe muhimu, au yenye uharaka kama zamani? Bila shaka, la!

2. Kwa nini huduma yetu inapaswa kufanywa kwa uharaka zaidi kadiri siku zinavyopita? (Marko 13:10)

2 Kadiri siku zinavyopita, ndivyo ambavyo huduma yetu inapaswa kufanywa kwa uharaka hata zaidi. Kwa nini? Kwa sababu wakati uliobaki ni mfupi. Fikiria jambo ambalo Yesu alitabiri kuhusu kazi ya kuhubiri katika siku za mwisho. (Soma Marko 13:10.) Kulingana na simulizi la Mathayo kuhusu tukio hilohilo, Yesu alisema kwamba habari njema ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kabla ya “mwisho” kuja. (Mt. 24:14) Msemo huo unarejelea mwisho kabisa wa mfumo mwovu wa mambo wa Shetani. Yehova ameweka ‘siku na saa’ ambayo mambo hayo yatatukia. (Mt. 24:36; 25:13; Mdo. 1:7) Kadiri siku zinavyopita, ndivyo siku hiyo inavyokaribia zaidi. (Rom. 13:11) Kwa sasa, ni lazima tuendelee kuhubiri hadi mwisho utakapofika.

3. Ni jambo gani linalotuchochea kuhubiri?

3 Tunapotafakari kuhusu huduma yetu, inafaa tufikirie swali hili muhimu: Kwa nini tunahubiri habari njema? Kwa ufupi, upendo unatuchochea kuhubiri. Mambo tunayofanya katika kazi ya kuhubiri yanaonyesha upendo wetu—upendo wetu kuelekea habari njema, upendo wetu kuelekea watu na, zaidi ya yote, upendo wetu kumwelekea Yehova na jina lake. Acheni tuchunguze mambo hayo moja baada ya lingine.

TUNAHUBIRI KWA SABABU TUNAIPENDA HABARI NJEMA

4. Tunatendaje tunaposikia habari fulani njema?

4 Je, unakumbuka jinsi ulivyohisi uliposikia habari fulani njema, kama vile, kuzaliwa kwa mtoto katika familia yenu au kupata kazi uliyohitaji sana? Bila shaka, ulikuwa na hamu ya kuwaambia watu wa familia na marafiki habari hiyo njema. Je, ilikuwa hivyo pia uliposikia habari bora zaidi kuliko zote, yaani, habari njema ya Ufalme wa Mungu?

5. Ulihisije uliposikia kwa mara ya kwanza kweli kutoka katika Neno la Mungu? (Tazama pia picha.)

5 Kumbuka jinsi ulivyohisi uliposikia kwa mara ya kwanza kweli kutoka katika Neno la Mungu. Ulijifunza kwamba Baba yako wa mbinguni anakupenda, anataka uwe sehemu ya familia ya waabudu wake, amekuahidi kukomesha maumivu na kuteseka, na unaweza kuwa na tumaini kwamba katika ulimwengu mpya utawaona tena wapendwa wako waliokufa—na mambo mengine mengi. (Marko 10:​29, 30; Yoh. 5:​28, 29; Rom. 8:​38, 39; Ufu. 21:​3, 4) Kweli hizo zilikugusa moyo. (Luka 24:32) Ulipenda mambo uliyokuwa ukijifunza, na kwa msisimko ulitaka kumwambia kila mtu kuhusu kweli hizo zenye thamani!—Linganisha Yeremia 20:9.

Tuliposikia habari njema kwa mara ya kwanza, kwa msisimko tulitaka kumwambia kila mtu kuhusu kweli hizo zenye thamani! (Tazama fungu la 5)


6. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Ernest na Rose?

6 Fikiria mfano ufuatao. Ndugu anayeitwa Ernest b alikuwa na umri wa miaka kumi baba yake alipokufa. Ernest anasema hivi: “Nilijiuliza: ‘Je, ameenda mbinguni? Au je, hatakuwepo tena milele?’ Niliwaonea wivu watoto wengine ambao bado walikuwa na baba zao.” Ernest alienda kwa ukawaida makaburini, alipiga magoti kwenye kaburi la baba yake, na kusali hivi: “Tafadhali, Mungu, ningependa kujua mahali alipo baba yangu.” Miaka 17 hivi baada ya kifo cha baba yake, Ernest aliulizwa ikiwa angependa kujifunza Biblia, naye alikubali bila kusita. Alifurahi sana kujifunza kwamba wafu hawajui lolote, ni kana kwamba wamelala usingizi mzito, na kwamba Biblia inaahidi kutakuwa na ufufuo wakati ujao. (Mhu. 9:​5, 10; Mdo. 24:15) Hatimaye, alipata majibu ya maswali yaliyomsumbua kwa muda mrefu! Ernest alifurahia sana kweli za Biblia alizokuwa akijifunza. Rose, mke wake, alijiunga naye katika funzo hilo, naye pia aliupenda ujumbe wa Ufalme. Walibatizwa mwaka wa 1978. Waliwahubiria kwa bidii watu wa familia, marafiki, na yeyote ambaye angesikiliza kweli zenye thamani walizojifunza. Matokeo ni kwamba Ernest na Rose wamewasaidia zaidi ya watu 70 kufanya maendeleo ya kiroho na kubatizwa.

7. Ni nini kinachotokea upendo wetu kuelekea kweli za Biblia unapotia mizizi moyoni mwetu? (Luka 6:45)

7 Ni wazi kwamba upendo wetu kuelekea kweli za Biblia unapotia mizizi moyoni mwetu, hatutaweza kunyamaza. (Soma Luka 6:45.) Tunahisi kama walivyohisi wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza waliosema hivi: “Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:20) Tunaipenda sana kweli hivi kwamba tunataka kuwaambia watu wengi iwezekanavyo kuihusu.

TUNAHUBIRI KWA SABABU TUNAWAPENDA WATU

8. Ni nini kinachotuchochea kuwahubiria watu wengine habari njema? (Tazama sanduku  Wapende Watu—Fanya Wanafunzi.”) (Tazama pia picha.)

8 Kama Yehova na Mwana wake, sisi pia tunawapenda watu. (Met. 8:31; Yoh. 3:16) Tunawaonea huruma sana wale ambao ‘hawana tumaini’ na wanaishi “bila Mungu” katika ulimwengu huu. (Efe. 2:12) Wametumbukia katika shimo refu la matatizo ya maisha, nasi tuna kamba ya kuwavuta kutoka katika shimo hilo, yaani, habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kwa kuwa tunawapenda na kuwahurumia watu hao, tunachochewa kufanya kila jitihada ili kuwahubiria habari njema. Ujumbe huo wenye thamani unaweza kuwapa tumaini, kuwasaidia kuwa na maisha bora zaidi sasa, na kuwapatia tarajio la kuwa na “uzima ulio wa kweli”—uzima wa milele—katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Tim. 6:19.

Kwa kuwa tunawapenda na kuwahurumia watu, tunachochewa kufanya kila jitihada ili kuwahubiria habari njema (Tazama fungu la 8)


9. Tunatoa onyo gani kuhusu wakati ujao, na kwa nini? (Ezekieli 33:​7, 8)

9 Upendo wetu kuelekea watu unatuchochea pia kuwaonya kuhusu mwisho wa ulimwengu huu mwovu. (Soma Ezekieli 33:​7, 8.) Tunawahurumia jirani zetu na watu wa familia ambao si waabudu wa Yehova. Wengi wanaendelea na shughuli zao za kila siku bila kutambua jambo litakalotokea, yaani, “dhiki kuu ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatokea tena.” (Mt. 24:21) Tunataka wajue kitakachotokea katika wakati huo wa hukumu—dini za uwongo zitaondolewa na kufuatiwa na kuharibiwa kwa mfumo huu wote mwovu kwenye Har–​Magedoni. (Ufu. 16:​14, 16; 17:​16, 17; 19:​11, 19, 20) Tunasali kwamba watu wengi iwezekanavyo watii onyo hilo na kujiunga nasi sasa katika ibada ya kweli. Lakini namna gani wale ambao hawatii onyo hilo sasa, kutia ndani watu wa familia tunaowapenda?

10. Kwa nini ni muhimu tuendelee kutoa onyo?

10 Kama ilivyofafanuliwa katika makala iliyotangulia, inawezekana kwamba mapenzi ya Yehova ni kuwaokoa watu ambao watabadili njia zao baada ya kuona Babiloni Mkubwa akiharibiwa. Ikiwa ndivyo, basi ni muhimu hata zaidi kuendelea kutoa onyo hilo. Fikiria jambo hili: Mambo tunayowaambia sasa, huenda wakayakumbuka wakati huo. (Linganisha Ezekieli 33:33.) Labda watakumbuka onyo walilosikia kutoka kwetu na kuchochewa kujiunga na ibada ya kweli kabla haijawa kuchelewa mno. Kama yule mlinzi wa jela jijini Filipi ambaye alibadili maoni yake baada tu ya “tetemeko kubwa la ardhi,” huenda baadhi ya watu ambao hawaitikii vizuri sasa, wakabadili maoni yao baada ya kuona tukio litakalotikisa ulimwengu la kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa.—Mdo. 16:​25-34.

TUNAHUBIRI KWA SABABU TUNAMPENDA YEHOVA NA JINA LAKE

11. Tunampaje Yehova utukufu, heshima, na nguvu? (Ufunuo 4:11) (Tazama pia picha.)

11 Kumpenda Yehova Mungu na jina lake takatifu ndiyo sababu muhimu zaidi inayotuchochea kuhubiri habari njema. Tunaiona huduma yetu kuwa njia ya kumsifu Mungu tunayempenda. (Soma Ufunuo 4:11.) Tunakubali kwa moyo wote kwamba Yehova Mungu anastahili kupokea utukufu, heshima, na nguvu kutoka kwa waabudu wake washikamanifu. Tunampa utukufu na heshima tunaposhiriki na wengine uthibitisho wenye kuridhisha kwamba Mungu ‘aliumba vitu vyote’ na kwamba tunaishi kwa sababu ametupatia uhai. Tunampa nguvu—nguvu zetu—tunapotumia wakati, nishati, na mali zetu ili tushiriki kikamili katika huduma kadiri hali zetu zinavyoturuhusu. (Mt. 6:33; Luka 13:24; Kol. 3:23) Kwa ufupi, tunapenda kuzungumza kumhusu Mungu tunayempenda. Pia, tunachochewa kuwaambia wengine kuhusu jina lake na maana ya jina hilo. Kwa nini?

Tunampa Yehova nguvu zetu tunapotumia wakati, nishati, na mali zetu ili tushiriki kikamili katika huduma kadiri hali zetu zinavyoturuhusu (Tazama fungu la 11)


12. Tunalitakasaje jina la Yehova katika huduma yetu?

12 Upendo wetu kwa Yehova unatuchochea kulitakasa jina lake. (Mt. 6:9) Tunataka kuchangia katika kuliondolea suto jina lake ambalo Shetani amelichafua kupitia uwongo wake mbaya. (Mwa. 3:​1-5; Ayu. 2:4; Yoh. 8:44) Katika huduma yetu, tuko tayari kumtetea Mungu wetu, kwa kuwaeleza watu wote watakaotusikiliza ukweli kumhusu. Tunataka kila mtu ajue kwamba sifa yake kuu zaidi ni upendo, njia yake ya kutawala ni ya uadilifu na haki, na kwamba hivi karibuni Ufalme wake utakomesha kuteseka kote na kuleta amani na furaha kwa wanadamu. (Zab. 37:​10, 11, 29; 1 Yoh. 4:8) Tunapotetea sifa nzuri ya Yehova katika huduma yetu, tunalitakasa jina lake. Pia, tunafurahi kujua kwamba tunaishi kulingana na jina letu. Kwa nini tunasema hivyo?

13. Kwa nini tunajivunia kuitwa Mashahidi wa Yehova? (Isaya 43:​10-12)

13 Yehova ametuchagua tuwe “mashahidi” wake. (Soma Isaya 43:​10-12.) Miaka kadhaa iliyopita, barua kutoka kwa Baraza Linaloongoza ilisema hivi: “Kuitwa Mashahidi wa Yehova ni pendeleo lisilo na kifani.” c Kwa nini? Fikiria mfano ufuatao. Ikiwa ungehitaji mtu wa kutoa ushahidi mahakamani kuhusu sifa au tabia yako, ungemchagua mtu ambaye unamjua na kumtumaini, mtu ambaye sifa yake itafanya ushahidi atakaotoa uaminike. Kwa kutuchagua tuwe Mashahidi wake, Yehova ameonyesha kwamba anatujua vizuri na anaamini tutatoa ushahidi kwamba yeye pekee ndiye Mungu wa kweli. Tunaliona kuwa pendeleo kubwa kuwa Mashahidi wake hivi kwamba tunatumia kila fursa kuwajulisha watu jina lake na kupinga uwongo mwingi ambao wameambiwa kumhusu. Kwa kufanya hivyo, tunaishi kulingana na jina ambalo tunajivunia kuitwa, Mashahidi wa Yehova!—Zab. 83:18; Rom. 10:​13-15.

TUTAENDELEA KUHUBIRI HADI MWISHO

14. Tunatarajia kwa hamu kuona mambo gani?

14 Tunatarajia kwa hamu kuona mambo yatakayotokea hivi karibuni! Kwa baraka za Yehova, tunatumaini kuona watu wengi zaidi wakikubali kweli kabla ya dhiki kuu kuanza. Pia, tunafurahi kuna uwezekano kwamba hata kwenye kipindi kigumu zaidi katika historia ya wanadamu—dhiki kuu—huenda bado tutaona watu wengi zaidi wakigeuka na kuuacha ulimwengu huu wa Shetani unaokaribia mwisho wake na kujiunga nasi ili kumsifu Yehova!—Mdo. 13:48.

15-16. Tutaendelea kufanya nini, na hadi lini?

15 Lakini kwa sasa, tuna kazi ya kufanya. Tuna pendeleo la kushiriki katika kazi ambayo haitarudiwa tena—kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu duniani kote. Wakati huohuo, ni lazima tuendelee kutoa onyo. Watu wanahitaji kujua kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu sana. Kisha, wakati huo wa hukumu utakapofika, watajua kwamba ujumbe tuliokuwa tukihubiri ulitoka kwa Yehova Mungu.—Eze. 38:23.

16 Basi, tumeazimia kufanya nini? Tukichochewa na upendo—upendo kuelekea habari njema, upendo kuelekea watu na, zaidi ya yote, upendo kumwelekea Yehova na jina lake—tutaendelea kuhubiri kwa utayari, uharaka, na kwa bidii hadi Yehova atakaposema, “Imetosha!”

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

a Mkutano wa kila mwaka ulifanywa Oktoba 7, 2023, kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la Newburgh, New York, Marekani. Programu yote ilionyeshwa baadaye kwenye JW Broadcasting®—Sehemu ya 1 ilitolewa Novemba 2023 na Sehemu ya 2 ilitolewa Januari 2024.

b Tazama makala “Biblia Inabadili Maisha—Nilivutiwa na Majibu ya Biblia Yaliyo Wazi na Yanayoeleweka,” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2015.

c Tazama 2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova, uku. 3.