MAKALA YA 21

WIMBO 107 Mungu—Kielelezo cha Upendo

Jinsi ya Kupata Mwenzi wa Ndoa Anayefaa

Jinsi ya Kupata Mwenzi wa Ndoa Anayefaa

“Ni nani anayeweza kumpata mke mwema? Thamani yake inazidi kabisa thamani ya marijani.”MET. 31:10.

JAMBO KUU

Kanuni za Biblia zitakazomsaidia mtu aweze kumtambua mwenzi wa ndoa anayefaa na zinazowasaidia wengine kutanikoni wajue jinsi wanavyoweza kuwaunga mkono wale ambao wangependa kufunga ndoa.

1-2. (a) Ni mambo gani ambayo Wakristo waseja wanapaswa kufikiria kabla ya kuanzisha uchumba? (b) Inamaanisha nini kuanzisha “uchumba”? (Tazama “Ufafanuzi wa Maneno.”)

 JE, UNGEPENDA kufunga ndoa? Ingawa si lazima kufunga ndoa ili mtu awe na furaha, Wakristo wengi waseja, vijana kwa wazee, wanatazamia kwa hamu kupata mwenzi wa ndoa. Bila shaka, kabla ya kuanzisha uchumba, unapaswa kuwa tayari kutimiza majukumu ya kifedha, kiroho, na kihisia katika ndoa. a (1 Kor. 7:36) Ukifanya hivyo, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba ndoa yako itafanikiwa.

2 Hata hivyo, si rahisi sikuzote kupata mwenzi wa ndoa anayefaa. (Met. 31:10) Na hata unapompata mtu ambaye ungependa kumjua vizuri zaidi, huenda isiwe rahisi kuanzisha naye uchumba. b Katika makala hii, tutazungumzia mambo yanayoweza kuwasaidia Wakristo waseja kupata mwenzi wa ndoa anayefaa na kuanzisha uchumba. Pia, tutajifunza jinsi wengine kutanikoni wanavyoweza kuwaunga mkono wale wanaotaka kufunga ndoa.

KUTAFUTA MWENZI ANAYEFAA

3. Ni mambo gani ambayo Mkristo mseja anapaswa kuzingatia anapotafuta mwenzi wa ndoa?

3 Ikiwa ungependa kufunga ndoa, ni vema ujue sifa ambazo unatamani mwenzi wako awe nazo kabla ya kuanzisha uchumba. La sivyo, unaweza kutomkazia fikira mtu anayekufaa au unaweza kuanzisha uchumba na mtu ambaye hakufai. Bila shaka, mwenzi yeyote anayefaa anapaswa kuwa Mkristo aliyebatizwa. (1 Kor. 7:39) Lakini si kila mtu aliyebatizwa anaweza kuwa mwenzi wa ndoa anayekufaa. Hivyo, unaweza kujiuliza hivi: ‘Nina malengo gani maishani mwangu? Ni sifa gani zilizo muhimu zaidi kwangu ambazo ningependa mwenzi wangu wa ndoa awe nazo? Je, matarajio yangu ni yenye usawaziko?’

4. Baadhi ya watu wamesali kuhusu nini?

4 Ikiwa unatamani kufunga ndoa, hapana shaka kwamba umesali kuhusu kupata mwenzi wa ndoa. (Flp. 4:6) Bila shaka, Yehova hajatoa ahadi ya kumpatia mtu yeyote mwenzi wa ndoa. Lakini anajali kuhusu mahitaji na hisia zako, na anaweza kukusaidia unapoendelea kumtafuta mwenzi wa ndoa anayekufaa. Hivyo, endelea kumweleza hisia zako na mambo unayotamani. (Zab. 62:8) Sali ili akupe subira na hekima. (Yak. 1:5) John, c ndugu mseja kutoka Marekani, anaeleza hivi kuhusu mambo anayotaja katika sala zake, anasema: “Ninamweleza Yehova kuhusu sifa ambazo ninatamani mwenzi wangu wa ndoa awe nazo. Ninasali ili nipate nafasi za kukutana na mwenzi anayenifaa. Pia, ninamwomba Yehova anisaidie nisitawishe sifa zitakazonisaidia niwe mume mzuri.” Tanya, dada kutoka Sri Lanka, anasema hivi: “Ninapoendelea kutafuta mwenzi wa ndoa anayenifaa, ninamwomba Yehova anisaidie niendelee kuwa mwaminifu, mwenye mtazamo unaofaa, na mwenye shangwe.” Hata ikiwa utahitaji kusubiri kwa muda mrefu kuliko ulivyotarajia ili kupata mwenzi anayekufaa, Yehova anaahidi kwamba ataendelea kukutunza kimwili na kihisia.—Zab. 55:22.

5. Wakristo waseja wana fursa zipi za kukutana na watu wengine ambao wanampenda Yehova? (1 Wakorintho 15:58) (Tazama pia picha.)

5 Biblia inatutia moyo tuwe “na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Unapoendelea kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova na kutumia wakati pamoja na ndugu na dada tofauti-tofauti, utafurahia kuwa na marafiki wenye kujenga na pia utapata nafasi ya kukutana na waseja wengine, ambao kama wewe, wanakazia fikira kumtumikia Yehova. Na unapojitahidi kufanya yote unayoweza ili kumfurahisha Yehova, utapata furaha ya kweli.

Ikiwa utakuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova na kutumia wakati pamoja na ndugu na dada tofauti-tofauti, huenda ukakutana na wengine ambao wangependa kufunga ndoa (Tazama fungu la 5)


6. Wakristo waseja wanapaswa kuzingatia nini wanapotafuta mwenzi wa ndoa?

6 Hata hivyo, zingatia jambo hili: Usiruhusu jitihada zako za kutafuta mwenzi ziwe jambo muhimu zaidi maishani mwako. (Flp. 1:10) Furaha ya kweli haitegemei ikiwa umefunga ndoa au la, bali inategemea uhusiano wako mzuri pamoja na Yehova. (Mt. 5:3) Na unapokuwa mseja, huenda ukawa na uhuru zaidi wa kupanua huduma yako. (1 Kor. 7:​32, 33) Tumia vizuri wakati wako wa useja. Jessica, dada kutoka Marekani ambaye alifunga ndoa alipokuwa anakaribia umri wa miaka 40, anasema hivi, “Nilikuwa na mambo mengi ya kufanya katika huduma, na hilo lilinisaidia kuridhika licha ya kwamba nilitamani kufunga ndoa.”

TUMIA WAKATI KUFANYA UCHUNGUZI

7. Kwa nini ni jambo la hekima kumchunguza kwa muda fulani yule unayeona atafaa kuwa mwenzi wako kabla ya kumwambia kwamba unavutiwa naye? (Methali 13:16)

7 Namna gani ikiwa unafikiri kwamba mtu fulani anaweza kuwa mwenzi wa ndoa anayekufaa? Je, unapaswa kumwambia mara moja mtu huyo jinsi unavyohisi? Biblia inasema kwamba mtu mwenye hekima hutafuta ujuzi kabla ya kutenda. (Soma Methali 13:16.) Hivyo, ni jambo la hekima kumchunguza kwanza mtu kwa muda fulani bila kuzungumza naye moja kwa moja au kutumia wakati pamoja naye, kabla ya kumwambia kwamba unavutiwa naye. Aschwin kutoka Uholanzi anasema hivi: “Hisia zinaweza kusitawi haraka na kuisha haraka. Hivyo, unapotumia wakati kumchunguza mtu fulani, hutaanzisha uchumba kwa kutegemea hisia za muda mfupi.” Isitoshe, unapomchunguza mtu, huenda ukatambua kwamba hatakuwa mwenzi anayekufaa.

8. Mseja anawezaje kumchunguza mtu ambaye anaona atafaa kuwa mwenzi wake? (Tazama pia picha.)

8 Unawezaje kumchunguza mtu bila kuzungumza naye au kutumia wakati pamoja naye? Katika mikutano ya kutaniko au kwenye tafrija, huenda ukaona mambo yatakayokusaidia kutambua hali ya kiroho, utu, na mwenendo wa mtu huyo. Rafiki zake ni akina nani, na anapenda kuzungumzia mambo gani? (Luka 6:45) Je, malengo yake yanafanana na malengo yako? Huenda ukazungumza na wazee wa kutaniko lake au Wakristo wengine wakomavu wanaomjua vizuri. (Met. 20:18) Huenda ukaulizia jinsi watu wengine wanavyomwona na kuhusu sifa zake. (Rut. 2:11) Unapomchunguza mtu huyo, hakikisha unaepuka kumfanya asijihisi huru. Heshimu hisia zake na faragha yake.

Kabla ya kumwambia mtu kwamba unavutiwa naye, mchunguze kwa muda fulani bila kuzungumza naye moja kwa moja au kutumia wakati pamoja naye (Tazama fungu la 7-8)


9. Kabla ya kumfuata mtu na kumweleza kwamba unavutiwa naye, unapaswa kuwa na uhakika gani?

9 Unapaswa kumchunguza mtu kwa muda gani kabla ya kumwambia kwamba unavutiwa naye? Ikiwa utamweleza mapema mno, huenda akaona kwamba wewe hufanya maamuzi haraka-haraka bila kufikiri. (Met. 29:20) Kwa upande mwingine, ikiwa utachukua muda mrefu sana kabla ya kumwambia, huenda akafikiri kwamba huna msimamo unapofanya maamuzi, hasa ikiwa ametambua kwamba unavutiwa naye. (Mhu. 11:4) Kumbuka kwamba kabla ya kumfuata mtu na kumweleza kuwa unavutiwa naye, huhitaji kuwa na uhakika kwamba utafunga naye ndoa. Lakini unapaswa kuwa na uhakika kwamba uko tayari kwa ajili ya ndoa na kwamba mtu unayemfikiria anaweza kuwa mwenzi wa ndoa anayekufaa.

10. Unapaswa kufanya nini ikiwa unahisi kwamba mtu fulani anavutiwa nawe, lakini wewe huvutiwi naye?

10 Namna gani ukihisi kwamba mtu fulani anavutiwa nawe? Ikiwa huvutiwi naye, jitahidi kuonyesha hilo wazi kupitia matendo yako. Itakuwa jambo lisilo la fadhili kumfanya afikiri kwamba kuna uwezekano wa kuanzisha uhusiano, wakati jambo hilo si kweli.—1 Kor. 10:24; Efe. 4:25.

11. Katika nchi ambazo uchumba au ndoa inapangwa na watu wengine, ni mambo gani ambayo yanapaswa kukumbukwa?

11 Katika nchi fulani, huenda wazazi au watu wengine wazima wakatarajiwa kumchagulia mwenzi wa ndoa mtu wao wa ukoo ambaye ni mseja. Katika nchi nyingine, watu wa familia au marafiki wanamtafutia mseja mwenzi ambaye wanahisi atamfaa, kisha wanafanya mipango mwanamume na mwanamke huyo wakutane ili waone ikiwa watafaana. Ikiwa utaombwa ufanye mipango ya uchumba au ndoa, fikiria mapendezi na mahitaji ya wote wawili. Mara tu unapopata mtu anayefaa, jitahidi kujua mengi kadiri uwezavyo kuhusu utu, sifa, na zaidi ya yote, hali ya kiroho ya mtu huyo. Uhusiano wa karibu pamoja na Yehova ni muhimu zaidi kuliko pesa, elimu, au hali ya maisha ya mtu. Hata hivyo, kumbuka kwamba ndugu na dada hao waseja ndio wanaopaswa kufanya uamuzi wa mwisho ikiwa watafunga ndoa au la.—Gal. 6:5.

KUANZISHA UCHUMBA

12. Ikiwa ungependa kuanzisha uchumba na mtu fulani, unawezaje kumweleza hisia zako?

12 Ikiwa ungependa kuanzisha uchumba na mtu fulani, unawezaje kumweleza hisia zako? d Unaweza kupanga kuwa na mazungumzo na mtu huyo, katika eneo la umma au kwa njia ya simu. Mweleze waziwazi kwamba umevutiwa naye kimahaba na ungependa kumjua vizuri zaidi. (1 Kor. 14:9) Ikihitajika, mpe wakati wa kufikiria jibu. (Met. 15:28) Na ikiwa mtu huyo hataki kuanzisha uhusiano pamoja nawe, heshimu hisia zake.

13. Unaweza kufanya nini ikiwa mtu fulani anakueleza kwamba anavutiwa nawe kimahaba? (Wakolosai 4:6)

13 Namna gani ikiwa mtu atakueleza kwamba anavutiwa nawe kimahaba? Inawezekana kwamba alihitaji ujasiri ili kukufuata na kukueleza hisia zake, hivyo, mtendee kwa fadhili na heshima. (Soma Wakolosai 4:6.) Ikiwa unahitaji muda wa kufikiria kama utakubali kuanzisha naye uchumba au la, mweleze. Hata hivyo, jitahidi kumpatia jibu mapema iwezekanavyo. (Met. 13:12) Ikiwa huvutiwi naye, mweleze jambo hilo kwa fadhili na waziwazi. Ona jinsi ndugu anayeitwa Hans kutoka Austria, alivyomjibu dada ambaye alimweleza hisia zake: “Nilimweleza kuhusu uamuzi wangu kwa busara lakini waziwazi. Nilifanya hivyo mara moja kwa sababu sikutaka kumpa dada huyo tumaini la uwongo. Kwa sababu hiyohiyo, nilikuwa mwangalifu kuhusu jinsi nilivyoshirikiana naye baada ya hapo.” Kwa upande mwingine, ikiwa ungependa kuanzisha uchumba pamoja na mtu huyo, zungumzeni kuhusu hisia zenu na matarajio yenu kuhusiana na uchumba. Matarajio yenu yanaweza kutofautiana kwa kutegemea utamaduni au mambo mengine.

WENGINE WANAWEZAJE KUWAUNGA MKONO WAKRISTO WASEJA?

14. Tunawezaje kuwaunga mkono Wakristo waseja kupitia maneno yetu?

14 Sisi sote tunawezaje kuwaunga mkono Wakristo waseja ambao wangependa kufunga ndoa? Njia moja ni kwa kuwa waangalifu na mambo tunayosema. (Efe. 4:29) Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninawatania wale ambao wangependa kufunga ndoa? Ninapowaona ndugu na dada waseja wakizungumza, je, ninafikiri kwamba wana uhusiano wa kimahaba?’ (1 Tim. 5:13) Zaidi ya hayo, hatupaswi kamwe kuwafanya Wakristo waseja wahisi kwamba wamepungukiwa kwa njia fulani kwa sababu tu hawajafunga ndoa. Hans, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Baadhi ya akina ndugu wananiambia, ‘Kwa nini usifunge ndoa? Wewe si kijana tena.’ Maneno kama hayo yanawafanya waseja wahisi hawathaminiwi na yanawaongezea tu mkazo wa kutaka kufunga ndoa.” Ni bora zaidi kutafuta nafasi za kuwapongeza Wakristo waseja!—1 The. 5:11.

15. (a) Kulingana na kanuni inayopatikana kwenye Waroma 15:​2, tunapaswa kuzingatia nini kabla ya kumsaidia mtu kutafuta mwenzi wa ndoa? (Tazama pia picha.) (b) Ni masomo gani muhimu uliyojifunza katika video?

15 Namna gani ikiwa tunahisi kwamba ndugu na dada fulani watakuwa wenzi wa ndoa wazuri? Biblia inatuambia tujali hisia za wengine. (Soma Waroma 15:2.) Waseja wengi hawataki kutambulishwa kwa mtu ambaye anaonekana anafaa kuwa mwenzi wao, hivyo tunapaswa kuheshimu maoni yao. (2 The. 3:11) Huenda wengine wangependa tuwasaidie, lakini hatupaswi kuingilia kati bila wao kutuomba. e (Met. 3:27) Baadhi ya waseja wanapendelea kutambulishwa kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Lydia, dada mseja kutoka Ujerumani, anasema hivi: “Unaweza kumwalika ndugu au dada huyo kwenye tafrija yenye watu wengi. Watengenezee ndugu na dada hao fursa ya kukutana na kutumia wakati pamoja, na uache mambo mikononi mwao.”

Tafrija yenye watu wengi, inaweza kutokeza fursa kwa Wakristo waseja kukutana (Tazama fungu la 15)


16. Wakristo waseja wanapaswa kukumbuka nini?

16 Sisi sote—iwe ni waseja au tumefunga ndoa—tunaweza kuishi maisha ya furaha na yenye kuridhisha! (Zab. 128:1) Hivyo, ikiwa ungependa kufunga ndoa lakini bado hujapata mtu anayekufaa, endelea kukazia fikira utumishi wako kwa Yehova. Dada Sin Yi kutoka Macao, anasema hivi: “Wakati wa useja ni mfupi sana unapoulinganisha na wakati ambao utatumia pamoja na mwenzi wako katika Paradiso. Furahia wakati huo wa useja na uutumie vizuri.” Lakini namna gani ikiwa umempata mtu ambaye unahisi atafaa kuwa mwenzi wako na mmeanzisha uchumba? Katika makala inayofuata, tutazungumzia mambo unayoweza kufanya ili uchumba wenu ufanikiwe.

WIMBO 137 Wanawake Waaminifu, Dada Wakristo

a Ili kujua ikiwa uko tayari kufunga ndoa au la, tazama makala yenye kichwa “Urafiki wa Kimapenzi—Sehemu ya 1: Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?” kwenye jw.org.

b UFAFANUZI WA MANENO: Katika makala hii na inayofuata, neno “uchumba” linarejelea kipindi ambacho mwanamume na mwanamke wanafahamiana vizuri zaidi ili kuamua ikiwa wanaweza kuwa wenzi wa ndoa. Katika nchi nyingine, neno hilo hurejelewa pia kuwa urafiki wa kimahaba, kumjua vizuri zaidi mtu fulani, au uhusiano wa kimahaba. Uchumba unaanza wakati mwanamke na mwanamume wanapoelezana kwamba kila mmoja anavutiwa na mwenzake kimahaba, na unaendelea mpaka wanapoamua kufunga ndoa au kuvunja uchumba.

c Baadhi ya majina yamebadilishwa.

d Katika baadhi ya tamaduni, kwa kawaida ndugu ndiye anayemfuata dada ili kumwomba waanzishe uchumba. Hata hivyo, ni sawa ikiwa dada ataamua kumfuata ndugu. (Rut. 3:​1-13) Kwa habari zaidi, tazama makala “Vijana Huuliza . . . Nitamwambiaje Jinsi Ninavyohisi?” katika gazeti la Amkeni! la Oktoba 22, 2004.

e Tazama video Wapiganaji wa Imani Waliofanikiwa—Wakristo Waseja, kwenye jw.org