MAKALA YA 22

WIMBO 127 Napaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani?

Jinsi ya Kuwa na Uchumba Wenye Mafanikio

Jinsi ya Kuwa na Uchumba Wenye Mafanikio

“Yule mtu wa siri wa moyoni . . . ni [mwenye] thamani kubwa.”1 PET. 3:4.

JAMBO KUU

Mambo ambayo wale wanaochumbiana wanaweza kufanya ili uchumba wao ufanikiwe, na jinsi watu wengine kutanikoni wanavyoweza kuwaunga mkono.

1-2. Baadhi ya watu wanahisije kuhusu kipindi cha uchumba?

 KIPINDI cha uchumba kinaweza kuwa kipindi chenye shangwe na chenye kusisimua. Ikiwa kwa sasa una mchumba, bila shaka ungependa mambo yaende vizuri. Na mambo yamewaendea vizuri watu wengi wanaochumbiana. Tsion, a dada kutoka nchini Ethiopia, anasema hivi: “Mojawapo ya pindi zenye furaha zaidi maishani mwangu ni wakati mimi na mume wangu tulipokuwa wachumba. Tulizungumzia mambo muhimu, na tulicheka pia. Nilifurahi nilipogundua kwamba nimempata mtu ninayempenda na anayenipenda.”

2 Hata hivyo, Alessio, ndugu kutoka nchini Uholanzi, anasema hivi: “Nilifurahia kumfahamu mke wangu tulipokuwa tukichumbiana, lakini pia uchumba wetu ulikuwa na changamoto.” Katika makala hii, tutazungumzia baadhi ya changamoto zinazoweza kutokea wakati wa uchumba, na kanuni za Biblia zinazoweza kuwasaidia wale wanaochumbiana ili wawe na uchumba wenye mafanikio. Pia, tutachunguza jinsi wengine kutanikoni wanavyoweza kuwaunga mkono wale wanaochumbiana.

KUSUDI LA UCHUMBA

3. Kusudi la uchumba ni nini? (Methali 20:25)

3 Ingawa kipindi cha uchumba kinaweza kuwa chenye kufurahisha, kipindi hicho pia ni hatua muhimu inayoweza kuongoza kwenye ndoa. Katika siku yao ya ndoa, mwanamume na mwanamke wanaweka nadhiri mbele za Yehova ya kupendana na kuheshimiana kwa muda wote ambao wote wawili wataishi. Kabla ya kuweka nadhiri yoyote, tunapaswa kufikiria mambo yanayohusika kwa makini sana. (Soma Methali 20:25.) Kwa hakika, tunapaswa kufanya hivyo pia inapohusu nadhiri ya ndoa. Kipindi cha uchumba kinawawezesha wale wanaochumbiana kufahamiana vizuri na kufanya uamuzi mzuri. Nyakati fulani uamuzi huo ni kufunga ndoa; na nyakati nyingine uamuzi huo ni kuvunja uchumba. Ikiwa wale wanaochumbiana wanavunja uchumba wao, hilo halimaanishi kwamba uchumba wao haukufanikiwa. Badala yake, uchumba huo umetimiza kusudi lake—umewasaidia kufikia uamuzi mzuri.

4. Kwa nini tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu uchumba?

4 Kwa nini ni muhimu tuwe na maoni yanayofaa kuhusu kipindi cha uchumba? Waseja wanapokuwa na maoni yanayofaa kuhusu uchumba, hawataanzisha uchumba ikiwa hawana nia ya kufunga ndoa. Hata hivyo, si waseja pekee wanaohitaji kuwa na mtazamo unaofaa. Sisi sote tunapaswa kusitawisha mtazamo huo. Kwa mfano, baadhi ya watu wanafikiri kwamba ikiwa watu wanachumbiana, ni lazima wafunge ndoa. Mtazamo huo unawaathirije Wakristo waseja? Melissa, dada mseja kutoka nchini Marekani, anasema hivi: “Mashahidi wanaochumbiana wanapata mkazo mwingi sana. Matokeo ni kwamba baadhi ya watu wanaochumbiana huepuka kuvunja uchumba hata ikiwa hawafaani. Waseja wengine wanaepuka kabisa kuanzisha uchumba. Mkazo huo unaweza kukulemea sana.”

JITAHIDINI KUFAHAMIANA VIZURI

5-6. Wale wanaochumbiana wanapaswa kujitahidi kujua nini kuhusu yule ambaye huenda akawa mwenzi wao wa ndoa? (1 Petro 3:4)

5 Ikiwa una mchumba, ni nini kitakachokusaidia kuamua ikiwa mtafunga ndoa au la? Jitahidini kufahamiana vizuri. Inaelekea kwamba ulichunguza na kujua baadhi ya mambo kumhusu mtu huyo kabla ya kuanzisha uchumba. Lakini sasa una fursa ya kumjua “yule mtu wa siri wa moyoni.” (Soma 1 Petro 3:4.) Hilo linahusisha kujua kuhusu hali ya kiroho, utu, na njia ya kufikiri ya yule unayetarajia awe mwenzi wako wa ndoa. Baada ya muda, unapaswa kuwa na majibu ya maswali kama vile: ‘Je, atakuwa mwenzi wa ndoa anayenifaa?’ (Met. 31:​26, 27, 30; Efe. 5:33; 1 Tim. 5:8) ‘Je, tunaweza kutimiziana mahitaji yetu ya kihisia? Je, ninaweza kuishi pamoja na mtu huyu licha ya mapungufu yake?’ b (Rom. 3:23) Mnapoendelea kufahamiana vizuri, kumbukeni jambo hili: Kujua ikiwa mnafaana au la, kunategemea kwa sehemu kubwa jinsi kila mmoja wenu anavyoshughulika na tofauti za mwenzake, na si jinsi mnavyopenda mambo yanayofanana.

6 Ni mambo gani mengine ambayo unapaswa kufahamu kumhusu mchumba wako wakati wa uchumba? Kabla hamjawa na hisia kali za kimahaba, huenda ungependa kuzungumza pamoja na mchumba wako kuhusu baadhi ya mambo muhimu, kama vile malengo yake. Lakini namna gani kuhusu mambo ya kibinafsi kama vile, afya yake, matatizo ya kiuchumi, au mambo mabaya ambayo huenda amepitia maishani? Si kila jambo linahitaji kuzungumziwa mwanzoni mwa uchumba. (Linganisha Yohana 16:12.) Ikiwa unahisi kwamba ni mapema mno kujibu baadhi ya maswali kuhusu mambo ya kibinafsi, mjulishe mchumba wako. Hata hivyo, baada ya muda, yule anayetarajia kuwa mwenzi wako wa ndoa atahitaji kujua habari hizo ili afanye uamuzi mzuri. Hivyo, utahitaji kuzungumza naye kwa unyoofu kuhusu mambo hayo.

7. Wale wanaochumbiana wanaweza kufahamiana vizuri jinsi gani? (Tazama sanduku “ Mchumba Wako Anapoishi Mbali.”) (Tazama pia picha.)

7 Unawezaje kujua vizuri jinsi mtu alivyo? Mojawapo ya njia bora za kufanya hivyo ni kwa kuzungumza waziwazi na kwa unyoofu, kuuliza maswali na kusikiliza kwa makini. (Met. 20:5; Yak. 1:19) Ili ufanikiwe kufanya hivyo, huenda mkahitaji kufanya mambo fulani pamoja ambayo yatawasaidia kuwa na mazungumzo. Mambo hayo ni kama vile kula pamoja, kutembea pamoja kwenye maeneo ya umma, na kuhubiri pamoja. Pia, mnaweza kufahamiana vizuri mnapotumia wakati pamoja na marafiki na familia. Zaidi ya hayo, panga mambo ya kufanya ambayo yatakusaidia kujua jinsi anavyotenda katika hali mbalimbali na akiwa na watu tofauti-tofauti. Ona jambo ambalo Aschwin, kutoka nchini Uholanzi alifanya. Anasema hivi kuhusu uchumba wake na Alicia: “Tulitafuta mambo ya kufanya ambayo yangetusaidia kufahamiana vizuri. Mara nyingi yalikuwa mambo madogo-madogo kama vile kutayarisha mlo pamoja au kufanya kazi fulani za nyumbani pamoja. Tulipofanya mambo hayo pamoja, tuliweza kuona sifa nzuri na udhaifu wa kila mmoja wetu.”

Ikiwa mtafanya mambo fulani pamoja ambayo yatawasaidia kuwa na mazungumzo, inaelekea mtafahamiana vizuri zaidi (Tazama fungu la 7-8)


8. Wale wanaochumbiana wanaweza kunufaikaje kwa kujifunza pamoja?

8 Pia, mnaweza kufahamiana vizuri kwa kujifunza kuhusu habari za kiroho pamoja. Ikiwa mtafunga ndoa, mtahitaji kutenga wakati kwa ajili ya ibada ya familia, ili kumfanya Mungu awe sehemu muhimu ya ndoa yenu. (Mhu. 4:12) Hivyo, kwa nini msitenge muda wa kujifunza pamoja sasa, wakati wa uchumba? Bila shaka, wale wanaochumbiana bado si familia, na ndugu bado hajawa kichwa cha dada. Hata hivyo, kwa kujifunza pamoja kwa ukawaida, utajua hali ya kiroho ya mchumba wako. Max na Laysa, wenzi wa ndoa kutoka nchini Marekani, walipata faida nyingine. Max anasema hivi: “Mwanzoni mwa uchumba wetu tulianza kujifunza machapisho yaliyohusu urafiki wa kimahaba, ndoa, na maisha ya familia. Machapisho hayo yalitupatia fursa ya kuzungumzia mambo mengi muhimu ambayo tusingeweza kuanza kuzungumzia katika mazungumzo ya kawaida.”

MAMBO MENGINE YA KUFIKIRIA

9. Wale wanaochumbiana wanapaswa kuzingatia mambo gani wanapoamua watamweleza nani kuhusu uchumba wao?

9 Mnapaswa kumjulisha nani kuhusu uchumba wenu? Huo ni uamuzi wenu ninyi wawili. Huenda mwanzoni mwa uchumba wenu mkaamua kuwajulisha watu wachache. (Met. 17:27) Mkifanya hivyo, huenda mtaepuka maswali mengi kuhusu uhusiano wenu na mkazo usio wa lazima. Hata hivyo, ikiwa hamtamwambia mtu yeyote, huenda mkajitenga na wengine kwa sababu mnaogopa kwamba watajua mna uhusiano. Hilo linaweza kuwa hatari. Hivyo, ni jambo la hekima kuwajulisha wale ambao wanaweza kuwapa ushauri mzuri na msaada hususa. (Met. 15:22) Kwa mfano, mnaweza kuwaambia baadhi ya watu wa familia, marafiki wakomavu, au wazee wa kutaniko.

10. Wale wanaochumbiana wanaweza kufanya nini ili uchumba wao uwe wenye kuheshimika? (Methali 22:3)

10 Mnawezaje kudumisha uchumba wenu ukiwa wenye kuheshimika? Kadiri hisia zenu zinavyoongezeka, ndivyo kila mmoja atakavyovutiwa zaidi na mwenzake. Ni nini kitakachowasaidia kudumisha usafi wa kiadili? (1 Kor. 6:18) Epukeni kuzungumzia mambo machafu kiadili, kubaki peke yenu, na kunywa kileo kupita kiasi. (Efe. 5:3) Mambo hayo yanaweza kuamsha tamaa ya ngono na kudhoofisha azimio lenu la kufanya yaliyo sawa. Kwa nini msizungumzie pamoja hatua mnazoweza kuchukua ili kudumisha uchumba wenu ukiwa wenye kuheshimika? (Soma Methali 22:3.) Ona kilichowasaidia Dawit na Almaz kutoka nchini Ethiopia. Wanasema hivi: “Tulitumia wakati pamoja tukiwa kwenye sehemu zenye watu wengi au tukiwa pamoja na marafiki wetu. Kamwe hatukuwahi kuwa peke yetu kwenye gari au ndani ya nyumba. Hivyo, tuliepuka hali ambazo zingetushawishi.”

11. Ni mambo gani ambayo wale wanaochumbiana wanapaswa kuzingatia kabla ya kuamua kuonyeshana upendo?

11 Namna gani kuhusu njia za kuonyeshana upendo? Huenda baadhi ya njia zikafaa kadiri uhusiano wenu unavyoendelea. Hata hivyo, ikiwa mtaamsha hamu ya ngono, huenda haitakuwa rahisi kufanya maamuzi ya hekima kuhusu mchumba wako. (Wim. 1:2; 2:6) Pia, kuonyeshana upendo kunaweza kufanya iwe rahisi zaidi kujiingiza katika mwenendo mpotovu. (Met. 6:27) Hivyo, mapema katika uhusiano wenu, zungumzieni mipaka ya kuonyeshana upendo mtakayojiwekea, kulingana na kanuni za Biblia. c (1 The. 4:​3-7) Jiulizeni hivi: ‘Watu katika eneo tunaloishi watahisije tukiamua kuonyeshana upendo? Je, matendo hayo yanaweza kuamsha hamu ya ngono?’

12. Wale wanaochumbiana wanapaswa kujua nini kuhusu matatizo na hali za kutoelewana wakati wa uchumba?

12 Mnawezaje kushughulikia matatizo na hali ya kutoelewana? Namna gani ikiwa hali ya kutoelewana inatokea pindi fulani? Je, hilo linamaanisha kwamba hamfaani? Si lazima iwe hivyo; wenzi wote huwa na hali za kutoelewana pindi fulani. Ndoa imara inahusisha watu wawili wanaoweza kufanya kazi pamoja ili kushinda tofauti zao. Hivyo, jinsi mnavyoshughulikia matatizo sasa kunaweza kuonyesha ikiwa ndoa yenu itafanikiwa au la. Jiulizeni hivi: ‘Je, tunaweza kuyazungumzia matatizo yetu kwa utulivu na heshima? Je, tuko tayari kukiri makosa yetu na kujitahidi kubadilika? Je, sisi ni wepesi wa kukubali maoni ya wengine, kuomba msamaha, na kusamehe?’ (Efe. 4:​31, 32) Hata hivyo, ikiwa mnashindwa kufanya makubaliano au mnabishana kwa ukawaida wakati wa uchumba, inaelekea kwamba hali hiyo haitakuwa bora mtakapofunga ndoa. Ikiwa utatambua kwamba mtu unayechumbiana naye hakufai, uamuzi wa kuvunja uchumba ndio utakuwa uamuzi bora kwenu nyote. d

13. Ni mambo gani yanayoweza kuwasaidia wachumba kuamua watachumbiana kwa muda gani?

13 Mnapaswa kuchumbiana kwa muda mrefu kadiri gani? Maamuzi ya haraka-haraka mara nyingi huwa na matokeo mabaya. (Met. 21:5) Hivyo, mnapaswa kuchumbiana kwa muda wa kutosha ili mfahamiane vizuri. Hata hivyo, hampaswi kuendelea kuchumbiana kwa muda mrefu isivyo lazima. Biblia pia inasema hivi: “Matarajio yaliyoahirishwa hufanya moyo uwe mgonjwa.” (Met. 13:12) Zaidi ya hilo, kadiri mnavyochumbiana kwa muda mrefu, ndivyo inavyokuwa vigumu kupinga kishawishi cha kufanya ngono. (1 Kor. 7:9) Badala ya kukazia fikira muda ambao mmekuwa mkichumbiana, unaweza kujiuliza hivi, ‘Ni mambo gani mengine ambayo bado ninahitaji kujua kumhusu mchumba wangu ili nifanye uamuzi?’

WENGINE WANAWEZAJE KUWAUNGA MKONO WALE WANAOCHUMBIANA?

14. Ni kwa njia gani hususa wengine wanaweza kuwasaidia wale wanaochumbiana? (Tazama pia picha.)

14 Ikiwa tunawafahamu watu fulani wanaochumbiana, tunawezaje kuwasaidia? Tunaweza kuwakaribisha kwa ajili ya mlo, ibada ya familia, au tafrija. (Rom. 12:13) Wakiwa katika pindi hizo, wanaweza kupata nafasi ya kufahamiana vizuri zaidi. Je, wanahitaji mtu wa kuandamana nao, usafiri, au mahali pa faragha ambapo wanaweza kuzungumza? Ikiwa ndivyo, je, tunaweza kuwasaidia? (Gal. 6:10) Alicia, aliyetajwa awali, anakumbuka jambo ambalo yeye na Aschwin walithamini. Anasema hivi: “Tuliguswa moyo wakati baadhi ya akina ndugu waliposema kwamba tungeweza kuwatembelea nyumbani ikiwa tungehitaji mahali pa kutumia wakati pamoja na ambapo hatungekuwa peke yetu.” Ikiwa utaombwa uandamane na watu wanaochumbiana, lione jambo hilo kuwa pendeleo. Uwe mwangalifu usiwaache wale wanaochumbiana peke yao kabisa, lakini pia jitahidi kutambua wanapohitaji wakati na nafasi ili wazungumze faraghani.—Flp. 2:4.

Ikiwa tunawafahamu watu fulani wanaochumbiana, tunaweza kutafuta njia hususa za kuwasaidia (Tazama fungu la 14-15)


15. Ni jambo gani lingine ambalo wengine wanaweza kufanya ili kuwasaidia wale wanaochumbiana? (Methali 12:18)

15 Pia, tunaweza kuwaunga mkono wale wanaochumbiana kupitia mambo tunayosema au kutosema. Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kujidhibiti. (Soma Methali 12:18.) Kwa mfano, huenda tukatamani kuwaeleza wengine kwamba ndugu na dada fulani wameanza kuchumbiana, lakini huenda ndugu na dada hao wangependa kuwaambia wengine jambo hilo wao wenyewe. Hatupaswi kupiga porojo au kuwachambua wale wanaochumbiana kuhusu mambo yao ya kibinafsi. (Met. 20:19; Rom. 14:10; 1 The. 4:11) Zaidi ya hilo, ndugu na dada hao huenda hawatafurahia kusikia maelezo au maswali yanayofanya wahisi wanashinikizwa kufunga ndoa. Dada anayeitwa Elise na mume wake wanakumbuka hivi: “Tuliaibika wengine walipotuuliza kuhusu mipango yetu ya harusi wakati sisi wenyewe hatukuwa tumeizungumzia.”

16. Tunapaswa kutendaje ikiwa wale wanaochumbiana wameamua kuvunja uchumba?

16 Namna gani ikiwa wale wanaochumbiana wanaamua kuvunja uchumba wao? Tunapaswa kuepuka kuwauliza maswali ya kibinafsi au kumlaumu mmoja wao kwa kuvunja uchumba. (1 Pet. 4:15) Dada anayeitwa Lea anasema hivi: “Nilisikia kwamba wengine walikuwa wakikisia-kisia kuhusu sababu iliyofanya mimi na ndugu fulani tuvunje uchumba wetu. Jambo hilo liliniumiza sana.” Kama ilivyotajwa mwanzoni, kuvunjika kwa uchumba hakumaanishi kwamba uchumba haukufanikiwa. Kwa kawaida, hilo linamaanisha kwamba uchumba umetimiza kusudi lake—umewasaidia wanaochumbiana kufanya uamuzi mzuri. Hata hivyo, huenda uamuzi huo ukawasababishia maumivu ya kihisia na kuwafanya wahisi upweke. Hivyo, tunaweza kutafuta njia za kuwategemeza.—Met. 17:17.

17. Wale wanaochumbiana wanapaswa kuendelea kufanya nini?

17 Kama tulivyoona, kipindi cha uchumba kinaweza kuwa na changamoto, lakini kinaweza pia kuwa chenye kufurahisha. Jessica anakumbuka hivi: “Kusema ukweli, kipindi cha uchumba kilihitaji jitihada nyingi. Lakini ninaweza kusema kwa asilimia 100 kwamba wakati na jitihada nilizotumia hazikuwa za bure.” Ikiwa mnachumbiana, endeleeni kujitahidi kufahamiana vizuri. Mkifanya hivyo, mtakuwa na uchumba wenye mafanikio —utakaowasaidia kufanya uamuzi wenye hekima.

WIMBO 49 Kufurahisha Moyo wa Yehova

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Ili kupata maswali zaidi ya kufikiria, tazama kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, uku. 39-40.

c Kupapasa-papasa viungo vya uzazi vya mtu mwingine ni namna ya uasherati inayohitaji wazee wa kutaniko wachukue hatua ya kihukumu. Kupapasa-papasa matiti na mazungumzo yasiyo ya kimaadili kupitia jumbe fupi au kwa njia ya simu pia yanaweza kuhusisha hatua za kihukumu, ikitegemea hali.

d Kwa habari zaidi, tazama makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1999.