MAKALA YA 18

WIMBO 1 Sifa za Yehova

Mtumaini “Mwamuzi wa Dunia Yote” Mwenye Rehema!

Mtumaini “Mwamuzi wa Dunia Yote” Mwenye Rehema!

“Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?”MWA. 18:25.

JAMBO KUU

Kuelewa kwa kina zaidi kuhusu rehema na haki ya Yehova kuhusiana na ufufuo wa watu wasio waadilifu.

1. Yehova alimfundisha Abrahamu somo gani lenye kufariji?

 YALIKUWA mazungumzo ambayo Abrahamu hakusahau kamwe. Kupitia malaika, Mungu alimwambia Abrahamu kwamba angeharibu majiji ya Sodoma na Gomora. Jambo hilo lilimhangaisha mwanamume huyo mwaminifu. Aliuliza hivi: “Je, kweli utamfagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu? . . . Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?” Kwa subira, Yehova alimfundisha rafiki yake mpendwa Abrahamu somo hili ambalo linatunufaisha na kutufariji sisi sote: Mungu hatawaharibu kamwe watu waadilifu.—Mwa. 18:​23-33.

2. Ni nini kinachotuhakikishia kwamba Yehova anahukumu kwa uadilifu na rehema?

2 Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Yehova anahukumu kwa uadilifu na rehema? Tunaweza kuwa na uhakika kwa sababu tunajua kwamba “Yehova huona ndani ya moyo” wa mtu. (1 Sam. 16:7) Kwa kweli, anaujua “moyo wa kila mwanadamu.” (1 Fal. 8:39; 1 Nya. 28:9) Jambo hilo linapendeza sana. Kwa kuwa Yehova ana hekima nyingi sana kuliko sisi, huenda sikuzote tusielewe kikamili hukumu zake. Kwa kufaa, mtume Paulo aliongozwa na roho kusema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika!”—Rom. 11:33.

3-4. Huenda nyakati nyingine tukajiuliza maswali gani, na ni mambo gani tutakayochunguza katika makala hii? (Yohana 5:​28, 29)

3 Ingawa tunajua kwamba sikuzote Yehova anafanya yaliyo sawa, huenda bado tukajiuliza maswali kama aliyouliza Abrahamu. Huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, kuna tumaini lolote la wakati ujao kwa watu kama wale waliohukumiwa katika majiji ya Sodoma na Gomora? Je, inawezekana kwamba baadhi yao watapata “ufufuo . . . wa wasio waadilifu”?’—Mdo. 24:15.

4 Acheni tujikumbushe mambo ambayo tunaelewa kuhusu ufufuo. Hivi karibuni, kulikuwa na marekebisho katika uelewaji wetu kuhusu “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu.” a (Soma Yohana 5:​28, 29.) Uelewaji huo uliorekebishwa umetokeza marekebisho mengine zaidi, ambayo yatazungumziwa katika makala hii na makala inayofuata. Kuhusiana na hukumu za uadilifu za Yehova, kwanza tutazungumzia mambo ambayo hatujui na kisha mambo ambayo tunajua.

MAMBO AMBAYO HATUJUI

5. Wakati uliopita, machapisho yetu yalisema nini kuhusu wale walioangamizwa katika majiji ya Sodoma na Gomora?

5 Wakati uliopita, machapisho yetu yalizungumzia kile kinachowapata watu ambao Yehova anawahukumu kuwa wasio waadilifu. Tulisema kwamba watu walioharibiwa na Yehova, kama wale wa Sodoma na Gomora, hawana tumaini la kufufuliwa wakati ujao. Lakini, baada ya kusali na kujifunza kwa kina, swali hili limejitokeza: Je, kweli tunaweza kusema hivyo kwa uhakika?

6. Kuna mifano gani ya hukumu za Yehova dhidi ya watu wasio waadilifu, na ni jambo gani ambalo hatujui?

6 Fikiria mifano ifuatayo inayotajwa katika Biblia. Masimulizi kadhaa ya Biblia yanazungumzia hukumu za Yehova dhidi ya watu wasio waadilifu, kama vile kuhusu idadi isiyojulikana ya watu waliokufa wakati wa Gharika, au yale mataifa saba katika Nchi ya Ahadi ambayo Yehova aliwaamuru watu wake wayaangamize, au kuhusu wanajeshi Waashuru 185,000 walioangamizwa na malaika wa Yehova katika usiku mmoja. (Mwa. 7:23; Kum. 7:​1-3; Isa. 37:​36, 37) Katika visa hivyo, je, Biblia inatupatia habari za kutosha kujua ikiwa Yehova aliwahukumu watu wote hao uharibifu wa milele bila kuwa na tumaini lolote la ufufuo? La, hasha! Kwa nini tunaweza kusema hivyo?

7. Ni mambo gani ambayo hatujui kuhusu watu waliouawa wakati wa Gharika au wakati Waisraeli waliposhinda majiji ya Kanaani? (Tazama picha)

7 Hatujui jinsi Yehova alivyomhukumu kila mmoja wao; wala hatujui ikiwa wale waliouawa walikuwa wamepata nafasi ya kujifunza kumhusu Yehova na kutubu. Kuhusiana na wakati wa Gharika, Biblia inasema kwamba Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5) Lakini Biblia haisemi kwamba alipokuwa akijenga safina kubwa, Noa alikuwa pia akijaribu kumhubiria kila mtu duniani kabla ya wakati wa Gharika. Vivyo hivyo, kuhusiana na yale mataifa ya Kanaani, hatujui ikiwa watu wote hao waovu walikuwa wamepata nafasi ya kujifunza kumhusu Yehova na kubadili njia zao.

Noa na familia yake wakijenga safina kubwa. Haijulikani ikiwa Noa alipanga kampeni ya kuhubiri wakati wa ujenzi wa safina ili kuwafikia watu wote duniani kabla ya Gharika kuja (Tazama fungu la 7)


8. Ni mambo gani ambayo hatujui kuhusu watu wa Sodoma na Gomora?

8 Namna gani kuhusu watu wa Sodoma na Gomora? Mwanamume mwadilifu, aliyeitwa Loti, aliishi miongoni mwao. Lakini je, tunajua ikiwa Loti aliwahubiria watu wote hao? La! Hapana shaka kwamba walikuwa waovu, lakini je, kila mmoja wao alijua mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa? Kumbuka kwamba umati wa wanaume katika jiji hilo ulitaka kuwabaka wageni wa Loti. Biblia inasema “kuanzia mvulana mpaka mzee,” wote walikuwa katika umati huo. (Mwa. 19:4; 2 Pet. 2:7) Je, kweli tunajua kwa uhakika kwamba Yehova Mungu mwenye rehema alimhukumu kila mmoja wao kifo bila kuwa na tumaini la ufufuo? Yehova alimhakikishia Abrahamu kwamba hakukuwa hata na waadilifu kumi katika jiji hilo. (Mwa. 18:32) Hivyo, walikuwa watu wasio waadilifu, na Yehova alikuwa na haki ya kuwaangamiza kwa sababu ya matendo yao. Je, tunaweza kusema kwa uhakika kwamba hakuna hata mmoja wao atakayefufuliwa katika “ufufuo . . . wa wasio waadilifu”? Hapana, hatuwezi kusema hivyo kwa uhakika!

9. Ni jambo gani ambalo hatujui kumhusu Sulemani?

9 Pia, kwa upande mwingine, katika Biblia tunasoma kuhusu masimulizi ya watu ambao walikuwa waadilifu lakini baadaye wakawa wasio waadilifu. Mfano mmoja ni wa Mfalme Sulemani. Alifundishwa kikamili njia za Mungu na alibarikiwa sana na Yehova; hata hivyo, baadaye aligeuka na kuanza kuabudu miungu ya uwongo. Dhambi zake zilimkasirisha Yehova na matokeo ya dhambi hizo yalidumu kwa mamia ya miaka. Ni kweli, Maandiko yanasema kwamba Sulemani ‘alizikwa pamoja na mababu zake,’ kutia ndani wanaume waaminifu kama vile Mfalme Daudi. (1 Fal. 11:​5-9, 43; 2 Fal. 23:13) Kwa kuwa Biblia inatumia maneno hayo kuhusu jinsi alivyozikwa, je, huo ni uhakikisho kwamba atafufuliwa? La! Biblia haisemi hivyo. Hata hivyo, huenda wengine wakasema kwamba “yule ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” (Rom. 6:7) Hilo ni kweli, lakini haimaanishi kwamba kila mtu aliyekufa atafufuliwa, kana kwamba kuishi tena ni haki ambayo kila mtu anastahili. Ufufuo ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo. Anawapatia zawadi hiyo wale ambao anataka wapate nafasi ya kumtumikia milele. (Ayu. 14:​13, 14; Yoh. 6:44) Je, Sulemani atapata zawadi hiyo ya ufufuo? Yehova ndiye anayejua; sisi hatujui. Hata hivyo, jambo tunalojua ni kwamba Yehova atafanya yaliyo sawa.

MAMBO AMBAYO TUNAJUA

10. Yehova anahisije kuhusu kuwaangamiza wanadamu? (Ezekieli 33:11) (Tazama pia picha.)

10 Soma Ezekieli 33:11. Kwa fadhili, Yehova anatufunulia jinsi anavyohisi kuhusu kuwahukumu wanadamu. Mtume Petro aliongozwa na roho kuandika maneno yanayofanana na yale ya nabii Ezekieli aliposema kwamba “Yehova . . . hataki yeyote aangamizwe.” (2 Pet. 3:9) Kwa sababu ya kweli hiyo inayotufariji, tunajua kwamba Yehova hachukui hatua haraka ya kuwaharibu watu milele. Yeye ni mwenye rehema nyingi sana, na anaonyesha rehema inapowezekana.

Katika ufufuo wa wasio waadilifu, watu wa aina mbalimbali watapata nafasi ya kujifunza kumhusu Yehova (Tazama fungu la 10)


11. Ni nani ambao hawatafufuliwa, na tunajuaje jambo hilo?

11 Tunajua nini kuhusu watu ambao hawatafufuliwa? Biblia inataja mifano michache tu. b Yesu alionyesha kwamba Yuda Iskariote hatafufuliwa. (Marko 14:21; tazama pia Yohana 17:12. c) Yuda alijua kwamba alikuwa akimpinga Yehova Mungu na Mwana Wake, lakini kwa makusudi aliamua kufanya hivyo. (Tazama Marko 3:29. d) Vivyo hivyo, Yesu alisema kwamba baadhi ya viongozi wa dini waliokuwa wakimpinga wangekufa bila kuwa na tumaini la ufufuo. (Mt. 23:33; the man habari za utafiti za Kiingereza kuhusu Yoh. 19:11 nwtsty.) Na mtume Paulo alionya kwamba waasi-imani wasiotubu hawangefufuliwa.—Ebr. 6:​4-8; 10:29.

12. Tunajua nini kuhusu rehema ya Yehova? Toa mifano.

12 Hata hivyo, tunajua nini kuhusu rehema ya Yehova? Ameonyeshaje kwamba “hataki yeyote aangamizwe”? Fikiria jinsi alivyowaonyesha rehema baadhi ya watu waliofanya dhambi nzito. Mfalme Daudi alifanya dhambi nyingi nzito, kutia ndani uzinzi na uuaji. Hata hivyo, Daudi alitubu, na kwa rehema Yehova alimsamehe. (2 Sam. 12:​1-13) Kwa sehemu kubwa ya maisha yake, Mfalme Manase alifanya mambo mengi maovu. Ingawa Manase alikuwa mwovu sana, Yehova aliitikia kwa njia nzuri alipotubu na akatafuta msingi wa kumwonyesha rehema na msamaha. (2 Nya. 33:​9-16) Mifano hiyo inatukumbusha kwamba Yehova anaonyesha rehema wakati wowote anapoona kuna msingi wa kufanya hivyo. Atawafufua watu kama hao kwa sababu walitambua kwamba walifanya dhambi nzito na wakatubu.

13. (a) Kwa nini Yehova aliwaonyesha rehema Waninawi? (b) Baadaye Yesu alisema nini kuhusu Waninawi?

13 Pia, tunajua kuhusu jinsi Yehova alivyowaonyesha rehema Waninawi. Mungu alimwambia Yona hivi: “Nimeona uovu wao.” Lakini walipotubu dhambi zao, kwa fadhili Yehova aliwasamehe. Na aliwaonyesha Waninawi rehema nyingi zaidi kuliko Yona alivyofanya. Mungu alihitaji kumkumbusha nabii wake mwenye hasira kwamba Waninawi hao “hawajui kutofautisha jema na baya.” (Yona 1:​1, 2; 3:10; 4:​9-11) Baadaye, Yesu alitumia mfano huo kufundisha kuhusu haki na rehema ya Yehova. Yesu alisema kwamba Waninawi hao waliotubu “watasimama katika hukumu.”—Mt. 12:41.

14. “Ufufuo wa hukumu” utamaanisha nini kwa Waninawi?

14 Waninawi “watasimama katika hukumu” gani? Yesu alifundisha kuhusu “ufufuo wa hukumu” wa wakati ujao. (Yoh. 5:29) Alikuwa akirejelea Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, kipindi ambacho “waadilifu na wasio waadilifu” watafufuliwa. (Mdo. 24:15) Kwa wasio waadilifu, huo utakuwa “ufufuo wa hukumu.” Yaani, Yehova na Yesu watachunguza na kuchanganua tabia zao na jinsi wanavyoitikia mafundisho yanayotoka kwa Yehova. Ikiwa Mninawi aliyefufuliwa atakataa kujiunga na ibada ya kweli, Yehova hatamruhusu aendelee kuishi. (Isa. 65:20) Lakini wale wote watakaochagua kumwabudu Yehova kwa uaminifu, watapata hukumu nzuri. Watakuwa na tumaini la kuishi milele!—Dan. 12:2.

15. (a) Kwa nini tunapaswa kuepuka kusema kwamba watu wote walioangamizwa katika majiji ya Sodoma na Gomora hawatafufuliwa? (b) Tunaweza kuelewaje maneno yaliyoandikwa kwenye Yuda 7? (Tazama sanduku “ Yuda Alimaanisha Nini?”)

15 Alipokuwa akizungumza kuhusu watu wa Sodoma na Gomora, Yesu alisema kwamba ingekuwa afadhali zaidi kwao “katika Siku ya Hukumu” kuliko ambavyo ingekuwa kwa watu ambao walimkataa Yesu na kukataa mafundisho yake. (Mt. 10:​14, 15; 11:​23, 24; Luka 10:12) Alimaanisha nini? Huenda tukahisi kwamba Yesu alitumia usemi uliotiwa chumvi katika kisa hiki. Lakini inaonekana Yesu hakuwa akitia chumvi alipowazungumzia watu wa Sodoma na Gomora, sawa tu na alipowazungumzia watu wa Ninawi. e Badala yake, inaonekana kwamba Yesu alikuwa akimaanisha kile alichokuwa akisema. “Siku ya Hukumu” aliyoirejelea katika visa vyote viwili, bila shaka ilikuwa siku ileile. Kama Waninawi, watu wa Sodoma na Gomora walifanya mambo mabaya. Lakini Waninawi walikuwa na nafasi ya kutubu. Isitoshe, kumbuka jambo ambalo Yesu alisema kuhusu “ufufuo wa hukumu.” Utawahusu pia “wale waliozoea kutenda maovu.” (Yoh. 5:29) Hivyo, inaonekana kwamba huenda kukawa na tumaini kwa baadhi ya watu wa Sodoma na Gomora. Inawezekana kwamba baadhi ya watu hao watafufuliwa, na huenda tukawa na nafasi ya kuwafundisha kumhusu Yehova na Yesu Kristo.

16. Tunajua nini kuhusu jinsi Yehova atakavyoamua ni nani atakayefufuliwa? (Yeremia 17:10)

16 Soma Yeremia 17:10. Mstari huo unatusaidia kueleza kwa ufupi mambo ambayo tunajua: Sikuzote Yehova ndiye ‘anayeuchunguza moyo, na kukagua mawazo ya ndani kabisa.’ Inapohusu ufufuo wa wakati ujao, kama ilivyo kawaida yake, “[atampa] kila mmoja kulingana na njia zake.” Yehova atakuwa thabiti inapohitajika, lakini ataonyesha rehema inapowezekana. Hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba mtu fulani hana tumaini la ufufuo, isipokuwa iwe tunajua kwamba hana tumaini hilo kwa sababu Biblia imesema hivyo!

“MWAMUZI WA DUNIA YOTE” ATATENDA “JAMBO LA HAKI”

17. Wanadamu ambao wamekufa wana tumaini gani la wakati ujao?

17 Mabilioni ya wanadamu wamekufa tangu Adamu na Hawa walipojiunga na Shetani na kumwasi Yehova Mungu. Kifo ni “adui” mbaya sana! (1 Kor. 15:26) Ni nini kitakachowapata watu wote hao waliokufa? Idadi ndogo ya wafuasi waaminifu wa Kristo, yaani, 144,000, watafufuliwa ili waweze kupata uhai usioweza kufa mbinguni. (Ufu. 14:1) Idadi kubwa ya wanaume na wanawake waaminifu waliompenda Yehova watarudishiwa uhai wakati wa “ufufuo wa waadilifu,” na wataishi milele duniani ikiwa wataendelea kuwa waadilifu katika Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo na wakati wa jaribu la mwisho. (Dan. 12:13; Ebr. 12:1) Pia, wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, “wasio waadilifu”—kutia ndani wale ambao hawakumtumikia kabisa Yehova au hata wale “waliozoea kutenda maovu”—watapewa nafasi ya kubadili njia zao na kuwa waaminifu. (Luka 23:​42, 43) Hata hivyo, baadhi ya wanadamu walikuwa waovu sana, na walikuwa wameazimia kabisa kumwasi Yehova na makusudi yake hivi kwamba Yehova aliamua hawatafufuliwa.—Luka 12:​4, 5.

18-19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kuhusu hukumu za Yehova kwa watu ambao wamekufa? (Isaya 55:​8, 9) (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

 

18 Je, tuna sababu nzuri za kuwa na uhakika kwamba Yehova anapowahukumu watu, sikuzote hukumu zake zote ni za haki? Ndiyo! Abrahamu alielewa vizuri kwamba Yehova ni “Mwamuzi wa dunia yote” ambaye ni mkamilifu, mwenye hekima yote, na mwenye rehema. Amemzoeza Mwana wake na kumkabidhi kazi yote ya kuhukumu. (Yoh. 5:22) Yehova na Mwana wake wanaweza kusoma mambo yaliyo moyoni mwa kila mwanadamu. (Mt. 9:4) Katika kila kisa, watafanya “jambo la haki”!

19 Acheni tuendelee kuazimia kumtumaini Yehova na maamuzi yake yote. Tunatambua kwamba sisi hatustahili kutoa hukumu—lakini yeye anastahili! (Soma Isaya 55:​8, 9.) Kwa hiyo, tukiwa na uhakika, tunamwachia kazi yote ya kuhukumu yeye na Mwana wake, Mfalme ambaye anaiga kikamilifu haki na rehema ya Baba yake. (Isa. 11:​3, 4) Hata hivyo, namna gani kuhusu jinsi Yehova na Yesu watakavyowahukumu watu wakati wa dhiki kuu? Ni mambo gani ambayo hatujui? Na ni mambo gani ambayo tunajua? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.

WIMBO 57 Kuwahubiria Watu wa Namna Zote

a Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 2022, uku. 14-19.

b Kuhusu Adamu, Hawa, na Kaini, tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2013, uku. 12, maelezo ya chini.

c Msemo “mwana wa maangamizi” uliotumiwa kwenye Yohana 17:12 ulimaanisha kwamba Yuda Iskariote alipokufa angepatwa na uharibifu wa milele, bila kuwa na tumaini la ufufuo.

d Kwa habari zaidi tazama makala kwenye jw.org yenye kichwa “Dhambi Isiyoweza Kusamehewa Ni Nini?”

e Usemi uliotiwa chumvi ni usemi unaotumiwa kimakusudi kukuza jambo kuliko jinsi lilivyo kihalisi ili kukazia jambo kuu, lakini anayetumia usemi huo hatarajii ueleweke kama ulivyo. Hivyo, maelezo ya Yesu kuhusu watu wa Sodoma na Gomora yalikuwa halisi, si usemi uliotiwa chumvi.