MAKALA YA 36

Beba Majukumu Muhimu, Ondoa Uzito Usio wa Lazima

Beba Majukumu Muhimu, Ondoa Uzito Usio wa Lazima

“Acheni sisi pia tuondoe kila uzito . . . , na tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”​—EBR. 12:1.

WIMBO 33 Mtupie Yehova Mzigo Wako

MUHTASARI a

1. Kulingana na Waebrania 12:1, tunahitaji kufanya nini ili tufaulu kufika mwisho wa mbio za uzima?

 BIBLIA inalinganisha maisha yetu tukiwa Wakristo na mbio. Wakimbiaji ambao wanafaulu kumaliza mbio hizi wanapewa zawadi ya uzima wa milele. (2 Tim. 4:7, 8) Tunahitaji kufanya kila jitihada ili tuendelee kukimbia, hasa kwa sababu tumekaribia sana kufika mwisho wa mbio hizo. Mtume Paulo, ambaye alifaulu kumaliza mbio za uzima, alitaja mambo ambayo yanaweza kutusaidia kushinda mbio hizo. Alituagiza “tuondoe kila uzito na . . . tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”​—Soma Waebrania 12:1.

2. Inamaanisha nini ‘kuondoa kila uzito’?

2 Paulo alipoandika kwamba tunapaswa ‘kuondoa kila uzito,’ je, alimaanisha kuwa hakuna majukumu ambayo Mkristo anapaswa kubeba? Hapana, hakumaanisha hivyo. Badala yake, alimaanisha kwamba tunapaswa kuondoa kila uzito usio wa lazima. Uzito huo usio wa lazima unaweza kufanya tupunguze mwendo na kusababisha tuchoke. Ili tuvumilie, tunapaswa kutambua haraka na kuondoa mzigo wowote usio wa lazima ambao unaweza kufanya tupunguze mwendo wetu. Hata hivyo, hatungependa kupuuza majukumu ambayo tunapaswa kubeba. Ikiwa tutayapuuza, hatutastahili kushiriki katika mbio za uzima. (2 Tim. 2:5) Ni majukumu gani ambayo tunapaswa kubeba?

3. (a) Kulingana na Wagalatia 6:5, tunapaswa kubeba nini? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii, na kwa nini?

3 Soma Wagalatia 6:5. Paulo alitaja jambo fulani ambalo ni lazima tubebe. Aliandika kwamba “kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.” Hapa Paulo alirejelea mzigo wa majukumu yetu ya kibinafsi mbele za Mungu, mzigo ambao sisi wenyewe tunapaswa kuubeba. Katika makala hii, tutachunguza ‘mzigo wetu wenyewe’ unahusisha nini na jinsi tunavyoweza kuubeba. Pia, tutazungumzia mizigo isiyo ya lazima ambayo huenda tunabeba na kujifunza jinsi tunavyoweza kuiondoa. Kubeba mizigo yetu wenyewe na kuondoa uzito usio wa lazima kutatusaidia tufaulu kukimbia mbio za uzima hadi mwisho.

MIZIGO AMBAYO TUNAPASWA KUBEBA

Kubeba majukumu yetu kunatia ndani kuishi kulingana na ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu kwa Yehova, kutimiza majukumu yetu katika familia, na kuwajibika kwa sababu ya matokeo ya maamuzi yetu (Tazama fungu la 4 hadi 9)

4. Kwa nini ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu si mzigo mzito? (Tazama pia picha.)

4 Ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu. Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba tutamwabudu yeye na kufanya mapenzi yake. Ni lazima tutimize ahadi hiyo. Kuishi kulingana na wakfu wetu ni jukumu zito, lakini si mzigo mzito. Ni kwa sababu Yehova alituumba ili tufanye mapenzi yake. (Ufu. 4:11) Alituumba tukiwa na uhitaji wa kiroho na pia alituumba kwa mfano wake. Matokeo ni kwamba tunaweza kumkaribia na kufurahia kufanya mapenzi yake. (Zab. 40:8) Isitoshe tunapofanya mapenzi ya Mungu na kumfuata Mwana wake, sisi wenyewe ‘tunapata burudisho.’​—Mt. 11:28-30.

(Tazama fungu la 4-5)

5. Ni nini kitakachokusaidia utimize ahadi uliyotoa ulipojiweka wakfu? (1 Yohana 5:3)

5 Unawezaje kuubeba mzigo huo? Kuna mambo mawili yanayoweza kukusaidia. Kwanza, endelea kuimarisha upendo wako kwa Yehova. Unaweza kufanya hivyo kwa kutafakari kuhusu mambo yote mazuri ambayo amekufanyia na baraka za wakati ujao ambazo amekuahidi. Kadiri upendo wako kwa Yehova unavyozidi kukua, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwako kumtii. (Soma 1 Yohana 5:3.) Pili, mwige Yesu. Alifaulu kufanya mapenzi ya Mungu kwa sababu alisali kwa Yehova ili kupata msaada na akakazia fikira zawadi ambayo angepata. (Ebr. 5:7; 12:2) Kama Yesu, mwombe Yehova akupe nguvu na uendelee kuweka tumaini la uzima wa milele wazi kabisa akilini mwako. Upendo wako kwa Yehova unapozidi kukua na ukimwiga Mwana wake, utafaulu kutimiza ahadi uliyotoa ulipojiweka wakfu.

6. Kwa nini tunapaswa kutimiza majukumu yetu katika familia? (Tazama pia picha.)

6 Majukumu yetu katika familia. Katika mbio zetu za uzima, tunapaswa kumpenda Yehova na Yesu kuliko tunavyowapenda watu wetu wa ukoo. (Mt. 10:37) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba tunaweza kupuuza majukumu yetu katika familia kana kwamba yanatuzuia kufanya mambo yanayomfurahisha Mungu na Kristo. Kinyume chake, ili tumfurahishe Mungu na Kristo, tunahitaji kutimiza daraka letu katika familia. (1 Tim. 5:4, 8) Tunapofanya hivyo, tunakuwa wenye furaha zaidi. Kwa kweli, Yehova alikusudia familia ziwe na furaha mume na mke wanapotendeana kwa upendo na heshima, wazazi wanapowapenda na kuwazoeza watoto wao, na watoto wanapowatii wazazi wao.​—Efe. 5:33; 6:1, 4.

(Tazama fungu la 6-7)

7. Unawezaje kutimiza jukumu lako katika familia?

7 Unawezaje kuubeba mzigo huo? Hata uwe na jukumu gani katika familia, tegemea hekima inayopatikana katika Biblia badala ya kuongozwa tu na hisia zako, utamaduni, au mambo ambayo yanasemwa na wale wanaoitwa wataalamu. (Met. 24:3, 4) Tumia vizuri machapisho yanayotegemea Biblia. Machapisho hayo yana mapendekezo yanayofaa ya jinsi ya kutumia kanuni za Biblia. Kwa mfano, mfululizo wa makala wenye kichwa “Msaada kwa Ajili ya Familia” una habari kuhusu changamoto hususa ambazo wenzi wa ndoa, wazazi, na matineja wanakabili leo. b Azimia kufuata mambo ambayo Biblia inasema, hata ikiwa watu wengine katika familia hawafanyi hivyo. Ukifanya hivyo, familia yenu itanufaika na utafurahia baraka za Yehova.​—1 Pet. 3:1, 2.

8. Maamuzi yetu yanaweza kutuathirije?

8 Kuwajibika kwa sababu ya maamuzi yetu. Yehova ametupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua, na anataka tupate furaha inayotokana na kufanya maamuzi mazuri. Lakini pia hatukingi dhidi ya matokeo ya maamuzi mabaya tunayofanya. (Gal. 6:7, 8) Kwa hiyo, tunakubali matokeo mabaya tunayopata kwa sababu ya maamuzi tuliyofanya, kuzungumza bila kufikiri, na kutenda kwa kimbelembele. Ikitegemea jambo tulilofanya, huenda tukasumbuliwa na dhamiri yenye hatia. Hata hivyo, kutambua kwamba tunawajibika kwa sababu ya maamuzi yetu, kunaweza kutuchochea tuungame dhambi zetu, turekebishe makosa yetu, na tuepuke kurudia makosa hayo. Kuchukua hatua kama hizo kunaweza kutusaidia tuendelee kukimbia katika mbio za uzima.

(Tazama fungu la 8-9)

9. Ni nini kitakachokusaidia kukabiliana na matokeo ya uamuzi mbaya? (Tazama pia picha.)

9 Unawezaje kuubeba mzigo huo? Ikiwa umefanya uamuzi mbaya, kubali hali yako ya sasa. Tambua kwamba huwezi kubadili mambo yaliyotokea wakati uliopita. Usipoteze muda na nguvu zako ukijaribu kujitetea au kujilaumu au kuwalaumu wengine kwa sababu ya uamuzi wako mbaya. Badala yake, kubali makosa yako, na ujitahidi kufanya yote unayoweza ili kuboresha hali yako. Ikiwa unahisi hatia kwa sababu ya kosa ulilofanya, sali kwa Yehova kwa unyenyekevu, kubali kosa lako, na umwombe akusamehe. (Zab. 25:11; 51:3, 4) Waombe msamaha wale ambao huenda umewakosea, na ikihitajika, utafute msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko. (Yak. 5:14, 15) Jifunze kutokana na makosa yako na ujitahidi kutoyarudia. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuonyesha rehema na kukupatia msaada ambao unahitaji.​—Zab. 103:8-13.

UZITO AMBAO TUNAPASWA ‘KUUONDOA’

10. Kwa nini matarajio yasiyo halisi yanaweza kuwa mzigo mzito? (Wagalatia 6:4)

10 Matarajio yasiyo halisi. Tunaweza kujiongezea mzigo mzito kwa kuwa na matarajio yasiyo halisi ikiwa tutajilinganisha na wengine. (Soma Wagalatia 6:4.) Ikiwa sikuzote tunajilinganisha na wengine, tunaweza kuanza kuoneana wivu na kushindana. (Gal. 5:26) Ili kujaribu kufanya mambo ambayo wengine wametimiza, huenda tukajitahidi sana kufanya mambo yanayopita uwezo wetu, au ambayo yanazidi hali zetu. Na kwa kuwa “matarajio yaliyoahirishwa hufanya moyo uwe mgonjwa,” tutavunjika moyo hata zaidi ikiwa tutajiwekea matarajio ambayo hatuwezi kamwe kuyatimiza! (Met. 13:12) Kufanya hivyo, kunaweza kufanya tuchoke na kupunguza mwendo katika mbio zetu za uzima.​—Met. 24:10.

11. Ni nini kinachoweza kukusaidia uepuke matarajio yasiyo halisi?

11 Unawezaje kuuondoa uzito huo? Usitarajie kutimiza mengi kuliko yale ambayo Yehova anataka ufanye. Hatarajii kamwe umpe kile ambacho huna. (2 Kor. 8:12) Uwe na uhakika kwamba Yehova halinganishi mambo unayofanya na yale ambayo wengine wanafanya. (Mt. 25:20-23) Anathamini utumishi wako wa moyo wote, uaminifu wako, na uvumilivu wako. Uwe mwenye kiasi na kukubali kwamba huenda usiweze kutimiza mengi kwa sababu ya umri, afya, au hali zako. Kama Barzilai, uwe tayari kukataa mapendeleo fulani ikiwa hali yako ya kimwili inakuzuia kutimiza mapendeleo hayo. (2 Sam. 19:35, 36) Kama Musa, kubali msaada na uwape wengine majukumu inapofaa. (Kut. 18:21, 22) Kuwa mwenye kiasi kutakusaidia usiwe na matarajio yasiyo halisi ambayo yanaweza kukufanya uchoke katika mbio za uzima.

12. Je, tunawajibika kwa sababu ya maamuzi mabaya ambayo wengine wanafanya? Eleza.

12 Kuhisi kwamba unawajibika kwa sababu ya maamuzi mabaya ambayo wengine wanafanya. Hatuwezi kuwafanyia wengine maamuzi; wala hatuwezi sikuzote kuwalinda wasipatwe na matokeo ya maamuzi mabaya wanayofanya. Kwa mfano, huenda mwana au binti akaamua kuacha kumtumikia Yehova. Uamuzi huo unaweza kuwasababishia wazazi wake huzuni nyingi. Hata hivyo, wazazi ambao wanajilaumu kwa sababu ya uamuzi mbaya wa mtoto wao, wanabeba mzigo mzito sana. Yehova hataki wabebe mzigo huo.​—Rom. 14:12.

13. Mzazi anaweza kushughulikiaje uamuzi mbaya wa mtoto wake?

13 Unawezaje kuuondoa uzito huo? Kumbuka kwamba Yehova ametupatia sisi sote zawadi ya uhuru wa kuchagua. Anamruhusu kila mtu ajifanyie maamuzi yake. Hilo linatia ndani kuamua ikiwa tutamtumikia. Yehova anajua kwamba wewe si mzazi mkamilifu; anataka tu ujitahidi kufanya yote unayoweza. Uamuzi ambao mtoto wako anafanya ni jukumu lake, si jukumu lako. (Met. 20:11) Ingawa hivyo, huenda ukahangaishwa na makosa uliyofanya ukiwa mzazi. Ikiwa ndivyo, mweleze Yehova jinsi unavyohisi na umwombe msamaha. Anajua kwamba huwezi kubadili mambo yaliyotokea wakati uliopita. Wakati huohuo, hatarajii kwamba umlinde mtoto wako asivune kile ambacho amepanda. Kumbuka kwamba ikiwa mtoto wako atafanya jitihada za kumrudia Yehova, atakuwa tayari kumkaribisha.​—Luka 15:18-20.

14. Kwa nini tunapaswa kuondoa uzito wa kuhisi hatia kupita kiasi?

14 Kuhisi hatia kupita kiasi. Baada ya kutenda dhambi, ni jambo la kawaida kuhisi hatia. Hata hivyo, hatupaswi kuendelea kubeba uzito wa kuhisi hatia kupita kiasi. Tunapaswa kuondoa uzito huo. Tunawezaje kujua ikiwa tunahisi hatia kupita kiasi? Ikiwa tuliungama dhambi yetu, tukatubu, na tunachukua hatua ili kuepuka kurudia dhambi hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ametusamehe. (Mdo. 3:19) Baada ya kuchukua hatua hizo, Yehova hangependa tuendelee kuhisi hatia. Anajua madhara yanayoweza kutokea ikiwa tutaendelea kuhisi hatia. (Zab. 31:10) Ikiwa tutalemewa na huzuni, huenda tukaacha kukimbia mbio za uzima.​—2 Kor. 2:7.

Baada ya kutubu kikweli, Yehova haendelei kufikiria kuhusu dhambi zako, nawe hupaswi kuendelea kuzifikiria (Tazama fungu la 15)

15. Ni nini kinachoweza kukusaidia ushinde hisia za kuwa na hatia kupita kiasi? (1 Yohana 3:19, 20) (Tazama pia picha.)

15 Unawezaje kuuondoa uzito huo? Ikiwa unaendelea kuhisi hatia kupita kiasi, kazia fikira “msamaha wa kweli” unaotoka kwa Mungu. (Zab. 130:4) Anapowasamehe wale wanaotubu kwa unyoofu, anaahidi hivi: “Sitaikumbuka tena dhambi yao.” (Yer. 31:34) Hilo linamaanisha kwamba baada ya hapo, Yehova hatakumbuka tena dhambi ulizofanya wakati uliopita. Basi, usifikiri matokeo mabaya ya dhambi yako yanathibitisha kwamba bado hajakusamehe. Na usijikasirikie kwa sababu makosa yako ya zamani yanakuzuia kufanya mengi katika utumishi wa Yehova. Yehova haendelei kufikiria kuhusu dhambi zako, nawe hupaswi kufanya hivyo.​—Soma 1 Yohana 3:19, 20.

KIMBIA ILI USHINDE

16. Tukiwa wakimbiaji, tunapaswa kutambua jambo gani?

16 Tukiwa wakimbiaji katika mbio za uzima, tunapaswa ‘kukimbia kwa njia itakayotuwezesha kushinda tuzo.’ (1 Kor. 9:24) Tunaweza kufanya hivyo ikiwa tutatambua tofauti kati ya majukumu ambayo tunapaswa kubeba na uzito ambao tunapaswa kuuondoa. Katika makala hii, tumezungumzia mifano michache tu ya majukumu ambayo tunapaswa kubeba, na uzito ambao tunapaswa kuuondoa. Lakini kuna mizigo mingine pia. Yesu alisema kwamba tunaweza ‘kulemewa na kula na kunywa kupita kiasi na mahangaiko ya maisha.’ (Luka 21:34) Andiko hilo na maandiko mengine, yanaweza kukusaidia utambue mabadiliko ambayo huenda unahitaji kufanya unapokimbia katika mbio za uzima.

17. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutashinda mbio za uzima?

17 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutashinda mbio za uzima kwa sababu Yehova atatupatia nguvu tunazohitaji. (Isa. 40:29-31) Kwa hiyo, usipunguze mwendo! Mwige mtume Paulo ambaye alijitahidi kabisa kupata tuzo iliyokuwa mbele yake. (Flp. 3:13, 14) Hakuna mtu anayeweza kukimbia mbio hizo kwa ajili yako, lakini kwa msaada wa Yehova unaweza kufanikiwa. Yehova anaweza kukusaidia ubebe majukumu yako na kuondoa uzito usio wa lazima. (Zab. 68:19) Yehova akiwa upande wako, utafaulu kukimbia katika mbio kwa uvumilivu na kushinda!

WIMBO 65 Songa Mbele!

a Makala hii itatusaidia kukimbia mbio za uzima. Tukiwa wakimbiaji, ni lazima tubebe majukumu fulani. Majukumu hayo yanatia ndani ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu kwa Yehova, majukumu katika familia, na kuwajibika kwa sababu ya maamuzi tunayofanya. Lakini ni lazima tuondoe uzito wowote usio wa lazima unaoweza kufanya tupunguze mwendo. Hilo linatia ndani nini? Makala hii itajibu swali hilo.

b Unaweza kupata mfululizo wa makala “Msaada kwa Ajili ya Familia” kwenye jw.org. Baadhi ya makala zinazopatikana kwa ajili ya wenzi wa ndoa ni “Jinsi ya Kuonyesha Heshima” na “Jinsi ya Kuonyesha Uthamini”; kwa ajili ya wazazi, “Kuwafundisha Watoto Kutumia Simu ya Mkononi kwa Busara” na “Jinsi ya Kuwasiliana na Kijana Wako”; na kwa ajili ya matineja, “Jinsi ya Kuepuka Kushinikizwa na Marafiki” na “Jinsi ya Kukabiliana na Upweke.”