MAKALA YA 33

Jifunze Kutokana na Mfano wa Danieli

Jifunze Kutokana na Mfano wa Danieli

“Wewe ni mtu mwenye thamani sana.”​—DAN. 9:23.

WIMBO 73 Tupe Ujasiri

MUHTASARI a

1. Kwa nini Wababiloni walipendezwa na nabii Danieli?

 NABII Danieli alikuwa kijana Wababiloni walipomfanya kuwa mfungwa na kumpeleka nchi ya mbali huko Babiloni. Lakini ni wazi kwamba Danieli aliwafurahisha wale waliomchukua mateka. Waliona kile “kinachoonekana kwa macho”​—kwamba Danieli ‘hakuwa na kasoro yoyote, alikuwa mzuri kwa umbo’ na alitoka kwenye familia mashuhuri. (1 Sam. 16:7) Kutokana na sababu hizo, Wababiloni walimzoeza ili atumikie kwenye makao ya mfalme.​—Dan. 1:3, 4, 6.

2. Yehova alihisije kumhusu Danieli? (Ezekieli 14:14)

2 Yehova alimpenda Danieli, si kwa sababu ya mwonekano wake au kwa sababu alitumikia kwenye makao ya mfalme, bali kwa sababu ya sifa alizoamua kusitawisha. Kwa kweli, huenda Danieli alikuwa mwishoni mwa miaka yake ya utineja au mwanzoni mwa miaka yake ya 20, Yehova alipomtaja kwa njia nzuri pamoja na Noa na Ayubu, wanaume ambao walikuwa wamemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi. (Mwa. 5:32; 6:9, 10; Ayu. 42:16, 17; soma Ezekieli 14:14.) Na Yehova aliendelea kumpenda Danieli katika maisha yake yote marefu yenye mambo ya kustaajabisha.​—Dan. 10:11, 19.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutachunguza sifa mbili za Danieli ambazo zilimfanya awe mwenye thamani kwa Yehova. Kwanza, tutafafanua kila sifa na kuchunguza pindi ambazo alionyesha sifa hizo. Kisha, tutaona jinsi Danieli alivyojifunza kusitawisha sifa hizo. Mwishowe, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kumwiga. Ingawa makala hii inawahusu vijana, sisi sote tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Danieli.

IGA UJASIRI WA DANIELI

4. Danieli alionyeshaje ujasiri? Toa mfano.

4 Huenda watu wenye ujasiri wakapatwa na woga, lakini hawaruhusu woga uwazuie kufanya mambo yanayofaa. Danieli alikuwa kijana mwenye ujasiri sana. Fikiria pindi mbili ambazo alionyesha ujasiri. Inaelekea kwamba pindi ya kwanza ilikuwa miaka miwili baada ya Wababiloni kuharibu jiji la Yerusalemu. Mfalme Nebukadneza wa Babiloni aliota ndoto yenye kutisha kuhusu sanamu kubwa sana. Alitishia kuwaua wanaume wake wote wenye hekima, kutia ndani Danieli, ikiwa hawangemwambia ndoto aliyoota na pia ufafanuzi wake. (Dan. 2:3-5) Danieli alihitaji kutenda haraka; la sivyo, watu wengi wangekufa. Alienda “na kumwomba mfalme ampe muda ili amweleze maana ya ndoto yake.” (Dan. 2:16) Hilo lilihitaji ujasiri na imani. Biblia haina habari zozote zinazoonyesha kwamba Danieli alikuwa amewahi kufafanua ndoto kabla ya wakati huo. Aliwaomba rafiki zake—ambao majina yao ya Kibabiloni yalikuwa Shadraki, Meshaki, na Abednego—“wasali ili Mungu wa mbinguni awaonyeshe rehema na kuwajulisha siri hiyo.” (Dan. 2:18) Yehova alijibu sala hizo. Kwa msaada wa Mungu, Danieli alifafanua ndoto ya Nebukadneza. Uhai wa Danieli na rafiki zake uliokolewa.

5. Ni wakati gani mwingine Danieli alihitaji kuonyesha ujasiri?

5 Muda fulani baada ya Danieli kufafanua ndoto ya ile sanamu kubwa sana, ujasiri wake ulijaribiwa tena. Nebukadneza aliota ndoto nyingine yenye kutisha. Ndoto hiyo ilihusu mti mkubwa sana. Kwa ujasiri, Danieli alimfafanulia mfalme maana ya ndoto hiyo, kutia ndani ujumbe kwamba mfalme huyo angekuwa mwenda-wazimu na kupoteza cheo chake cha kuwa mfalme kwa kipindi fulani. (Dan. 4:25) Ingekuwa rahisi kwa mfalme kumwona Danieli kuwa mwasi kwa kutangaza ujumbe huo na hata kuagiza Danieli auawe. Lakini Danieli alionyesha ujasiri na kutangaza ujumbe huo.

6. Huenda ni nini kilichomsaidia Danieli awe jasiri?

6 Huenda ni nini kilichomsaidia Danieli awe jasiri katika maisha yake yote? Alipokuwa mtoto, Danieli aliiga mfano mzuri wa baba na mama yake. Bila shaka, walikuwa wametii maagizo ambayo Yehova aliwapatia wazazi Waisraeli, na walimfundisha mtoto wao Sheria ya Mungu. (Kum. 6:6-9) Danieli hakujua mambo ya msingi tu kuhusu Sheria, kama vile zile amri kumi, bali pia alijua habari nyingi kuhusu chakula ambacho Mwisraeli angeweza kula au kutokula. b (Law. 11:4-8; Dan. 1:8, 11-13) Pia, Danieli alijifunza kuhusu historia ya watu wa Mungu na alijua kilichowapata walipokosa kuishi kulingana na viwango vya Yehova. (Dan. 9:10, 11) Mambo ambayo Danieli alijionea katika maisha yake yote, yalimpa uhakika kwamba Yehova na malaika Wake wenye nguvu walikuwa wakimsaidia.​—Dan. 2:19-24; 10:12, 18, 19.

Danieli alisitawisha ujasiri kwa kujifunza, kusali, na kumtumaini Yehova (Tazama fungu la 7)

7. Ni nini kingine kilichomsaidia Danieli awe mwenye ujasiri? (Tazama pia picha.)

7 Danieli alijifunza mambo ambayo manabii wa Mungu waliandika, kutia ndani unabii wa Yeremia. Kutokana na mambo aliyojifunza, baadaye alitambua kwamba utekwa wa muda mrefu wa Wayahudi huko Babiloni ulikuwa karibu kwisha. (Dan. 9:2) Danieli alipoona unabii wa Biblia ukitimizwa, bila shaka hilo lilimsaidia kumtumaini Yehova hata zaidi, na wale wanaomtumaini Mungu kabisa wanaweza kuwa na ujasiri mwingi. (Linganisha Waroma 8:31, 32, 37-39.) Jambo muhimu zaidi, Danieli alisali kwa Baba yake wa mbinguni mara nyingi. (Dan. 6:10) Aliungama dhambi zake kwa Yehova na akamweleza hisia zake. Na Danieli aliomba msaada. (Dan. 9:4, 5, 19) Alikuwa mwanadamu kama sisi, basi, hakuzaliwa akiwa jasiri. Badala yake, alisitawisha sifa hiyo kupitia kujifunza, kusali, na kumtumaini Yehova.

8. Tunawezaje kusitawisha ujasiri?

8 Tunahitaji kufanya nini ili tusitawishe ujasiri? Huenda wazazi wetu wakatuhimiza tuwe jasiri, lakini hatuwezi kurithi sifa hiyo kutoka kwao kana kwamba ni mali ya familia yetu. Kupata ujasiri ni kama kujifunza ustadi mpya. Njia moja ya kuboresha ustadi huo ni kwa kutazama kwa makini matendo ya mwalimu, kisha kuiga mfano wake. Vivyo hivyo, tunajifunza kuwa jasiri kwa kutazama kwa makini jinsi wengine wanavyoonyesha sifa hiyo, kisha kuiga mfano wao. Basi, tumejifunza nini kutokana na Danieli. Kama yeye, tunahitaji kulifahamu vizuri Neno la Mungu. Tunapaswa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa kuzungumza naye kwa uhuru na mara nyingi. Na tunahitaji kumtumaini Yehova, na kusadiki kwamba sikuzote atatusaidia. Kisha imani yetu itakapojaribiwa, tutakuwa na ujasiri.

9. Tunanufaikaje kwa kuwa na ujasiri?

9 Tunanufaika kwa njia kadhaa kwa kuwa na ujasiri. Fikiria kisa cha Ben. Alisoma katika shule fulani huko Ujerumani ambapo kila mtu aliamini fundisho la mageuzi na kufikiri kwamba simulizi la uumbaji katika Biblia ni hadithi ya kutungwa. Siku moja, Ben alipewa nafasi ya kusimama mbele ya darasa na kueleza kwa nini anaamini kwamba uhai uliumbwa. Kwa ujasiri alizungumza kuhusu imani yake. Matokeo yalikuwaje? Ben anasema hivi: “Mwalimu alisikiliza kwa makini na akachapisha nakala za habari ambayo nilitumia ili kuunga mkono imani yangu, kisha akampa nakala kila mwanafunzi darasani.” Wanafunzi wenzake waliitikiaje? Ben anasema hivi: “Wengi wao walisikiliza mambo niliyosema, na wakasema kwamba wamefurahishwa nami.” Kama kisa cha Ben kinavyoonyesha, mara nyingi watu wanaoonyesha ujasiri huheshimiwa na wengine. Pia, huenda wakawasaidia watu wenye mioyo minyoofu wamjue Yehova. Bila shaka, tuna sababu nzuri za kusitawisha ujasiri.

IGA USHIKAMANIFU WA DANIELI

10. Ushikamanifu ni nini?

10 Katika Biblia, neno la Kiebrania linalomaanisha “ushikamanifu” au “upendo mshikamanifu,” linatokeza wazo la uhusiano mchangamfu wenye upendo ambao mara nyingi unafafanua upendo ambao Mungu huwaonyesha watumishi wake. Neno hilohilo pia linatumiwa kufafanua upendo ambao watumishi wa Mungu huonyeshana. (2 Sam. 9:6, 7) Ushikamanifu wetu unaweza kuimarika kadiri muda unavyopita. Fikiria jinsi hilo lilivyothibitika kuwa kweli kwa Danieli.

Yehova amthawabisha Danieli kwa sababu ya kuwa mshikamanifu kwa kumtuma malaika na kufunga vinywa vya simba (Tazama fungu la 11)

11. Ushikamanifu wa Danieli ulijaribiwaje alipokuwa amezeeka? (Tazama picha kwenye jalada.)

11 Ushikamanifu wa Danieli kwa Yehova ulijaribiwa katika maisha yake yote. Lakini alijaribiwa kwa njia kubwa zaidi alipokuwa na zaidi ya umri wa miaka 90. Kufikia wakati huo, jiji la Babiloni lilikuwa limeshindwa na Wamedi na Waajemi na lilitawaliwa na Mfalme Dario. Maofisa wa makao ya mfalme hawakumpenda Danieli na hawakumheshimu Mungu ambaye Danieli alimwabudu. Basi, walipanga njama ili Danieli auawe. Walimwomba mfalme atoe agizo ambalo lingeonyesha ikiwa Danieli alikuwa mshikamanifu kwa Mungu wake au kwa mfalme. Ili Danieli athibitishe kwamba alikuwa mshikamanifu kwa mfalme na awe sawa na watu wengine, alihitaji kuacha kusali kwa Yehova kwa siku 30. Danieli hakulegeza msimamo wake. Matokeo ni kwamba alitupwa katika shimo la simba. Lakini Yehova alithawabisha ushikamanifu wa Danieli kwa kumwokoa kutoka katika vinywa vya simba. (Dan. 6:12-15, 20-22) Tunawezaje kuendelea kuwa washikamanifu sikuzote kwa Yehova kama alivyofanya Danieli?

12. Danieli aliendeleaje kuwa mshikamanifu sikuzote kwa Yehova?

12 Kama ilivyotajwa awali, ushikamanifu unatokana na upendo wenye nguvu. Danieli aliendelea kuwa mshikamanifu sikuzote kwa Yehova kwa sababu alimpenda sana Baba yake wa mbinguni. Bila shaka, Danieli alisitawisha upendo huo kwa kufikiria kuhusu sifa za Yehova na kutafakari jinsi Yehova alivyozionyesha. (Dan. 9:4) Pia, Danieli alitafakari kwa uthamini kuhusu mambo yote mazuri ambayo Yehova alikuwa amemfanyia yeye na watu Wake.​—Dan. 2:20-23; 9:15, 16.

Kama Danieli, unaweza kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova sikuzote kwa kumpenda sana (Tazama fungu la 13)

13. (a) Vijana wetu wanakabili majaribu gani ya ushikamanifu? Toa mfano. (Tazama pia picha.) (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye video, unaweza kujibuje wengine wanapokuuliza ikiwa Mashahidi wa Yehova wanawaunga mkono wale wanaoamua kujihusisha katika ngono za watu wa jinsia moja?

13 Kama Danieli, vijana wetu wamezungukwa na watu ambao hawamheshimu Yehova na viwango vyake. Huenda watu hao wakamchukia mtu yeyote anayesema kwamba anampenda Mungu. Wengine hata hujaribu kuwashinikiza vijana wetu ili wavunje ushikamanifu wao kwa Yehova. Kwa mfano, fikiria jambo lililompata kijana anayeitwa Graeme, anayeishi nchini Australia. Alikabili hali ngumu alipokuwa kwenye shule ya sekondari. Mwalimu aliwauliza wanafunzi jinsi ambavyo wangetenda ikiwa rafiki yao angewaambia kwamba anajihusisha na ngono za watu wa jinsia moja. Mwalimu akasema kwamba wanafunzi wote darasani ambao wangemuunga mkono rafiki anayeishi maisha hayo wanapaswa kusimama upande mmoja wa darasa na ambao hawangemuunga mkono wasimame upande wa pili. Graeme anasema hivi: “Wanafunzi wote darasani walisimama upande wa wale ambao wangemuunga mkono isipokuwa mimi na Shahidi mwingine.” Jambo lililofuata lilijaribu sana ushikamanifu wa Graeme kwa Yehova. Anasema hivi: “Kwa muda uliobaki wa somo hilo lenye urefu wa saa moja, wale wanafunzi wengine na hata mwalimu walitudhihaki na kututukana. Nilijitahidi kabisa kuitetea imani yangu kwa njia ya upole na yenye usawaziko, lakini hawakunisikiliza kamwe.” Graeme alihisije alipokabili jaribu hilo la ushikamanifu? Anasema hivi: “Sikufurahia wanafunzi wenzangu waliponitukana, lakini nilifurahi sana kwamba nilifaulu kuitetea imani yangu bila kulegeza msimamo.” c

14. Tunawezaje kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova sikuzote?

14 Tunaweza kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova sikuzote, ikiwa kama Danieli, tutasitawisha upendo mwingi kumwelekea Yehova. Tunasitawisha upendo kama huo kwa kujifunza kuhusu sifa za Yehova. Kwa mfano, tunaweza kujifunza kuhusu vitu ambavyo aliumba. (Rom. 1:20) Ikiwa ungependa kuimarisha upendo na heshima yako kumwelekea Yehova, unaweza kusoma makala fupi kwenye mfululizo “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” au utazame video zake. Pia, unaweza kusoma habari zilizo kwenye broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai. Ona jambo ambalo dada mmoja kijana anayeitwa Esther, kutoka nchini Denmark anasema kuhusu machapisho hayo: “Yanafafanua mambo kwa njia nzuri sana. Broshua hizo hazikuambii mambo unayopaswa kuamini; badala yake, zinaeleza sababu na kukuruhusu ufanye uamuzi.” Ben, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Broshua hizo ziliimarisha sana imani yangu. Zilinithibitishia kwamba Mungu aliumba uhai.” Baada ya kujifunza habari hizo, inaelekea kwamba utakubaliana na Biblia inaposema hivi: “Unastahili, Ee Yehova Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote.”​—Ufu. 4:11. d

15. Ni nini kingine kinachoweza kukusaidia kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova?

15 Njia nyingine ya kuimarisha upendo wetu kumwelekea Yehova ni kwa kuchunguza kwa makini maisha ya Yesu, Mwana wake. Dada kijana anayeitwa Samira, anayeishi nchini Ujerumani, alifanya hivyo. Anasema hivi: “Nilimfahamu Yehova vizuri zaidi kupitia Yesu.” Alipokuwa mtoto, ilikuwa vigumu kwa Samira kuelewa kwamba Yehova ana hisia. Lakini alielewa jinsi Yesu alivyohisi. Anaongezea hivi: “Nilimpenda Yesu kwa sababu alikuwa mwenye urafiki na aliwapenda watoto.” Kadiri alivyozidi kujifunza kumhusu Yesu, ndivyo alivyozidi kumpenda Yehova. Kwa nini? Anasema hivi: “Hatua kwa hatua nilielewa kwamba Yesu anamwiga kikamili Baba yake. Utu wao unafanana sana. Nilitambua kwamba hiyo ndiyo sababu moja iliyomfanya Yehova amtume Yesu duniani, ili kufanya iwezekane kwa wanadamu kumfahamu Yehova vizuri zaidi.” (Yoh. 14:9) Ikiwa ungependa kuimarisha urafiki wako pamoja na Yehova, kwa nini usitumie muda kujifunza mambo mengi iwezekanavyo kumhusu Yesu? Ukifanya hivyo, utaimarisha upendo na ushikamanifu wako kwa Yehova.

16. Tunanufaikaje kwa kuwa washikamanifu? (Zaburi 18:25; Mika 6:8)

16 Tunapokuwa washikamanifu kwa wengine, mara nyingi tunasitawisha urafiki wa karibu na wenye kudumu pamoja nao. (Rut. 1:14-17) Isitoshe, watu ambao ni washikamanifu kwa Yehova wanakuwa na utulivu na kuridhika. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anaahidi kuwa mshikamanifu kwa wale walio washikamanifu kwake. (Soma Zaburi 18:25; Mika 6:8.) Fikiria jambo hili—Muumba mweza-yote yuko tayari kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja nasi! Na tunapokuwa na urafiki huo, hakuna jambo ambalo linaweza kuvunja uhusiano huo iwe ni jaribu, upinzani, au hata kifo. (Dan. 12:13; Luka 20:37, 38; Rom. 8:38, 39) Ni muhimu sana kwetu kumwiga Danieli na kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova!

ENDELEA KUJIFUNZA KUTOKANA NA DANIELI

17-18. Ni nini kingine tunachoweza kujifunza kutoka kwa Danieli?

17 Katika makala hii, tumechunguza sifa mbili tu kati ya sifa nyingi za Danieli. Lakini kuna mengi zaidi tunayoweza kujifunza kutoka kwake. Kwa mfano, Yehova alimpatia Danieli mfululizo wa maono na ndoto, na akampa uwezo wa kufafanua ujumbe wa kinabii. Tayari unabii mwingi kati ya huo umetimizwa. Unabii mwingine unahusu matukio ya wakati ujao ambayo yatamwathiri kila mtu aliye duniani.

18 Katika makala inayofuata, tutachunguza masimulizi mawili ya kinabii yaliyorekodiwa na Danieli. Kuelewa unabii huo kunaweza kutusaidia sisi sote, vijana na wazee, tufanye maamuzi ya hekima sasa. Unabii huo pia unaweza kuimarisha ujasiri na ushikamanifu wetu ili tuwe tayari kushinda majaribu yatakayotokea hivi karibuni.

WIMBO 119 Lazima Tuwe na Imani

a Leo, vijana wanaomtumikia Yehova wanakabili changamoto ambazo zinajaribu ujasiri na ushikamanifu wao kwa Yehova. Huenda wanafunzi wenzao wakawadhihaki kwa sababu wanaamini uumbaji. Au huenda vijana wenzao wakajaribu kuwafanya wajione kuwa wapumbavu kwa sababu wanamtumikia Mungu na kuishi kulingana na viwango vyake. Lakini kama tutakavyoona kwenye makala hii, wale wanaomwiga nabii Danieli na kumtumikia Yehova kwa ujasiri na ushikamanifu, kwa kweli ni wenye hekima.

b Inawezekana kwamba Danieli alikuwa na sababu tatu zilizomfanya aone chakula cha Wababiloni kuwa kisicho safi: (1) Huenda walikula nyama ya wanyama waliokatazwa kwenye Sheria. (Kum. 14:7, 8) (2) Huenda nyama hiyo haikutolewa damu vizuri. (Law. 17:10-12) (3) Huenda kula chakula hicho kungeonwa kuwa kushiriki ibada ya miungu ya uwongo.​—Linganisha Mambo ya Walawi 7:15 na 1 Wakorintho 10:18, 21, 22.

c Tazama video “Matokeo ya Uadilifu wa Kweli Yatakuwa Amani” kwenye jw.org.

d Ili uimarishe upendo wako kwa Yehova, pia unaweza kujifunza kitabu Mkaribie Yehova, ambacho kinazungumzia kwa undani sifa na utu wa Yehova.