MAKALA YA 34

Jifunze Kutokana na Unabii wa Biblia

Jifunze Kutokana na Unabii wa Biblia

“Wale walio na ufahamu wataelewa.”​—DAN. 12:10.

WIMBO 98 Maandiko—Yaliongozwa na Roho ya Mungu

MUHTASARI a

1. Ni kinachoweza kutusaidia kufurahia kujifunza unabii wa Biblia?

 NDUGU kijana anayeitwa Ben anasema hivi: “Ninapenda kujifunza kuhusu unabii wa Biblia.” Je, unakubaliana naye? Au je, unahisi kwamba ni vigumu kujifunza kuhusu unabii? Hata huenda ukahisi kwamba inachosha kujifunza kuhusu unabii. Hata hivyo, unapojifunza kwa nini Yehova aliagiza unabii uandikwe katika Neno lake, huenda ukaanza kupendezwa na unabii.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Katika makala hii, hatutazungumzia tu kwa nini tunapaswa kujifunza unabii wa Biblia, bali pia jinsi tunavyoweza kujifunza unabii huo. Kisha tutachunguza masimulizi mawili ya kinabii katika kitabu cha Danieli na tutaona jinsi kuelewa unabii huo kunavyoweza kutusaidia leo.

KWA NINI TUJIFUNZE KUHUSU UNABII WA BIBLIA?

3. Tunahitaji kufanya nini ili tuelewe unabii wa Biblia?

3 Tunahitaji kuomba msaada ili tuelewe unabii wa Biblia. Fikiria mfano ufuatao. Wazia kwamba unatembelea eneo fulani ambalo hulifahamu, lakini rafiki yako ambaye mnasafiri pamoja analielewa vizuri eneo hilo. Anajua kabisa mahali mlipo na anajua kila barabara katika eneo hilo. Bila shaka, utafurahi kwamba rafiki yako alikubali kusafiri pamoja nawe! Vivyo hivyo, Yehova anajua mahali tulipo katika mkondo wa wakati na mambo yatakayotokea wakati ujao. Basi, ili kuelewa unabii wa Biblia, tunapaswa kumwomba Yehova msaada kwa unyenyekevu.​—Dan. 2:28; 2 Pet. 1:19, 20.

Kujifunza kuhusu unabii wa Biblia kunaweza kutusaidia tujitayarishe kwa ajili ya matukio ya wakati ujao (Tazama fungu la 4)

4. Kwa nini Yehova aliagiza unabii uandikwe katika Neno lake? (Yeremia 29:11) (Tazama pia picha.)

4 Kama mzazi mwenye upendo, Yehova anataka watoto wake wawe na wakati ujao wenye furaha. (Soma Yeremia 29:11.) Lakini tofauti na wazazi wa kibinadamu, Yehova anaweza kutabiri kuhusu wakati ujao kwa usahihi kabisa. Aliagiza unabii uandikwe katika Neno lake ili tujue matukio muhimu kabla hayajatokea. (Isa. 46:10) Unabii mbalimbali wa Biblia ni zawadi za upendo kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Lakini unawezaje kuwa na uhakika kwamba mambo ambayo Biblia inatabiri kwa kweli yatatimia?

5. Vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Max?

5 Mara nyingi vijana wetu wanapokuwa shuleni, wanazungukwa na watu ambao hawaiheshimu Biblia. Mambo wanayosema na mwenendo wao unaweza kusababisha shaka katika akili za vijana walio Mashahidi. Fikiria kisa cha ndugu anayeitwa Max. Anasema hivi: “Nilipokuwa tineja nilianza kutilia shaka ikiwa wazazi wangu wananifundisha dini ya kweli na ikiwa kweli Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.” Wazazi wake walifanya nini? Anasema hivi: “Waliitikia kwa upole, hata ingawa nilijua kwamba walikuwa na wasiwasi.” Wazazi wa Max walijibu maswali yake kwa kutumia Biblia. Max pia alichukua hatua fulani. Anasema hivi: “Nilijifunza unabii wa Biblia mimi mwenyewe na nikazungumzia mambo niliyojifunza pamoja na vijana wengine.” Matokeo yalikuwaje? Max anasema hivi: “Baada ya hapo, nilisadiki kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu!”

6. Unahitaji kufanya nini ikiwa una shaka, na kwa nini?

6 Ikiwa kama Max, unaanza kutilia shaka kuwa Biblia inafundisha ukweli, huhitaji kuhisi hatia. Lakini unahitaji kuchukua hatua haraka. Shaka ni kama kutu. Kutu inapopuuzwa, inaweza kuharibu kitu chenye thamani. Ili uanze kuondoa “kutu” yoyote iliyo kwenye imani yako, unahitaji kujiuliza hivi: ‘Je, ninaamini mambo ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao?’ Ikiwa huna uhakika, basi unahitaji kujifunza unabii wa Biblia ambao tayari umetimizwa. Unawezaje kufanya hivyo?

JINSI YA KUJIFUNZA UNABII WA BIBLIA

Ili tumtumaini Yehova kama Danieli alivyofanya, tunapaswa kujifunza unabii wa Biblia kwa unyenyekevu, kwa makini, na tukiwa na nia nzuri (Tazama fungu la 7)

7. Danieli aliweka mfano gani kuhusu jinsi ya kujifunza unabii? (Danieli 12:10) (Tazama pia picha.)

7 Danieli alituwekea mfano mzuri kuhusu jinsi ya kujifunza unabii. Alichunguza unabii akiwa na nia nzuri, alitaka kujua ukweli. Pia, Danieli alikuwa mnyenyekevu, alitambua kwamba Yehova huwapatia uelewaji wale wanaomfahamu na wanaoishi kulingana na viwango vyake safi. (Dan. 2:27, 28; soma Danieli 12:10.) Danieli alithibitisha kwamba alikuwa mnyenyekevu kwa kumtegemea Yehova ili amsaidie. (Dan. 2:18) Pia, Danieli alijifunza kwa makini. Alifanya utafiti katika Maandiko yaliyoongozwa na roho ambayo yalipatikana wakati huo. (Yer. 25:11, 12; Dan. 9:2) Unawezaje kumwiga Danieli?

8. Kwa nini baadhi ya watu hawaamini kwamba unabii wa Biblia unatimia, lakini tunapaswa kufanya nini?

8 Chunguza nia yako. Je, unajifunza unabii wa Biblia kwa sababu unatamani sana kujua ukweli? Ikiwa ndivyo, Yehova atakusaidia. (Yoh. 4:23, 24; 14:16, 17) Watu wengine hujifunza wakiwa na nia gani? Baadhi yao hujifunza wakitumaini watapata uthibitisho unaoonyesha kwamba Biblia haijaongozwa na roho ya Mungu. Wanapofanya hivyo, wanahisi kwamba wana haki ya kujiwekea viwango vyao wenyewe kuhusu mambo yanayofaa na yasiyofaa na kuishi kulingana na viwango hivyo. Hata hivyo, tunahitaji kujifunza tukiwa na nia nzuri. Isitoshe, tunahitaji sifa fulani muhimu ili kuelewa unabii wa Biblia.

9. Tunahitaji sifa gani ili kuelewa unabii wa Biblia? Eleza.

9 Uwe mnyenyekevu. Yehova anaahidi kwamba atawasaidia wanyenyekevu. (Yak. 4:6) Basi, tunahitaji kumwomba atusaidie kuelewa unabii wa Biblia. Pia, tunapaswa kukubali kwamba tunahitaji msaada wa mtumwa mwaminifu ambaye Yehova anamtumia kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Luka 12:42) Yehova ni Mungu mwenye utaratibu, basi inapatana na akili kuamini kwamba anatumia chanzo kimoja tu ili kutusaidia kuelewa kweli zilizo katika Neno lake.​—1 Kor. 14:33; Efe. 4:4-6.

10. Unajifunza nini kutokana na kisa cha Esther?

10 Jifunze kwa makini. Chagua unabii ambao unaupenda, kisha ufanye utafiti kuhusu unabii huo. Hivyo ndivyo alivyofanya dada anayeitwa Esther. Alipendezwa na unabii uliotabiri kuhusu kuja kwa Masihi. Anasema hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilianza kufanya utafiti ili kuthibitisha kwamba kwa kweli unabii huo uliandikwa kabla ya Yesu kuja duniani.” Alipata uthibitisho alipojifunza kuhusu Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi. Anasema hivi: “Baadhi ya vitabu hivyo viliandikwa kabla ya wakati wa Kristo. Basi unabii ulio katika vitabu hivyo ulitoka kwa Mungu.” Esther anakiri hivi: “Nilihitaji kusoma baadhi ya mambo mara kadhaa ili kuyaelewa.” Lakini anafurahi kwamba alifanya jitihada hizo. Baada ya kujifunza kwa makini unabii mbalimbali wa Biblia anasema hivi: “Nilijionea waziwazi kwamba Biblia inafundisha ukweli!”

11. Tunanufaikaje tunapojithibitishia wenyewe kwamba Biblia inafundisha ukweli?

11 Tunapoona jinsi ambavyo tayari baadhi ya unabii katika Neno la Mungu umetimizwa, tunamtumaini Yehova hata zaidi na mwongozo tunaopata kutoka kwake. Isitoshe, unabii wa Biblia unatusaidia kudumisha tumaini zuri kuhusu wakati ujao, hata iwe tunakabili majaribu gani sasa. Acheni tuchunguze kwa ufupi masimulizi mawili ya unabii yaliyoandikwa na Danieli, ambayo yanatimizwa leo. Kuelewa unabii huo kunaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima.

UNABII WA NYAYO ZA CHUMA NA UDONGO WA MFINYANZI UNAKUHUSUJE?

12. Nyayo za ‘chuma kilichochanganyika na udongo laini wa mfinyanzi’ zinafananisha nini? (Danieli 2:41-43)

12 Soma Danieli 2:41-43. Katika ndoto ambayo Danieli alimfafanulia Mfalme Nebukadneza, nyayo za sanamu ambayo mfalme aliona zilikuwa za ‘chuma kilichochanganyika na udogo laini wa mfinyanzi.’ Kwa kulinganisha unabii huo na unabii mwingine katika kitabu cha Danieli na Ufunuo, tunaweza kufikia mkataa kwamba nyayo hizo zinafananisha Muungano wa Uingereza na Marekani, serikali kuu ya ulimwengu inayotawala leo. Kuhusu serikali hiyo kuu ya ulimwengu, Danieli alisema kwamba ufalme huo utakuwa na “nguvu kwa sehemu na kuwa dhaifu kwa sehemu.” Kwa nini utakuwa dhaifu kwa sehemu? Kwa sababu watu wa kawaida, wanaofananishwa na udongo laini wa mfinyanzi, wanadhoofisha uwezo wake wa kutenda kama chuma. b

13. Tunajifunza kweli gani muhimu kwa kuelewa unabii huo?

13 Kutokana na ufafanuzi wa Danieli kuhusu ndoto ya ile sanamu na hasa nyayo zake, tunajifunza kweli fulani muhimu. Kwanza, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani imeonyesha nguvu zake kwa njia fulani. Kwa mfano, muungano wa nchi hizo ulikuwa kati ya mataifa yaliyoshinda Vita vya Kwanza vya Ulimwengu na Vita vya Pili vya Ulimwengu. Hata hivyo, serikali hiyo kuu ya ulimwengu imedhoofishwa na itaendelea kudhoofishwa na mizozo kati ya raia wake. Pili, muungano wa nchi hizo ndio serikali kuu ya mwisho ya ulimwengu itakayotawala kabla Ufalme wa Mungu haujakomesha falme zote za wanadamu. Ingawa huenda mataifa mengine yakaipinga Serikali Kuu ya Uingereza na Marekani, hayawezi kuchukua nafasi ya serikali hiyo. Tunajua hivyo kwa sababu “jiwe” linalofananisha Ufalme wa Mungu litaponda nyayo, sehemu ya sanamu hiyo inayofananisha muungano wa Uingereza na Marekani.​—Dan. 2:34, 35, 44, 45.

14. Kuelewa unabii kuhusu nyayo za chuma na udongo wa mfinyanzi kunawezaje kutusaidia tufanye maamuzi yenye hekima?

14 Je, unasadiki kwamba unabii wa Danieli kuhusu nyayo za chuma na udongo wa mfinyanzi ni wa kweli? Ikiwa ndivyo, jambo hilo litakusaidia kuamua jinsi utakavyoishi maisha yako. Utaepuka kukazia fikira kujikusanyia vitu vya kimwili katika ulimwengu ambao utaangamizwa hivi karibuni. (Luka 12:16-21; 1 Yoh. 2:15-17) Kuelewa unabii huo kutakusaidia uelewe umuhimu wa kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Mt. 6:33; 28:18-20) Baada ya kujifunza unabii huo, unaweza kujiuliza swali hili: ‘Je, maamuzi ninayofanya yanaonyesha ninasadiki kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za wanadamu?’

“MFALME WA KASKAZINI” NA “MFALME WA KUSINI” WANAKUHUSUJE?

15. Leo “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” ni nani? (Danieli 11:40)

15 Soma Danieli 11:40. Danieli sura ya 11 inazungumza kuhusu wafalme wawili, au serikali za kisiasa ambazo zinashindana kuutawala ulimwengu. Kwa kulinganisha unabii huo na unabii mwingine katika Biblia, tunaweza kusema kwamba “mfalme wa kaskazini” ni serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono. Na “mfalme wa kusini” ni Muungano wa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. c

Tunaweza kuimarisha imani yetu na kuepuka kuwa na wasiwasi ikiwa tutatambua kwamba upinzani kutoka kwa “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” unatimiza unabii wa Biblia (Tazama fungu la 16 hadi 18)

16. “Mfalme wa kaskazini” anawatendeaje watu wa Mungu?

16 Watu wa Mungu wanaoishi chini ya utawala wa “mfalme wa kaskazini” wanateswa moja kwa moja na mfalme huyo. Baadhi ya Mashahidi wamepigwa na kufungwa gerezani kwa sababu ya imani yao. Badala ya kuwafanya waogope, mateso ya “mfalme wa kaskazini” dhidi ya ndugu zetu yameimarisha imani yao. Kwa nini? Kwa sababu ndugu zetu wanajua kwamba watu wa Mungu wanapoteswa, hilo linatimiza unabii uliotolewa na Danieli. d (Dan. 11:41) Kujua jambo hilo kunaweza kutusaidia kuwa na tumaini imara na kudumisha utimilifu wetu.

17. Watu wa Mungu wamekabili changamoto gani chini ya utawala wa “mfalme wa kusini”?

17 Wakati uliopita “mfalme wa kusini” pia aliwashambulia moja kwa moja watu wa Yehova. Kwa mfano, katika miaka 50 ya kwanza ya karne ya 20, ndugu wengi walifungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote na baadhi ya watoto wa Mashahidi walifukuzwa shuleni kwa sababu hiyohiyo. Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, watumishi wa Yehova wanaoishi chini ya utawala wa mfalme huyo wamekabili mashambulizi yasiyo ya moja kwa moja kuelekea ushikamanifu wao kwa Ufalme wa Mungu. Kwa mfano, wakati wa kampeni za uchaguzi, huenda Mkristo akashawishiwa kuunga mkono chama fulani cha kisiasa au mgombeaji fulani. Huenda Mkristo asifikie hatua ya kupiga kura; lakini katika akili na moyo wake anaweza kuunga mkono upande fulani. Ni jambo muhimu kwamba tuendelee kutounga mkono upande wowote kisiasa, si kwa matendo tu, bali pia katika mawazo na hisia zetu!—Yoh. 15:18, 19; 18:36.

18. Tunatendaje inapohusu mzozo kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini”? (Tazama pia picha.)

18 Wale ambao hawaamini unabii wa Biblia huenda wakapatwa na wasiwasi mwingi wanapoona “mfalme wa kusini” ‘akimenyana’ na “mfalme wa kaskazini.” (Dan. 11:40, maelezo ya chini) Wafalme wote wawili wana silaha za kutosha za nyuklia zinazoweza kuangamiza uhai wote duniani. Lakini tunajua kwamba Yehova hataruhusu jambo hilo litokee. (Isa. 45:18) Basi, badala ya kutuletea wasiwasi, mzozo kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” unaimarisha imani yetu. Unathibitisha kwamba mwisho wa mfumo huu umekaribia.

ENDELEA KUKAZIA UANGALIFU UNABII

19. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu unabii wa Biblia?

19 Hatujui jinsi baadhi ya unabii wa Biblia utakavyotimizwa. Hata nabii Danieli hakuelewa maana ya kila jambo aliloandika. (Dan. 12:8, 9) Lakini kwa kuwa hatujui kikamili jinsi unabii fulani utakavyotimizwa, hilo halimaanishi kwamba hautatimizwa. Bila shaka, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatufunulia mambo tunayohitaji kujua kwa wakati unaofaa, kama alivyofanya zamani.​—Amo. 3:7.

20. Ni unabii gani wa Biblia wenye kusisimua ambao tutaona ukitimizwa hivi karibuni, na tunapaswa kuendelea kufanya nini?

20 Tangazo la “amani na usalama” litatolewa. (1 The. 5:3) Kisha serikali za kisiasa za ulimwengu zitashambulia dini za uwongo na kuziangamiza. (Ufu. 17:16, 17) Kisha zitashambulia watu wa Mungu. (Eze. 38:18, 19) Matukio hayo yataongoza moja kwa moja kwenye vita vya mwisho vya Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16) Tunaweza kuwa na hakika kwamba matukio hayo yatatokea hivi karibuni. Kabla wakati huo haujafika, acheni tuendelee kuonyesha uthamini wetu kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo kwa kukazia uangalifu unabii wa Biblia na kuwasaidia wengine wafanye hivyo pia.

WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

a Hata hali zizidi kuwa mbaya kadiri gani ulimwenguni, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutakuwa na wakati ujao wenye furaha. Tunapata uhakika huo kwa kujifunza unabii wa Biblia. Makala hii itazungumzia sababu hususa zinazoonyesha kwa nini tunapaswa kujifunza mambo ambayo Biblia ilitabiri. Pia, tutachunguza kwa ufupi masimulizi mawili ya unabii ambayo Danieli aliandika na kuona jinsi tunavyoweza kunufaika kibinafsi kwa kuyaelewa.

b Tazama makala “Yehova Anafunua Mambo Ambayo ‘Lazima Yatendeke Upesi,’” fu. 7-9, katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 2012.

c Tazama makala “‘Mfalme wa Kaskazini’ Ni Nani Leo?,” fu. 3-4, katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 2020.

d Tazama makala “‘Mfalme wa Kaskazini’ Ni Nani Leo?,” fu. 7-9, katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 2020.