MAKALA YA 7

Jinsi Unavyoweza Kunufaika Zaidi Unaposoma Biblia

Jinsi Unavyoweza Kunufaika Zaidi Unaposoma Biblia

“Wewe unasomaje?”​—LUKA 10:26.

WIMBO 97 Uhai Unategemea Neno la Mungu

MUHTASARI a

1. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu aliyaona Maandiko kuwa muhimu?

 WAZIA jinsi ilivyokuwa kumsikiliza Yesu akifundisha. Mara nyingi alinukuu Maandiko kutoka katika kumbukumbu yake! Kwa kweli, katika maneno yake ya kwanza baada ya kubatizwa na katika baadhi ya maneno yake ya mwisho kabla ya kifo chake, Yesu alinukuu Maandiko. b (Kum. 8:3; Zab. 31:5; Luka 4:4; 23:46) Na katika kipindi cha miaka mitatu na nusu iliyokuwa kati ya matukio hayo mawili, mara nyingi Yesu alisoma na kunukuu Maandiko hadharani na kuyafafanua.​—Mt. 5:17, 18, 21, 22, 27, 28; Luka 4:16-20.

Katika maisha yake yote, Yesu alionyesha kwamba aliyapenda Maandiko na aliruhusu yaongoze matendo yake (Tazama fungu la 2)

2. Yesu alipoendelea kukua, ni nini kilichomsaidia kuelewa vizuri Maandiko? (Tazama picha kwenye jalada.)

2 Miaka mingi kabla ya kuanza huduma yake, Yesu alisoma na kulisikia Neno la Mungu mara nyingi. Akiwa nyumbani, bila shaka alimsikia Maria na Yosefu wakinukuu Maandiko katika mazungumzo ya kila siku kwenye familia yao. c (Kum. 6:6, 7) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu alienda kwenye sinagogi kila siku ya Sabato pamoja na familia yao. (Luka 4:16) Wakiwa huko, ni lazima alisikiliza kwa makini Maandiko yaliposomwa. Baada ya muda, Yesu alijifunza kusoma Maandishi hayo Matakatifu yeye mwenyewe. Matokeo ni kwamba Yesu hakujua tu Maandiko, bali pia aliyapenda na akaruhusu yaongoze matendo yake. Kwa mfano, kumbuka jambo lililotokea kwenye hekalu Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12 tu. Walimu walioifahamu vizuri Sheria ya Musa “walikuwa wakishangazwa na majibu [ya Yesu] na uwezo wake wa kuelewa.”​—Luka 2:46, 47, 52.

3. Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Sisi pia tunaweza kulifahamu na kulipenda Neno la Mungu tunaposoma Maandiko kwa ukawaida. Hata hivyo, tunawezaje kunufaika zaidi kutokana na mambo tunayosoma? Tunaweza kujifunza kutokana na mambo ambayo Yesu aliwaambia wale walioifahamu Sheria, kutia ndani waandishi, Mafarisayo, na Masadukayo. Viongozi hao wa kidini walisoma Maandiko kwa ukawaida, lakini hawakunufaika na mambo waliyosoma. Yesu alionyesha njia tatu ambazo wanaume hao hawakuwa wakinufaika kikamili na Maandiko. Maneno aliyowaambia yatatusaidia kuboresha uwezo wetu wa (1) kuelewa mambo tunayosoma, (2) kutafuta hazina za kiroho, na (3) kuliruhusu Neno la Mungu litufinyange.

ELEWA MAMBO UNAYOSOMA

4. Andiko la Luka 10:25-29 linatufundisha nini kuhusu kusoma Neno la Mungu?

4 Tungependa kuelewa maana ya mambo tunayosoma katika Neno la Mungu. Tusipofanya hivyo, hatutanufaika kikamili kutokana na mambo tunayosoma. Kwa mfano, fikiria mazungumzo kati ya Yesu na “mtu fulani mwenye ujuzi wa Sheria.” (Soma Luka 10:25-29.) Mwanamume huyo alipouliza kuhusu jambo alilohitaji kufanya ili apate uzima wa milele, Yesu alimwelekeza kwenye Neno la Mungu kwa kumuuliza hivi: “Ni mambo gani yameandikwa katika Sheria? Wewe unasomaje?” Mwanamume huyo alitoa jibu sahihi kwa kunukuu maandiko kuhusu kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Law. 19:18; Kum. 6:5) Lakini ona jambo alilosema baada ya hapo: “Kwa kweli jirani yangu ni nani?” Mwanamume huyo alifunua kwamba hakuwa ameelewa maana halisi ya mambo aliyosoma. Matokeo ni kwamba hakujua jinsi ya kutumia maandiko hayo kwa njia sahihi maishani mwake.

Tunaweza kusitawisha ustadi wa kuelewa yale tunayosoma

5. Kusali na kusoma kwa mwendo wa polepole kunawezaje kutusaidia kuelewa kikamili zaidi yale tunayosoma?

5 Tunaweza kuongeza uelewaji wetu wa Neno la Mungu kwa kusitawisha mazoea mazuri ya kusoma. Yafuatayo ni baadhi ya madokezo yanayoweza kukusaidia. Sali kabla ya kuanza kusoma. Tunahitaji msaada wa Yehova ili kuelewa Maandiko, hivyo tunahitaji kumwomba roho yake takatifu ili tukazie fikira mambo tunayosoma. Kisha soma kwa mwendo wa polepole. Hilo litakusaidia uelewe mambo unayosoma. Huenda ukanufaika zaidi unaposoma kwa sauti au kufuatana na usomaji wa Biblia uliorekodiwa. Kwa njia hiyo, utatumia hisi zako nyingi zaidi, na hilo litakusaidia kuelewa, kukumbuka, na kujifunza mengi zaidi kutokana na mambo unayojifunza katika Neno la Mungu. (Yos. 1:8) Unapomaliza kusoma, sali tena ili kumshukuru Yehova kwa zawadi ya Neno lake na umwombe akusaidie kutumia mambo uliyosoma.

Kwa nini kuandika mambo fulani kunaweza kukusaidia uelewe na kukumbuka mambo unayosoma? (Tazama fungu la 6)

6. Kwa nini kujiuliza maswali na kuandika mambo fulani kutakusaidia unaposoma? (Tazama pia picha.)

6 Yafuatayo ni madokezo mawili zaidi yatakayokusaidia uelewe vizuri zaidi Biblia. Jiulize maswali kuhusu mambo unayosoma. Unapochunguza simulizi fulani, jiulize: ‘Wahusika wakuu ni nani? Ni nani anayezungumza? Anazungumza na nani, na kwa nini? Matukio hayo yanatukia wapi na wakati gani?’ Maswali kama hayo yatakusaidia ufikirie kuhusu na kufuatana na mawazo makuu ya simulizi hilo. Pia, andika mambo fulani unaposoma. Unapoandika, unajilazimisha kufikiria zaidi mambo unayosoma, jambo ambalo litakusaidia uelewe vizuri zaidi. Kuandika kutakusaidia pia ukumbuke mambo unayosoma. Huenda ukaandika maswali uliyo nayo, mambo uliyopata katika utafiti wako, muhtasari wa mambo makuu, jinsi unavyoweza kutumia mambo unayosoma, au kuandika hisia zako. Huenda ukatambua kwamba kuandika mambo hayo kunaweza kukusaidia ulione Neno la Mungu kama ujumbe wake kwako binafsi.

7. Tunahitaji sifa gani tunaposoma, na kwa nini? (Mathayo 24:15)

7 Yesu alitaja sifa muhimu ambayo tunahitaji ili kuelewa yale tunayosoma katika Neno la Mungu—sifa ya utambuzi. (Soma Mathayo 24:15.) Utambuzi ni nini? Ni uwezo wa kuelewa jinsi wazo moja linavyohusiana na wazo lingine na jinsi linavyotofautiana na wazo lingine na kuelewa jambo ambalo halijatajwa waziwazi. Isitoshe, kama Yesu alivyosema, tunahitaji utambuzi ili kutambua matukio yanayotimiza unabii wa Biblia. Pia, tunahitaji sifa hiyo ili tunufaike kikamili na kila jambo tunalosoma katika Biblia.

8. Tunawezaje kusoma kwa utambuzi?

8 Yehova huwapatia watumishi wake utambuzi. Basi sali kwake, na umwombe akusaidie usitawishe sifa hiyo. (Met. 2:6) Unawezaje kutenda kupatana na sala yako? Chunguza kwa makini mambo unayosoma, na utambue jinsi yanavyohusiana na mambo mengine unayojua. Ili kupata msaada, chunguza vifaa vyetu vya kujifunzia Biblia, kama vile Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Vifaa hivyo vitakusaidia utambue maana ya masimulizi ya Biblia na kuona njia ambazo unaweza kutumia habari hiyo katika maisha yako. (Ebr. 5:14) Unaposoma kwa utambuzi, utaelewa Maandiko vizuri zaidi.

TAFUTA HAZINA ZA KIROHO UNAPOSOMA

9. Masadukayo walipuuza kweli gani muhimu ya Kimaandiko?

9 Masadukayo walivifahamu vizuri sana vitabu vitano vya kwanza vya Maandiko ya Kiebrania, lakini walipuuza kweli muhimu zilizo katika vitabu hivyo vilivyoongozwa na roho. Kwa mfano, fikiria jinsi Yesu alivyowajibu Masadukayo walipomuuliza kuhusu ufufuo. Aliwauliza hivi: “Je, hamkusoma katika kitabu cha Musa, simulizi kuhusu kile kichaka cha miiba kwamba Mungu alimwambia: ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’?” (Marko 12:18, 26) Ingawa kwa kweli Masadukayo walikuwa wamesoma mistari hiyo mara nyingi, swali la Yesu lilifunua kwamba walikuwa wamepuuza kweli fulani muhimu ya Kimaandiko, yaani, fundisho kuhusu ufufuo.​—Marko 12:27; Luka 20:38. d

10. Tunapaswa kuwa makini kuhusu mambo gani tunaposoma?

10 Tunajifunza somo gani? Tunaposoma, tunapaswa kuwa makini ili kutambua mambo yote tunayoweza kujifunza kwenye mstari au simulizi fulani la Biblia. Tungependa kutambua mafundisho ya msingi na pia kweli na kanuni nzito zaidi zilizofichika.

11. Kulingana na andiko la 2 Timotheo 3:16, 17, unawezaje kutafuta hazina zilizo katika Biblia?

11 Unawezaje kutafuta hazina za kiroho unaposoma Biblia? Fikiria jambo ambalo andiko la 2 Timotheo 3:16, 17 linasema. (Soma.) Ona kwamba “kila Andiko ni . . . lenye faida” kwa (1) kufundisha, (2) kukaripia (3) kunyoosha mambo, na (4) kutia nidhamu. Unaweza kunufaika kwa njia hizo nne, hata kutoka katika vitabu vya Biblia ambavyo huvitumii kwa ukawaida. Chunguza simulizi fulani ili uone jambo ambalo simulizi hilo linakufundisha kumhusu Yehova, kusudi lake, au kuhusu kanuni za Mungu. Fikiria jinsi linavyoweza kutumiwa kukaripia. Unaweza kufanya hivyo kwa kutambua jinsi mistari hiyo inavyoweza kukusaidia kutambua na kukataa mielekeo na mitazamo isiyofaa na kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. Chunguza jinsi simulizi hilo linavyoweza kutumiwa kunyoosha, au kurekebisha maoni yasiyofaa, labda ni maoni ambayo umesikia katika huduma. Na utafute nidhamu yoyote iliyo katika mistari hiyo ambayo inaweza kukuzoeza ili uige njia ya Yehova ya kufikiri. Ukitumia njia hizo nne zenye manufaa, utapata hazina za kiroho zinazoweza kukusaidia unufaike zaidi na usomaji wako wa Biblia.

RUHUSU USOMAJI WAKO UKUFINYANGE

12. Kwa nini Yesu aliwauliza Mafarisayo “Je, hamjasoma?”

12 Pia, Yesu aliuliza swali “Je, hamjasoma?” ili kufunua kwamba Mafarisayo walikuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu Maandiko. (Mt. 12:1-7) e Pindi hiyo, Mafarisayo walidai kwamba wanafunzi wa Yesu walikuwa wamevunja sheria ya Sabato. Yesu aliwajibu kwa kutaja mifano miwili ya Kimaandiko, na akanukuu mstari fulani kutoka kwenye kitabu cha Hosea ili kuonyesha kwamba Mafarisayo hawakuwa wameelewa kusudi la sheria ya Sabato na walikosa kuonyesha rehema. Kwa nini wanaume hao hawakufinyangwa na usomaji wao wa Neno la Mungu? Kwa sababu walilisoma wakiwa na mtazamo wa kuchambua-chambua na kiburi. Mtazamo wao uliwazuia kuelewa maana ya mambo waliyosoma.​—Mt. 23:23; Yoh. 5:39, 40.

13. Tunapaswa kusoma Biblia tukiwa na mtazamo gani, na kwa nini?

13 Maneno ya Yesu yanatufundisha kwamba tunapaswa kuwa na mtazamo unaofaa tunaposoma Biblia. Kinyume na Mafarisayo, tunapaswa kuwa wanyenyekevu na tayari kufundishwa. Ni lazima “[tupokee] kwa upole kupandwa kwa lile neno.” (Yak. 1:21) Ikiwa sisi ni wapole, tutaruhusu Neno la Mungu litie mizizi katika mioyo yetu. Ikiwa tutaepuka mtazamo wa kuchambua-chambua au kiburi, hapo ndipo masomo ya Biblia kuhusu kuonyesha rehema, huruma, na upendo yatafinyanga maisha yetu.

Tunawezaje kujua ikiwa tunaliruhusu Neno la Mungu litufinyange? (Tazama fungu la 14) f

14. Tunawezaje kujua ikiwa tunaliruhusu Neno la Mungu litufinyange? (Tazama pia picha.)

14 Njia tunayowatendea wengine inaweza kuonyesha ikiwa tunaruhusu Neno la Mungu litufinyange. Mafarisayo hawakuruhusu Neno la Mungu lichochee mioyo yao na matokeo ni kwamba ‘waliwalaumu watu wasio na hatia.’ (Mt. 12:7) Vivyo hivyo, tunaonyesha kwamba tunaruhusu Neno la Mungu litufinyange kupitia jinsi tunavyowaona na kuwatendea wengine. Kwa mfano, je, tuna mwelekeo wa kutaja mambo mazuri tunayoona kuhusu wengine, au je, sisi ni wepesi wa kutaja makosa yao? Je, sisi ni wenye rehema na tuko tayari kusamehe, au je, tuna mwelekeo wa kuchambua-chambua wengine na kuweka kinyongo? Kujiuliza maswali kama hayo kunaweza kufunua ikiwa tunaruhusu mambo tunayosoma yafinyange mawazo, hisia, na matendo yetu.​—1 Tim. 4:12, 15; Ebr. 4:12.

KUSOMA NENO LA MUNGU HULETA FURAHA

15. Yesu alihisije kuhusu Maandiko Matakatifu?

15 Yesu aliyapenda Maandiko Matakatifu, na hisia zake zilitabiriwa kwenye Zaburi 40:8 inayosema: “Ee Mungu wangu, ninafurahia kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu kabisa.” Matokeo ni kwamba alikuwa mwenye furaha na alifanikiwa katika utumishi wake kwa Yehova. Sisi pia tunaweza kupata furaha na kufanikiwa ikiwa tutajitahidi kulisoma na kulipenda Neno la Mungu.​—Zab. 1:1-3.

16. Utafanya nini ili unufaike zaidi kutokana na mambo unayosoma katika Neno la Mungu? (Tazama sanduku “ Maneno ya Yesu Yanaweza Kukusaidia Uelewe Yale Unayosoma.”)

16 Kupatana na maneno na mfano wa Yesu, acheni tuboreshe ustadi wetu wa kusoma Biblia. Tunaweza kuelewa vizuri zaidi masimulizi ya Biblia kwa kusali, kusoma kwa mwendo wa polepole, kujiuliza maswali, na kuandika mambo fulani. Tunaweza kutumia utambuzi tunapochunguza kwa makini mambo tunayosoma kwa kutumia machapisho yetu yanayotegemea Biblia. Tunaweza kujifunza kutumia Maandiko kwa njia nzuri zaidi, hata mistari ambayo hatuifahamu vizuri, kwa kutafuta hazina za kiroho zilizo katika masimulizi hayo. Na tunaweza kuliruhusu Neno la Mungu litufinyange kwa kudumisha mtazamo unaofaa tunaposoma. Tukijitahidi kabisa kufanya mambo hayo, tutanufaika vizuri zaidi tunaposoma Biblia na kumkaribia Yehova hata zaidi.​—Zab. 119:17, 18; Yak. 4:8.

WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

a Sisi sote tunaomwabudu Yehova tunajitahidi kusoma Neno lake kila siku. Wengine wengi husoma Biblia pia; ingawa hivyo, kwa kweli hawaelewi yale wanayosoma. Hivyo ndivyo ilivyokuwa pia kwa baadhi ya watu katika siku za Yesu. Tunapochunguza mambo ambayo Yesu aliwaambia wale waliosoma Neno la Mungu, tutapata masomo ambayo yanaweza kutusaidia tunufaike zaidi tunaposoma Biblia.

b Wakati wa ubatizo wake na alipotiwa mafuta kwa roho takatifu, inaonekana kwamba Yesu alirudishiwa kumbukumbu ya uhai wake kabla ya kuwa mwanadamu.​—Mt. 3:16.

c Maria alifahamu Maandiko vizuri na aliyarejelea. (Luka 1:46-55) Inawezekana kwamba Yosefu na Maria hawakuwa na pesa za kutosha kununua nakala za Maandiko. Ni lazima walisikiliza kwa makini Neno la Mungu liliposomwa kwenye sinagogi ili wakumbuke baadaye.

d Tazama makala “Mkaribie Mungu—‘Yeye Ni Mungu . . . wa Walio Hai’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2013.

e Pia, tazama Mathayo 19:4-6, ambapo Yesu aliwauliza Mafarisayo swali hilohilo, “Je, hamkusoma?” Ingawa walikuwa wamesoma simulizi kuhusu uumbaji, hawakukazia fikira jambo ambalo simulizi hilo lilifundisha kuhusu maoni ya Mungu kuelekea ndoa.

f MAELEZO YA PICHA: Wakati wa mkutano katika Jumba la Ufalme, ndugu anayesaidia katika mfumo wa sauti na video anafanya makosa kadhaa. Ingawa hivyo, baada ya mkutano akina ndugu wanampongeza kwa sababu ya jitihada zake, badala ya kukazia fikira makosa yake.