MAKALA YA 8

“Tunzeni Akili Zenu, Iweni Waangalifu!”

“Tunzeni Akili Zenu, Iweni Waangalifu!”

“Tunzeni akili zenu, iweni waangalifu!”​—1 PET. 5:8.

WIMBO 144 Kaza Macho Kwenye Zawadi!

MUHTASARI a

1. Yesu aliwaambia nini wanafunzi wake kuhusu wakati ambapo mwisho ungetukia, naye aliwapa onyo gani?

 SIKU chache kabla ya kifo cha Yesu, wanne kati ya wanafunzi wake walimuuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara . . . ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3) Inaelekea kwamba wanafunzi hao walikuwa wanajiuliza jinsi ambavyo wangeweza kutambua wakati ambapo mfumo wa mambo wa Kiyahudi ungefikia mwisho wake. Katika jibu lake, Yesu hakuzungumzia tu mwisho wa mfumo wa Kiyahudi, bali pia kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo” ambao sasa tunaishi. Kuhusu wakati ambapo mwisho ungetukia, Yesu alisema: “Kuhusu siku hiyo au saa hiyo hakuna mtu anayejua, wala malaika mbinguni wala Mwana, ila Baba.” Kisha akawaonya wanafunzi wake ‘waendelee kukaa macho’ na ‘waendelee kukesha.’​—Marko 13:32-37.

2. Kwa nini ilikuwa muhimu kwa wale walioishi chini ya mfumo wa mambo wa Kiyahudi waendelee kuwa macho?

2 Wakristo Wayahudi katika karne ya kwanza walipaswa kuendelea kukaa macho ili kuokoa uhai wao. Yesu aliwaambia wafuasi wake mambo ambayo yangewasaidia kutambua wakati ambapo mfumo wa Kiyahudi ungefikia mwisho wake. Alisema hivi: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, jueni kwamba linakaribia kuharibiwa.” Wakati huo walipaswa kutii onyo la Yesu na “waanze kukimbilia milimani.” (Luka 21:20, 21) Wale waliotii onyo hilo waliokoka Waroma walipoliharibu jiji la Yerusalemu.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Leo, tunaishi katika wakati wa mwisho wa mfumo huu wa mambo. Basi, sisi pia tunapaswa kutunza akili zetu na kuendelea kukaa macho. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuonyesha usawaziko tunapoendelea kutazama kwa makini matukio ya ulimwengu, jinsi tunavyoweza kujiangalia wenyewe, na jinsi tunavyoweza kutumia vizuri kabisa muda uliobaki.

UWE MWENYE USAWAZIKO UNAPOTAZAMA MATUKIO YA ULIMWENGU

4. Kwa nini unapaswa kupendezwa unapoona jinsi matukio ya sasa ya ulimwengu yanavyotimiza unabii wa Biblia?

4 Tuna sababu nzuri ya kupendezwa tunapoona jinsi matukio ya sasa ya ulimwengu yanavyotimiza unabii wa Biblia. Kwa mfano, Yesu alitaja kihususa matukio mbalimbali ambayo yangetusaidia kujua kwamba mwisho wa mfumo wa mambo wa Shetani unakaribia. (Mt. 24:3-14) Mtume Petro alitutia moyo kukazia uangalifu kutimizwa kwa unabii ili imani yetu iendelee kuwa na nguvu. (2 Pet. 1:19-21) Kitabu cha mwisho cha Biblia kinaanza na maneno haya: “Ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa ili kuwaonyesha watumwa wake mambo yanayopaswa kutukia hivi karibuni.” (Ufu. 1:1) Basi, tunapendezwa sana na matukio ya sasa ya ulimwengu na kujua jinsi ambavyo huenda yanatimiza unabii wa Biblia. Na huenda tukatamani kuzungumzia matukio hayo na watu wengine.

Tunapozungumzia unabii wa Biblia tunapaswa kuepuka kufanya nini, na tunapaswa kufanya nini? (Tazama fungu la 5) b

5. Tunapaswa kuepuka nini, lakini tunapaswa kufanya nini? (Tazama pia picha.)

5 Hata hivyo, tunapozungumzia unabii wa Biblia, tunapaswa kuepuka kukisiakisia mambo. Kwa nini? Kwa sababu hatungependa kusema jambo lolote linaloweza kuvuruga umoja katika kutaniko. Kwa mfano, huenda tukawasikia viongozi wa ulimwengu wakizungumzia jinsi wanavyoweza kutatua mzozano fulani na kuleta amani na usalama. Badala ya kukisia kwamba maneno kama hayo yanatimiza unabii wa 1 Wathesalonike 5:3, tunahitaji kujua uelewaji wa karibuni zaidi uliochapishwa. Ikiwa mazungumzo yetu yatategemea habari zilizochapishwa na tengenezo la Yehova, tutalisaidia kutaniko liendelee kuwa na umoja katika “njia ileile ya kufikiri.”​—1 Kor. 1:10; 4:6.

6. Tunaweza kujifunza masomo gani kutoka katika 2 Petro 3:11-13?

6 Soma 2 Petro 3:11-13. Mtume Petro anatusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko tunapochunguza unabii wa Biblia. Anatuhimiza ‘tuweke karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ Kwa nini? Si kwa sababu tunataka kujua ‘siku na saa’ ambayo Yehova ataleta Har–Magedoni, bali kwa sababu tunataka kutumia wakati uliobaki kufanya “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (Mt. 24:36; Luka 12:40) Kwa maneno mengine, tungependa kudumisha mwenendo unaofaa na kuhakikisha kwamba jitihada zetu katika utumishi wa Yehova zinafunua jinsi tunavyompenda sana. Ili kuendelea kukazia fikira jambo hilo, tunapaswa kujiangalia wenyewe.

INAMAANISHA NINI KUJIANGALIA WENYEWE?

7. Tunaonyeshaje kwamba tunajiangalia wenyewe? (Luka 21:34)

7 Yesu aliwaambia wanafunzi wake wakazie uangalifu matukio ya ulimwengu na pia wajiangalie wenyewe. Jambo hilo linaonekana wazi kwenye onyo lililo katika Luka 21:34. (Soma.) Ona maneno hayo ya Yesu: “Jiangalieni wenyewe.” Mtu anayejiangalia mwenyewe yuko makini kutambua hatari zozote zinazohatarisha uhusiano wake na Yehova, na anachukua hatua ili kuziepuka. Kwa kufanya hivyo, anaendelea kujitunza katika upendo wa Mungu.​—Met. 22:3; Yuda 20, 21.

8. Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wafanye nini?

8 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wajiangalie wenyewe. Kwa mfano, aliwaambia hivi Wakristo huko Efeso: “Endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima.” (Efe. 5:15, 16) Hali yetu ya kiroho inaendelea kushambuliwa, basi Biblia inatushauri ‘tuendelee kuyafahamu mapenzi ya Yehova’ ili tujilinde dhidi ya mashambulizi ya aina yoyote.​—Efe. 5:17.

9. Tunawezaje kuyafahamu mapenzi ya Yehova kwa ajili yetu?

9 Biblia haitaji kila hatari ambayo inaweza kuhatarisha urafiki wetu pamoja na Yehova. Mara nyingi tunalazimika kufanya maamuzi kuhusu mambo ambayo hayajazungumziwa moja kwa moja katika Maandiko. Ili tufanye maamuzi yenye hekima, tunahitaji kufahamu au kutambua “mapenzi ya Yehova.” Tunaweza kufanya hivyo kwa kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu na kulitafakari. Kadiri tunavyozidi kuelewa mapenzi ya Yehova na kusitawisha “akili ya Kristo,” ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwetu kutembea kama “watu wenye hekima,” hata wakati ambapo hatuna sheria hususa ya kuongoza mwenendo wetu. (1 Kor. 2:14-16) Ni rahisi kutambua baadhi ya hatari; lakini kuna hatari ambazo hazionekani waziwazi.

10. Ni baadhi ya hatari gani tunazopaswa kuepuka?

10 Baadhi ya hatari ambazo tunapaswa kuepuka ni kuwachezea wengine kimapenzi, kunywa pombe kupita kiasi, kula kupita kiasi, kusema mambo yanayowaumiza wengine, na pia kutazama burudani zenye ukatili, ponografia, na mambo kama hayo. (Zab. 101:3) Sikuzote adui yetu Ibilisi anatafuta nafasi ya kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. (1 Pet. 5:8) Tusipokuwa waangalifu Shetani anaweza kupanda ndani ya akili na mioyo yetu mbegu za husuda, kukosa unyoofu, pupa, chuki, kiburi, na kinyongo. (Gal. 5:19-21) Mwanzoni, huenda hisia hizo zisiwe na nguvu sana. Lakini ikiwa hatutachukua hatua mara moja ili kuzing’oa, zitaendelea kukua kama mmea wenye sumu na kusababisha matatizo.​—Yak. 1:14, 15.

11. Ni hatari gani moja iliyojificha tunayopaswa kuepuka, na kwa nini?

11 Hatari moja iliyojificha ni kushirikiana na watu wabaya. Fikiria hali ifuatayo. Unafanya kazi pamoja na mtu ambaye si Shahidi wa Yehova. Ungependa mfanyakazi mwenzako awe na maoni yanayofaa kuhusu Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo unamtendea kwa fadhili na unamsaidia. Hata huenda ukakubali kula chakula cha mchana pamoja na mtu huyo pindi fulani. Baada ya muda, unaanza kufanya hivyo kwa ukawaida. Wakati mwingine, anaanza kuzungumzia mambo yenye ukosefu wa maadili, na mwanzoni unajaribu kuepuka mazungumzo hayo. Baada ya muda kupita, unazoea mazungumzo hayo hivi kwamba hayakukasirishi. Kisha siku moja, mfanyakazi mwenzako anakukaribisha mpate kinywaji baada ya kazi, nawe unakubali. Mwishowe, unaanza kufikiri kama mfanyakazi mwenzako. Kufikia wakati huo, haitachukua muda kabla uanze kufanya mambo ambayo mfanyakazi mwenzako anafanya. Bila shaka, tunawatendea watu wote kwa fadhili na heshima, lakini tunapaswa kukumbuka kwamba tutaathiriwa kwa njia kubwa na wale tunaoshirikiana nao. (1 Kor. 15:33) Tukijiangalia wenyewe, kama Yesu alivyotuhimiza, tutaepuka kushirikiana isivyo lazima na wale ambao hawaishi kulingana na viwango vya Yehova. (2 Kor. 6:15) Tutaona hatari na kuiepuka.

TUMIA VIZURI KABISA WAKATI WAKO

12. Wanafunzi wa Yesu walipaswa kufanya nini walipokuwa wakisubiri mwisho wa mfumo wa mambo?

12 Wanafunzi wa Yesu walipaswa kuwa na shughuli nyingi walipokuwa wakisubiri mwisho wa mfumo wa mambo. Yesu aliwapatia kazi ya kufanya. Aliwaamuru wahubiri habari njema “katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:6-8) Wafuasi wa Yesu walipewa kazi kubwa sana! Walitumia muda wao vizuri kabisa kwa kufanya yote waliyoweza ili kutimiza mgawo huo.

13. Kwa nini tunapaswa kutumia wakati wetu vizuri kabisa? (Wakolosai 4:5)

13 Soma Wakolosai 4:5. Ili tujiangalie wenyewe, tunapaswa kufikiria jinsi tunavyotumia wakati wetu. “Matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kumpata yeyote kati yetu. (Mhu. 9:11) Tunaweza kufa ghafla.

Tunawezaje kutumia vizuri kabisa wakati wetu? (Tazama fungu la 14 na 15)

14-15. Tunawezaje kutumia vizuri kabisa wakati wetu? (Waebrania 6:11, 12) (Tazama pia picha.)

14 Tunaweza kutumia wakati wetu vizuri kabisa kwa kufanya mapenzi ya Yehova na kuimarisha urafiki wetu pamoja naye. (Yoh. 14:21) Tunapaswa kuwa “imara, thabiti, sikuzote [tukiwa] na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Kisha mwisho utakapofika—iwe ni mwisho wa uhai wetu au mwisho wa mfumo huu wa mambo—hatutajuta.​—Mt. 24:13; Rom. 14:8.

15 Leo, Yesu anaendelea kuongoza wanafunzi wake wanapohubiri kuhusu Ufalme wa Mungu katika dunia yote. Tayari ametimiza ahadi yake. Kupitia tengenezo la Yehova, Yesu anatuzoeza jinsi ya kuhubiri na anatuandalia vifaa tunavyohitaji ili kutangaza habari njema. (Mt. 28:18-20) Tunatimiza sehemu yetu kwa kuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri na kufundisha na kwa kuendelea kuwa macho tunaposubiri Yehova alete mwisho wa mfumo huu wa mambo. Tukifuata ushauri ulio katika Waebrania 6:11, 12, tutashikilia tumaini letu “mpaka mwisho.”​—Soma.

16. Tumeazimia kufanya nini?

16 Yehova ameweka siku na saa ambayo ataondoa mfumo wa Shetani. Siku hiyo itakapofika, kwa hakika Yehova atatimiza unabii ambao aliongoza uandikwe katika Neno lake. Lakini wakati mwingine, huenda ikaonekana kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo umechelewa. Hata hivyo, siku ya Yehova ‘haitachelewa!’ (Hab. 2:3) Basi, acheni tuazimie “kumtazamia Yehova” na kuonyesha “mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu [wetu].”​—Mika 7:7.

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

a Katika makala hii, tutachunguza jinsi tunavyoweza kudumisha usawaziko wa kiroho na kuendelea kukaa macho. Pia, tutaona jinsi tunavyoweza kujiangalia wenyewe, na jinsi tunavyoweza kutumia vizuri kabisa muda tulio nao.

b MAELEZO YA PICHA: (Juu) Wenzi wa ndoa wanatazama taarifa ya habari. Baadaye, baada ya mkutano wa kutaniko, wanawaeleza wengine maoni yao kuhusu maana ya matukio kwenye taarifa ya habari. (Chini) Wenzi wa ndoa wakitazama ripoti ya Baraza Linaloongoza ili kupata habari za uelewaji wetu wa karibuni zaidi kuhusu unabii wa Biblia. Wanawapa wengine machapisho yanayotegemea Biblia ambayo yanaandaliwa na mtumwa mwaminifu.