MAKALA YA 11

Unawezaje Kujitayarisha kwa Ajili ya Ubatizo?

Unawezaje Kujitayarisha kwa Ajili ya Ubatizo?

“Ni nini kinachonizuia kubatizwa?”​—MDO. 8:36.

WIMBO 50 Sala Yangu ya Wakfu

MUHTASARI a

Ulimwenguni pote, vijana kwa wazee wanafanya maendeleo na kubatizwa (Tazama fungu la 1 na 2)

1-2. Ikiwa huko tayari kubatizwa, kwa nini hupaswi kuvunjika moyo? (Tazama picha kwenye jalada.)

 IKIWA unatamani kubatizwa, umejiwekea lengo zuri sana. Je, uko tayari kuchukua hatua hiyo sasa? Ikiwa unaamini uko tayari na wazee wanakubali, usisite kubatizwa kwenye kusanyiko linalofuata. Maisha yenye kuridhisha kwenye utumishi wa Yehova yanakungojea.

2 Kwa upande mwingine, je, umeambiwa unahitaji kufanya maendeleo zaidi ili ubatizwe? Au je, umetambua jambo hilo mwenyewe? Ikiwa ndivyo, usivunjike moyo. Unaweza kufanya maendeleo ili ufikie hatua hiyo muhimu, iwe wewe ni kijana au mzee.

“NI NINI KINACHONIZUIA?”

3. Ofisa Mwethiopia wa makao ya kifalme alimuuliza nini Filipo, na hilo linatokeza swali gani? (Matendo 8:36, 38)

3 Soma Matendo 8:36, 38. Ofisa Mwethiopia wa makao ya kifalme alimuuliza Filipo mweneza injili hivi: “Ni nini kinachonizua kubatizwa?” Mwanamume huyo Mwethiopia alitamani kubatizwa, lakini je, kweli alikuwa tayari kuchukua hatua hiyo muhimu?

Ofisa Mwethiopia aliazimia kuendelea kujifunza kumhusu Yehova (Tazama fungu la 4)

4. Mwanamume Mwethiopia alionyeshaje kwamba alikuwa ameazimia kuendelea kujifunza?

4 Mwanamume huyo Mwethiopia “alikuwa ameenda Yerusalemu kuabudu.” (Mdo. 8:27) Hivyo, ni lazima alikuwa amebadili dini na kuwa mfuasi wa dini ya Kiyahudi. Bila shaka, alikuwa amejifunza kumhusu Yehova katika maandishi matakatifu ya Maandiko ya Kiebrania. Hata hivyo, alitamani kujifunza mengi zaidi. Isitoshe, Filipo alipokutana na ofisa huyo barabarani, mwanamume huyo alikuwa akifanya nini? Alikuwa akisoma hatikunjo ya maandishi ya nabii Isaya. (Mdo. 8:28) Hicho ni chakula kigumu cha kiroho. Ofisa huyo wa makao ya kifalme hakuridhika tu kujifunza mambo machache ya msingi; alitaka kuendelea kujifunza.

5. Mwanamume Mwethiopia alifanya nini baada ya kujifunza?

5 Mwanamume huyo alikuwa ofisa mwenye cheo cha juu akiwa chini ya Malkia Kandake wa Ethiopia; “alisimamia hazina yote ya malkia.” (Mdo. 8:27) Hivyo, ni lazima alikuwa mwanamume mwenye shughuli na majukumu mengi. Lakini alitenga wakati wa kumwabudu Yehova. Hakuridhika tu kujifunza kweli; alitenda kulingana na yale aliyojifunza. Hivyo, alisafiri mbali kutoka Ethiopia ili kumwabudu Yehova hekaluni jijini Yerusalemu. Lazima safari hiyo ilichukua muda mrefu na ilihusisha gharama kubwa, lakini mwanamume huyo alitaka kumwabudu Yehova haidhuru ni jitihada gani iliyohusika.

6-7. Upendo wa mwanamume Mwethiopia kwa Yehova uliendeleaje kuimarika?

6 Mwanamume Mwethiopia alijifunza kutoka kwa Filipo baadhi ya kweli mpya muhimu, kutia ndani utambulisho wa Masihi. (Mdo. 8:34, 35) Bila shaka, ofisa huyo wa makao ya kifalme alifurahi kujifunza mambo ambayo Yesu alikuwa amemfanyia. Alifanya nini baada ya kujifunza mambo hayo? Angeweza kuendelea kuwa mfuasi wa dini ya Kiyahudi aliyeheshimiwa. Badala yake, upendo wake kwa Yehova na Mwana Wake uliongezeka. Naye alichochewa kufanya uamuzi muhimu wa kubatizwa akiwa mfuasi wa Yesu Kristo. Alipoona kwamba mwanamume huyo alikuwa tayari, Filipo alimbatiza.

7 Ikiwa utafuata mfano wa mwanamume huyo Mwethiopia, unaweza kujitayarisha ili ustahili kubatizwa. Wewe pia, utaweza kusema kwa uhakika, “Ni nini kinachonizuia kubatizwa?” Acheni tuchunguze jinsi unavyoweza kuchukua hatua zilezile alizochukua: Aliendelea kujifunza, alitenda kulingana na yale aliyojifunza, na aliendelea kuimarisha upendo wake kwa Mungu.

ENDELEA KUJIFUNZA

8. Andiko la Yohana 17:3 na maelezo ya chini, linasema unapaswa kufanya nini?

8 Soma Yohana 17:3 na maelezo ya chini. Je, maneno hayo ya Yesu yalikusaidia kufanya uamuzi wa kujifunza Biblia? Hilo ni kweli kwa wengi wetu. Lakini je, maneno hayo yanatuambia pia tuendelee kujifunza? Ndiyo. Hatutaacha kamwe ‘kuendelea kupata ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli.’ (Mhu. 3:11) Tutaendelea kujifunza kwa umilele wote. Kadiri tunavyojifunza zaidi, ndivyo tutakavyomkaribia zaidi Yehova.​—Zab. 73:28.

9. Tunahitaji kufanya nini baada ya kujifunza kweli za msingi?

9 Inaeleweka kwamba tunapojifunza kumhusu Yehova tunaanza na mambo ya msingi. Katika barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo aliyarejelea mafundisho hayo kuwa “mambo ya msingi.” Hakuwa akisema kuwa “fundisho la msingi” halikuwa muhimu; alikuwa akililinganisha na maziwa yenye lishe ambayo mtoto anapatiwa. (Ebr. 5:12; 6:1) Lakini pia, aliwahimiza Wakristo wote waendelee kujifunza mengi zaidi ya mafundisho ya msingi na kujifunza kweli nzito za Neno la Mungu. Je, umesitawisha tamaa ya kujifunza mafundisho mazito ya Biblia? Je, uko tayari kuendelea kukua, kuendelea kujifunza zaidi kumhusu Yehova na mapenzi yake?

10. Kwa nini si rahisi kwa baadhi ya watu kusoma na kujifunza?

10 Hata hivyo, si rahisi kwa wengi wetu kujifunza. Namna gani wewe? Je, ulipokuwa shuleni ulifundishwa kusoma na kujifunza kwa njia nzuri? Je, ulinufaika na kufurahia kusoma na kujifunza? Au je, ulifikia mkataa kwamba huna uwezo mzuri wa kujifunza? Ikiwa ndivyo, huko peke yako. Yehova anaweza kukusaidia. Yeye ni mkamilifu na ndiye Mwalimu bora kabisa.

11. Yehova amethibitikaje kuwa “Mfundishaji wako Mkuu”?

11 Yehova anajiita “Mfundishaji wako Mkuu.” (Isa. 30:20, 21) Yeye ni Mwalimu mwenye subira, fadhili, na anatuelewa. Anakazia fikira sifa nzuri za wanafunzi wake. (Zab. 130:3) Na kamwe hatarajii mengi zaidi ya yale tunayoweza kutimiza. Kumbuka kwamba alibuni ubongo wako, zawadi yenye kustaajabisha. (Zab. 139:14) Tuna tamaa ya asili ya kujifunza. Muumba wetu anataka tuendelee kujifunza na kufurahia kufanya hivyo. Hivyo, ni jambo la hekima ‘kukuza hamu’ kwa ajili ya kweli za Biblia sasa. (1 Pet. 2:2) Jiwekee malengo ambayo unaweza kufikia, na shikamana na ratiba yako ya kusoma na kujifunza Biblia. (Yos. 1:8) Kwa msaada wa Yehova, utafurahia kusoma na kujifunza kumhusu zaidi na zaidi.

12. Kwa nini tunapaswa kumkazia fikira Yesu katika funzo letu la kibinafsi?

12 Tenga wakati kwa ukawaida ili kutafakari kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu, ndilo jambo muhimu ambalo litatusaidia kumtumikia Yehova, hasa katika nyakati hizi ngumu. (1 Pet. 2:21) Yesu alisema waziwazi kuhusu changamoto ambazo wafuasi wake wangekabili. (Luka 14:27, 28) Hata hivyo, alikuwa na uhakika kwamba wafuasi wake wa kweli wangefanikiwa kama yeye alivyofanikiwa. (Yoh. 16:33) Jifunze mambo hususa kuhusu maisha ya Yesu na jiwekee malengo ili umwige katika maisha yako ya kila siku.

13. Unapaswa kuendelea kumwomba Yehova nini, na kwa nini?

13 Ujuzi pekee hautoshi. Sababu ya kuhitaji ujuzi ni ili ukusaidie kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova na kusitawisha sifa kama vile kumpenda na kuwa na imani kwake. (1 Kor. 8:1-3) Unapojifunza, endelea kumwomba Yehova akusaidie uwe na imani zaidi. (Luka 17:5) Anajibu sala hizo kwa ukarimu. Imani ya kweli inayotegemea ujuzi sahihi kumhusu Mungu wetu itakusaidia kufanya maendeleo zaidi.​—Yak. 2:26.

ENDELEA KUTUMIA MAMBO UNAYOJIFUNZA

Kabla ya Gharika, Noa na familia yake walitumia kwa uaminifu mambo waliyojifunza (Tazama fungu la 14)

14. Mtume Petro alikaziaje umuhimu wa kutumia yale tunayojifunza? (Tazama pia picha.)

14 Mtume Petro alikazia jinsi ilivyo muhimu kwa wafuasi wa Kristo kuendelea kutumia yale wanayojifunza. Alirejelea simulizi la Biblia kumhusu Noa. Yehova alimwambia Noa kwamba kupitia gharika angewaharibu watu waovu wa siku zake. Kujua tu kwamba kungekuwa na gharika hakungetosha kumwokoa Noa na familia yake. Ona kwamba Petro alirejelea kipindi kabla ya Gharika kuwa wakati “safina ilipokuwa ikijengwa.” (1 Pet. 3:20) Naam, Noa na familia yake walitumia yale waliyojifunza kutoka kwa Mungu kwa kujenga safina, meli kubwa. (Ebr. 11:17) Kisha Petro akalinganisha jambo alilofanya Noa na ubatizo kwa kuandika hivi: “Ubatizo, ambao unalingana na hili, unawaokoa ninyi sasa pia.” (1 Pet. 3:21) Hivyo, tunaweza kulinganisha kazi unayofanya sasa ya kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo na kazi ya kujenga safina ambayo Noa na familia yake walifanya kwa miaka mingi. Ni kazi gani unayohitaji kufanya ili uwe tayari kwa ajili ya ubatizo?

15. Kutubu kikweli kunahusisha nini?

15 Jambo la kwanza tunalohitaji kufanya ni kutubu kwa unyoofu dhambi zetu. (Mdo. 2:37, 38) Ikiwa tutatubu kikweli tutafanya mabadiliko ya kweli. Je, umeacha kufanya mambo yanayomchukiza Yehova, kama vile kuishi maisha mapotovu kiadili, kutumia tumbaku, au kutumia lugha chafu? (1 Kor. 6:9, 10; 2 Kor. 7:1; Efe. 4:29) Ikiwa bado hujafanya hivyo, endelea kujitahidi kufanya mabadiliko. Zungumza na mtu unayejifunza naye Biblia, au waombe wazee wa kutaniko wakupatie msaada na mwongozo. Ikiwa wewe ni kijana na unaishi nyumbani, endelea kuwaomba wazazi wako msaada ili uache mazoea yoyote mabaya ambayo huenda yanakuzuia kubatizwa.

16. Ratiba nzuri ya kiroho inahusisha nini?

16 Pia, ni muhimu kuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Hilo linatia ndani kuhudhuria na kushiriki kwenye mikutano ya Kikristo. (Ebr. 10:24, 25) Na unapostahili kushiriki katika huduma ya Kikristo, hakikisha unafanya hivyo kwa ukawaida. Kadiri unavyoshiriki kwenye kazi hiyo ya kuokoa uhai, ndivyo utakavyoifurahia zaidi. (2 Tim. 4:5) Ikiwa wewe ni kijana na unaishi nyumbani, jiulize hivi: ‘Je, wazazi wangu wanahitaji kunikumbusha kuhudhuria mikutano au kushiriki katika huduma? Au je, ninafanya hivyo bila kukumbushwa?’ Kwa kuchukua hatua hizo mwenyewe, unaonyesha imani yako na unaonyesha kwamba unampenda na kumshukuru Yehova Mungu. Hivyo ni “vitendo vya ujitoaji-kimungu,” zawadi unazomtolea Yehova. (2 Pet. 3:11; Ebr. 13:15) Zawadi zote ambazo tunazitoa kwa hiari na bila kulazimishwa zinampendeza Mungu wetu. (Linganisha 2 Wakorintho 9:7.) Tunafanya mambo hayo kwa sababu tunafurahia kumtolea Yehova kilicho bora.

ENDELEA KUIMARISHA UPENDO WAKO KWA YEHOVA

17-18. Ni sifa gani muhimu itakayokusaidia kufikia hatua ya ubatizo, na kwa nini? (Methali 3:3-6)

17 Unapoendelea kujitahidi kufikia ubatizo, utakabili changamoto. Huenda baadhi ya watu wakakudhihaki kwa sababu ya imani yako mpya; huenda hata wakakupinga au kukutesa. (2 Tim. 3:12) Unapojitahidi kushinda zoea baya, huenda pindi fulani ukarudia tabia hiyo. Au huenda ukakosa subira na kukata tamaa kwa sababu unahisi uko mbali na lengo lako. Ni nini kitakachokusaidia kuvumilia? Sifa muhimu—upendo wako kwa Yehova.

18 Upendo wako kwa Yehova ni sifa maridadi sana, sifa bora zaidi uliyo nayo. (Soma Methali 3:3-6.) Upendo wenye nguvu kwa Mungu unaweza kukusaidia kukabiliana na changamoto maishani kwa mafanikio. Biblia inarejelea mara kwa mara upendo mshikamanifu wa Yehova kwa watumishi wake. Huo ni upendo unaoshikamana kabisa na mtu, hivyo hatatuacha kamwe. (Zab. 100:5) Umeumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwa. 1:26) Unawezaje kuonyesha upendo wa aina hiyo?

Unaweza kumshukuru Yehova kila siku (Tazama fungu la 19) b

19. Unawezaje kuonyesha shukrani zaidi kwa mambo yote ambayo Yehova amekufanyia? (Wagalatia 2:20)

19 Anza kwa kuonyesha shukrani. (1 The. 5:18) Kila siku, jiulize, ‘Yehova amenionyeshaje upendo?’ Kisha hakikisha kwamba unamshukuru Yehova katika sala zako, ukitaja mambo hususa ambayo amekufanyia. Yaone matendo yake ya upendo kuwa yanaelekezwa kwako wewe kibinafsi, kama tu mtume Paulo alivyotambua jambo hilo kumhusu Yehova. (Soma Wagalatia 2:20.) Jiulize, ‘Je, ninataka kumwonyesha upendo pia?’ Upendo wako kwa Yehova utakusaidia kupinga vishawishi na kukabiliana na changamoto kwa mafanikio. Utakusaidia kushikamana na ratiba yako ya kiroho, na kuendelea kumwonyesha Baba yako upendo siku baada ya siku.

20. Wakfu wako kwa Yehova unahusisha nini, na uamuzi huo ni muhimu kadiri gani?

20 Baada ya muda, upendo wako kwa Yehova utakuchochea umtolee sala ya pekee. Utajiweka wakfu kwa Mungu. Kumbuka kwamba utakapojiweka wakfu kwa Yehova utakuwa na tumaini hili zuri: Utakuwa mali yake kwa umilele wote. Nadhiri ya kujiweka wakfu kwa Yehova haiathiriwi na panda-shuka za maisha. Haihitaji kutolewa upya. Ni kweli kwamba tunapojiweka wakfu, tunachukua hatua muhimu. Hata hivyo, fikiria jambo hili: Utafanya maamuzi mengi katika maisha yako, na baadhi ya maamuzi hayo yatakuwa mazuri sana, lakini hutawahi kufanya uamuzi bora zaidi kuliko kujiweka wakfu kwa Yehova. (Zab. 50:14) Shetani atajaribu kudhoofisha upendo wako kwa Baba yako, akitarajia kwamba utavunja utimilifu wako. Kamwe usimruhusu Shetani ashinde! (Ayu. 27:5) Upendo wako wenye nguvu kwa Yehova utakusaidia uishi kulingana na wakfu wako na kumkaribia zaidi Baba yako wa mbinguni.

21. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ubatizo si mwisho wa safari, bali ni mwanzo tu?

21 Baada ya kujiweka wakfu kwa Yehova, zungumza na wazee wa kutaniko lako kuhusu kuchukua hatua muhimu inayofuata. Hata hivyo, sikuzote kumbuka kwamba ubatizo si mwisho, bali ni mwanzo tu. Ni mwanzo wa safari isiyo na mwisho ya kumtumikia Yehova. Hivyo, imarisha upendo wako kumwelekea Baba yako sasa. Jiwekee malengo ili upendo wako uendelee kuimarika siku baada ya siku. Kufanya hivyo kutakuongoza kwenye hatua ya ubatizo. Hiyo itakuwa siku nzuri sana. Lakini huu ni mwanzo tu. Upendo wako kwa Yehova na Mwana wake uendelee kuongezeka milele!

WIMBO 135 Mwaliko Wenye Upendo wa Yehova: “Uwe na Hekima, Mwanangu”

a Ili tufanye maendeleo yatakayotusaidia kustahili kubatizwa, tunahitaji kuchochewa na nia nzuri. Pia, tunahitaji kuchukua hatua sahihi. Kwa kutumia mfano wa ofisa Mwethiopia wa makao ya kifalme, tutachunguza hatua ambazo mwanafunzi wa Biblia anahitaji kuchukua ili astahili kubatizwa.

b MAELEZO YA PICHA: Dada kijana anamwambia Yehova katika sala jinsi anavyoshukuru kwa yale aliyomwandalia.