MAKALA YA 19

Hakuna Kitu Chochote Kinachoweza Kuwakwaza Waadilifu

Hakuna Kitu Chochote Kinachoweza Kuwakwaza Waadilifu

“Wale wanaoipenda sheria yako wana amani nyingi; hakuna chochote kinachoweza kuwakwaza.”—ZAB. 119:165.

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

MUHTASARI a

1-2. Mwandishi fulani alisema nini, na tutachunguza nini katika makala hii?

 LEO, mamilioni ya watu wanadai kwamba wanamwamini Yesu, lakini hawakubali mambo aliyofundisha. (2 Tim. 4:3, 4) Isitoshe, mwandishi fulani alisema hivi: “Ikiwa kungekuwa na ‘Yesu’ mwingine miongoni mwetu leo, ambaye angesema mambo kama ambayo Yesu mwenyewe alisema . . . , je, tungemkataa kama Yesu alivyokataliwa miaka 2,000 iliyopita? . . . Matendo na mtazamo wa watu wengi unaonyesha kwamba jibu lao ni: Ndiyo, tungemkataa.”

2 Katika karne ya kwanza, watu wengi walimsikia Yesu akifundisha na kumwona akifanya miujiza, lakini walikataa kumwamini. Kwa nini? Katika makala iliyotangulia, tulichunguza sababu nne kwa nini watu walikwazika na mambo ambayo Yesu alisema na kutenda. Acheni tuchunguze sababu nne zaidi. Tunapofanya hivyo, tutaona kwa nini watu leo wanawakataa wafuasi wa Yesu na jinsi tunavyoweza kuepuka kukwazika.

(1) YESU HAKUWA NA UBAGUZI

Watu wengi walikwazika kwa sababu ya watu ambao Yesu alichagua kushirikiana nao. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 3) b

3. Yesu alichagua kufanya mambo gani yaliyosababisha baadhi ya watu wakwazike?

3 Yesu alipokuwa duniani, alichagua kushirikiana na watu wa aina zote. Alikula pamoja na matajiri na wenye mamlaka, lakini pia alitumia muda wake mwingi pamoja na maskini na watu waliokandamizwa. Pia, aliwahurumia watu ambao walionwa kuwa “watenda dhambi.” Watu waliojiona kuwa waadilifu walikwazika kwa sababu ya mambo ambayo Yesu alifanya. Waliwauliza hivi wanafunzi wake: “Kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi?” Ili kuwajibu, Yesu alisema: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji. Sikuja kuwaita waadilifu, bali kuwahimiza watenda dhambi watubu.”—Luka 5:29-32.

4. Kulingana na nabii Isaya, Wayahudi walipaswa kutarajia nini kumhusu Masihi?

4 Maandiko yanasema nini? Muda mrefu kabla ya Masihi kuja, nabii Isaya alimfafanua kuwa mtu ambaye hangekubaliwa na ulimwengu. Unabii huo ulitabiri hivi: “Alidharauliwa na kuepukwa na wanadamu . . . Ilikuwa kana kwamba uso wake ulifichwa kutoka kwetu. Alidharauliwa, nasi tulimwona kuwa asiye na maana.” (Isa. 53:3) Masihi angeepukwa “na wanadamu,” kwa hiyo Wayahudi hao wa karne ya kwanza walipaswa kutarajia kwamba Yesu angekataliwa.

5. Watu wengi leo wana maoni gani kuhusu wafuasi wa Yesu?

5 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Makasisi wengi wanafurahia kuwakubali katika dini zao watu ambao ni mashuhuri, matajiri, na wanaoonwa na ulimwengu kuwa wenye hekima. Makasisi hao wanafanya hivyo hata ingawa maadili na njia ya maisha ya washiriki hao wapya mara nyingi haipatani na viwango vya Mungu. Makasisi haohao wanawadharau watumishi wa Yehova wenye bidii na maadili safi kwa sababu wao si mashuhuri kulingana na viwango vya ulimwengu huu. Ni kama tu mtume Paulo alivyosema, Mungu aliwachagua wale ‘wanaodharauliwa.’ (1 Kor. 1:26-29) Hata hivyo, machoni pa Yehova, watumishi wake wote waaminifu ni wenye thamani.

6. Kama Mathayo 11:25, 26 inavyoonyesha, tunaweza kuigaje mtazamo wa Yesu?

6 Tunaweza kuepukaje kukwazika? (Soma Mathayo 11:25, 26.) Usikubali kuathiriwa na maoni ya ulimwengu kuhusu watu wa Mungu. Tambua kwamba Yehova huwatumia tu watu wanyenyekevu ili wafanye mapenzi yake. (Zab. 138:6) Tafakari kuhusu jinsi ambavyo ametimiza mambo mengi kwa kuwatumia watu ambao ulimwengu unawaona kuwa hawana hekima au si wasomi.

(2) YESU ALIFUNUA MAFUNDISHO YA UWONGO

7. Kwa nini Yesu aliwaita Mafarisayo wanafiki, nao waliitikiaje?

7 Kwa ujasiri Yesu alishutumu matendo ya kinafiki ya viongozi wa kidini wa siku zake. Kwa mfano, alifunua unafiki wa Mafarisayo ambao walihangaikia sana jinsi walivyoosha mikono yao kuliko walivyowatunza wazazi wao. (Mt. 15:1-11) Huenda wanafunzi wa Yesu walishangazwa na maneno yake. Isitoshe, walimuuliza hivi: “Unajua kwamba Mafarisayo walikwazika waliposikia mambo uliyosema?” Yesu aliwajibu hivi: “Kila mmea ambao Baba yangu wa mbinguni hakuupanda utang’olewa. Waacheni. Wao ni viongozi vipofu. Basi, kipofu akimwongoza kipofu, wote wawili watatumbukia ndani ya shimo.” (Mt. 15:12-14) Yesu hakuruhusu hasira ya viongozi hao wa kidini imzuie kusema ukweli.

8. Yesu alionyeshaje kwamba si imani zote za kidini zinazokubalika machoni pa Mungu?

8 Pia, Yesu alifunua mafundisho ya kidini ya uwongo. Hakusema kwamba imani zote za kidini zinakubalika machoni pa Mungu. Badala yake, alizungumza kuhusu watu wengi ambao wangekuwa kwenye barabara yenye nafasi kubwa inayoongoza kwenye uharibifu, lakini alisema ni wachache tu wangekuwa kwenye barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima. (Mt. 7:13, 14) Alisema wazi kwamba baadhi ya watu wangedai wanamtumikia Mungu, lakini kihalisi hawakuwa wanamtumikia. Alionya hivi: “Jihadharini na manabii wa uwongo ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwamwitu wakali. Kwa matunda yao mtawatambua.”—Mt. 7:15-20.

Watu wengi walikwazika kwa sababu ya jinsi Yesu alivyoshutumu imani na mazoea ya uwongo. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 9) c

9. Yesu alifunua mafundisho gani ya kidini ya uwongo?

9 Maandiko yanasema nini? Kuhusu Masihi, Biblia ilitabiri kwamba bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova ingemla. (Zab. 69:9; Yoh. 2:14-17) Bidii hiyo ilimchochea Yesu kufunua imani na mazoea ya uwongo ya kidini. Kwa mfano, Mafarisayo walifundisha kwamba nafsi haiwezi kufa; Yesu alifundisha kwamba wafu wamelala usingizi. (Yoh. 11:11) Masadukayo walipinga ufufuo; Yesu alimfufua Lazaro, rafiki yake. (Yoh. 11:43, 44; Mdo. 23:8) Mafarisayo walifundisha kwamba kila kitu kinachotokea ni majaliwa, au kinasababishwa na Mungu; Yesu alifundisha kwamba wanadamu wanaweza kuchagua kumtumikia Mungu au la.—Mt. 11:28.

10. Kwa nini watu wengi hukwazwa na mafundisho yetu?

10 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Watu wengi wanakwazika kwa sababu mafundisho yetu yanayotegemea Biblia yanafunua mafundisho ya uwongo ya kidini. Makasisi wanafundisha wafuasi wao kwamba Mungu huwaadhibu waovu kwenye moto wa mateso. Wanatumia mafundisho hayo ya uwongo kuwadhibiti watu. Tukiwa watumishi wa Yehova wanaomwabudu Mungu mwenye upendo, tunafunua fundisho hilo la uwongo. Pia, makasisi wanafundisha kwamba nafsi haiwezi kufa. Sisi tunafunua chanzo cha kipagani cha fundisho hilo, ambalo ikiwa lingekuwa la kweli, ufufuo usingehitajika. Kinyume na fundisho la kwamba Mungu hupanga mambo yote kimbele—ambalo dini nyingi zinafundisha—sisi tunafundisha kwamba wanadamu wana uhuru wa kuchagua na wanaweza kuchagua kumtumikia Mungu. Viongozi wa kidini wanatendaje tunapofunua mafundisho yao ya uwongo? Mara nyingi, wanakasirika sana!

11. Kulingana na maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Yohana 8:45-47, Mungu anataka watu wake wafanye nini?

11 Tunaweza kuepukaje kukwazika? Ikiwa tunaipenda kweli, ni lazima tuyakubali maneno ya Mungu. (Soma Yohana 8:45-47.) Tofauti na Shetani Ibilisi, sisi tunasimama imara katika kweli. Sikuzote tunashikamana na mambo tunayoamini. (Yoh. 8:44) Mungu anataka watu wake ‘wachukie maovu’ na ‘kushikamana na mema,’ kama tu Yesu alivyofanya.—Rom. 12:9; Ebr. 1:9.

(3) YESU ALITESWA

Watu wengi walikwazika kwa sababu ya jinsi Yesu alivyokufa kwenye mti wa mateso. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 12) d

12. Kwa nini njia ambayo Yesu aliuawa iliwakwaza Wayahudi wengi?

12 Ni jambo gani lingine ambalo liliwakwaza Wayahudi katika siku za Yesu? Paulo alisema hivi: “Tunamhubiri Kristo aliyeuawa kwenye mti, kwa Wayahudi ni sababu ya kujikwaa.” (1 Kor. 1:23) Kwa nini Wayahudi wengi walihangaishwa na njia ambayo Yesu alikufa? Kulingana na maoni yao, Yesu kufa kwenye mti wa mateso kulifanya aonekane kuwa mhalifu na mtenda dhambi, na si Masihi.—Kum. 21:22, 23.

13. Wale waliokwazika kwa sababu ya Yesu walishindwa kutambua nini?

13 Wayahudi ambao walikwazika kwa sababu ya Yesu walishindwa kutambua kwamba hakuwa na hatia, kwamba alishtakiwa kwa uwongo, na kwamba alitendewa isivyo haki. Wale ambao walikuwa wanaendesha kesi yake hawakutenda kwa haki. Washiriki wa mahakama kuu ya Kiyahudi walikusanyika haraka, na waliendesha kesi hiyo bila kufuata utaratibu uliowekwa. (Luka 22:54; Yoh. 18:24) Badala ya kusikiliza bila ubaguzi mashtaka na ushahidi dhidi ya Yesu, watu hao waliomhukumu walitafuta “ushahidi wa uwongo dhidi ya Yesu ili wamuue.” Mbinu yao iliposhindikana, kuhani mkuu alijaribu kumtega Yesu ili aseme jambo ambalo wangeweza kutumia kumshtaki. Hilo lilikuwa kinyume kabisa na sheria zilizowekwa. (Mt. 26:59; Marko 14:55-64) Baada ya Yesu kufufuliwa kutoka kwa wafu, mahakimu hao wasio waadilifu waliwalipa askari wa Roma ambao walikuwa wanalinda kaburi lake, “kiasi kikubwa cha fedha” ili wasambaze hadithi ya uwongo iliyoeleza kwa nini kaburi lilikuwa tupu.—Mt. 28:11-15.

14. Maandiko yalitabiri nini kuhusu kifo cha Masihi?

14 Maandiko yanasema nini? Ingawa Wayahudi wengi katika siku za Yesu hawakutarajia kwamba Masihi angehitaji kufa, Maandiko yalitabiri hivi: “Aliumwaga uhai wake mpaka kifo naye alihesabiwa miongoni mwa wakosaji; aliibeba dhambi ya watu wengi, naye aliwatetea wakosaji.” (Isa. 53:12) Hivyo, Wayahudi hawakuwa na sababu ya kukwazika Yesu alipouawa kama mtenda dhambi.

15. Ni mashtaka gani dhidi ya Mashahidi wa Yehova ambayo yamewafanya baadhi ya watu wakwazike?

15 Je, tunaona tatizo hilo leo? Bila shaka! Yesu alishtakiwa na kuhukumiwa isivyo haki, na Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitendewa kwa njia hiyohiyo isiyo ya haki. Tuchunguze mifano kadhaa. Nchini Marekani katika miaka ya 1930 na 1940, uhuru wetu wa kumwabudu Mungu ulipingwa mahakamani tena na tena. Baadhi ya mahakimu, walitubagua bila aibu. Katika jimbo la Quebec, Kanada, Kanisa Katoliki lilishirikiana bega kwa bega na serikali ili kupinga kazi yetu. Wahubiri wengi walifungwa gerezani kwa sababu tu waliwaeleza majirani zao kuhusu Ufalme wa Mungu. Nchini Ujerumani, wakati wa serikali ya Wanazi, ndugu wengi vijana waaminifu waliuawa na utawala huo usiomwogopa Mungu. Katika miaka ya karibuni, ndugu zetu wengi nchini Urusi wamehukumiwa na kufungwa gerezani kwa sababu ya kuzungumza na wengine kuhusu Biblia, jambo ambalo wenye mamlaka wanadai kwamba ni utendaji wenye “msimamo mkali.” Hata Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Kirusi imepigwa marufuku na kutangazwa kuwa ni chapisho lenye “msimamo mkali” kwa sababu linatumia jina Yehova.

16. Kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Yohana 4:1, kwa nini hatupaswi kupotoshwa na hadithi za uwongo kuhusu watu wa Yehova?

16 Tunaweza kuepukaje kukwazika? Tafuta habari kamili. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwaonya wasikilizaji wake kwamba baadhi ya watu ‘wangewasingizia kila aina ya uovu.’ (Mt. 5:11) Chanzo cha uwongo huo ni Shetani. Yeye huwachochea wapinzani waeneze uchongezi mbaya sana kuhusu wale wanaoipenda kweli. (Ufu. 12:9, 10) Ni lazima tukatae uwongo unaosemwa na wapinzani wetu. Hatupaswi kamwe kuruhusu uwongo kama huo ututetemeshe au kudhoofisha imani yetu.—Soma 1 Yohana 4:1.

(4) YESU ALISALITIWA NA KUACHWA

Watu wengi walikwazika kwa sababu ya jinsi Yesu alivyosalitiwa na Yuda. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 17 na 18) e

17. Ni kwa njia gani matukio yaliyotangulia kifo cha Yesu yangeweza kuwakwaza baadhi ya watu?

17 Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisalitiwa na mmoja wa mitume wake 12. Mtume mwingine alimkana Yesu mara tatu, na mitume wake wote walimwacha usiku uliotangulia kifo chake. (Mt. 26:14-16, 47, 56, 75) Yesu hakushangazwa na jambo hilo. Hata alikuwa ametabiri kwamba mambo hayo yangetokea. (Yoh. 6:64; 13:21, 26, 38; 16:32) Walipoona mambo hayo, huenda baadhi ya watu wangeweza kukwazika, wakitoa sababu kwamba ‘Ikiwa hivyo ndivyo mitume wa Yesu wanavyojiendesha, mimi sitaki kuwa mmoja wao!’

18. Ni unabii gani mbalimbali uliotimizwa kupitia mambo yaliyotukia muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu?

18 Maandiko yanasema nini? Karne nyingi mapema, Yehova alifunua katika Neno lake kwamba Masihi angesalitiwa kwa vipande thelathini vya fedha. (Zek. 11:12, 13) Msaliti angekuwa mtu wa karibu wa Yesu. (Zab. 41:9) Nabii Zekaria pia aliandika hivi: “Mpige mchungaji, acha kondoo watawanyike.” (Zek. 13:7) Badala ya kukwazwa na matukio hayo, watu wenye mioyo minyoofu walipaswa kuimarishwa kwa kuona unabii huo mbalimbali ukitimizwa kupitia Yesu.

19. Watu wenye mioyo minyoofu wanatambua nini?

19 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Katika nyakati zetu, Mashahidi wachache wanaojulikana sana wameiacha kweli, wakawa waasi-imani, na kisha wanajaribu kuwapotosha wengine. Wameeneza ripoti mbaya, kweli nusu-nusu, na uwongo wa moja kwa moja kuhusu Mashahidi wa Yehova kupitia vyombo vya habari na Intaneti. Lakini watu wenye mioyo minyoofu hawakwaziki. Badala yake, wanatambua kwamba Biblia ilitabiri kwamba mambo kama hayo yangetokea.—Mt. 24:24; 2 Pet. 2:18-22.

20. Tunaweza kuepukaje kukwazwa na wale walioiacha kweli? (2 Timotheo 4:4, 5)

20 Tunaweza kuepukaje kukwazika? Tunahitaji kuimarisha imani yetu kwa kujifunza kwa ukawaida, kwa kusali bila kuacha, na kuwa na bidii katika kazi ambayo Yehova ametupatia tuifanye. (Soma 2 Timotheo 4:4, 5.) Ikiwa tuna imani, hatutaogopa tunaposikia ripoti mbaya kuhusu Mashahidi wa Yehova. (Isa. 28:16) Upendo wetu kwa Yehova, Neno lake, na ndugu zetu utatusaidia kuepuka kukwazwa na wale walioiacha kweli.

21. Hata ingawa watu wengi wanaukataa ujumbe wetu, tunaweza kuwa na uhakika gani?

21 Katika karne ya kwanza, wengi walikwazika, na walimkataa Yesu. Hata hivyo, wengine wengi walimkubali Yesu. Watu hao walitia ndani angalau mshiriki mmoja wa Sanhedrini ya Wayahudi na hata “umati mkubwa wa makuhani.” (Mdo. 6:7; Mt. 27:57-60; Marko 15:43) Vivyo hivyo leo, mamilioni ya watu hawajakwazika. Kwa nini? Kwa sababu wanajua na wanazipenda kweli zinazopatikana katika Maandiko. Neno la Mungu linasema hivi: “Wale wanaoipenda sheria yako wana amani nyingi; hakuna chochote kinachoweza kuwakwaza.”—Zab. 119:165.

WIMBO 124 Washikamanifu Sikuzote

a Katika makala iliyotangulia, tulizungumzia sababu nne zilizofanya watu wamkatae Yesu wakati uliopita, na kwa nini wanawakataa wafuasi wake leo. Katika makala hii, tutachunguza sababu nne zaidi. Pia, tutaona kwa nini watu wenye mioyo minyoofu wanaompenda Yehova hawaruhusu kitu chochote kiwakwaze.

b MAELEZO YA PICHA: Yesu akishiriki mlo pamoja na Mathayo na wakusanya kodi.

c MAELEZO YA PICHA: Yesu akiwafukuza hekaluni wafanyabiashara.

d MAELEZO YA PICHA: Yesu analazimishwa kubeba mti wa mateso.

e MAELEZO YA PICHA: Yuda anamsaliti Yesu kwa kumbusu.