MAKALA YA 18

Je, Utakwazika kwa Sababu ya Yesu?

Je, Utakwazika kwa Sababu ya Yesu?

“Mwenye furaha ni mtu ambaye hapati ndani yangu sababu ya kukwaza.”—MT. 11:6.

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

MUHTASARI a

1. Huenda ulishangazwa na nini ulipojaribu kwa mara ya kwanza kuwaambia wengine kuhusu ujumbe wa Biblia?

 JE, UNAKUMBUKA mara ya kwanza ulipotambua umeipata kweli? Mafundisho ya Biblia uliyojifunza yalikuwa rahisi kueleweka! Ulihisi kwamba kila mtu angekubali mambo ambayo ulianza kuamini. Ulisadiki kwamba ujumbe wa Biblia ungewapatia maisha yenye kusudi sasa na tumaini zuri sana la wakati ujao. (Zab. 119:105) Hivyo, kwa shauku uliwaambia marafiki na ndugu zako kuhusu kweli ulizopata. Lakini matokeo yalikuwaje? Ulishangaa kuona kwamba wengi walikataa mambo uliyowaambia.

2-3. Watu wengi katika siku za Yesu walikuwa na maoni gani kumhusu na kuhusu ujumbe wake?

2 Hatupaswi kushangaa wengine wanapokataa ujumbe tunaohubiri. Katika siku za Yesu, watu wengi walimkataa hata ingawa alifanya miujiza kuthibitisha kwamba alikuwa ametumwa na Mungu. Kwa mfano, Yesu alimfufua Lazaro—muujiza ambao wale waliompinga hawakuweza kuukataa. Hata hivyo, viongozi wa Wayahudi hawakukubali kwamba Yesu alikuwa Masihi. Hata walitaka kumuua Yesu na Lazaro!—Yoh. 11:47, 48, 53; 12:9-11.

3 Yesu alijua kwamba watu wengi wangekataa kukubali kwamba yeye ndiye Masihi. (Yoh. 5:39-44) Aliwaambia hivi wanafunzi wa Yohana Mbatizaji: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hapati ndani yangu sababu ya kukwaza.” (Mt. 11:2, 3, 6) Kwa nini watu wengi walimkataa Yesu?

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Katika makala hii na ile inayofuata, tutachunguza sababu kadhaa kwa nini watu wengi katika karne ya kwanza hawakumwamini Yesu. Pia, tutaona kwa nini watu wengi leo wanakwazwa na ujumbe wetu. Jambo la muhimu zaidi, tutajifunza jinsi tunavyoweza kuepuka kukwazika ili tuendelee kumfuata Yesu.

(1) MALEZI YA YESU

Watu wengi walikwazika kwa sababu ya malezi ya Yesu. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 5) b

5. Kwa nini huenda baadhi ya watu walifikiri kwamba Yesu hakuwa Masihi aliyetabiriwa?

5 Watu wengi walikwazika kwa sababu ya malezi ya Yesu. Walikubali kwamba Yesu alikuwa mwalimu mzuri na kwamba alifanya miujiza. Lakini machoni pao, alikuwa tu mwana wa seremala maskini. Na alitoka Nazareti, mji ambao ulionekana si muhimu. Hata Nathanaeli ambaye alikuja kuwa mwanafunzi wa Yesu, mwanzoni alisema hivi: “Je, kitu chochote kizuri kinaweza kutoka Nazareti?” (Yoh. 1:46) Huenda Nathanaeli hakuupenda mji ambao Yesu aliishi wakati huo. Au huenda alikuwa akikumbuka unabii unaopatikana katika Mika 5:2, ambao ulitabiri kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu, na si Nazareti.

6. Ni jambo gani ambalo lingewasaidia watu katika siku za Yesu kutambua kwamba Yesu alikuwa Masihi?

6 Maandiko yanasema nini? Nabii Isaya alitabiri kwamba maadui wa Yesu wangeshindwa kujishughulisha “na habari za kizazi [cha Masihi].” (Isa. 53:8) Habari nyingi kumhusu Masihi zilikuwa zimetabiriwa. Ikiwa watu hao wangekuwa wametenga wakati ili kupata habari kamili, wangetambua kwamba Yesu alizaliwa Bethlehemu na kwamba alikuwa uzao wa Mfalme Daudi. (Luka 2:4-7) Hivyo, Yesu alizaliwa mahali ambapo palitabiriwa katika Mika 5:2. Basi tatizo lilikuwa nini? Watu walifanya uamuzi haraka. Hawakuwa na habari kamili. Kwa sababu hiyo, walikwazika.

7. Kwa nini watu wengi leo wanawakataa watu wa Yehova?

7 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Kwa ujumla watu wengi wa Yehova si matajiri; wanaonwa na wengi kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Baadhi ya watu wanahisi kwamba watu wa Mungu hawawezi kufundisha kuhusu Biblia kwa sababu hawajahitimu kwenye shule za theolojia. Wengine wanasema kwamba Mashahidi wa Yehova ni “dini ya Marekani,” hata ingawa ukweli ni kwamba kwa kukadiria ni Shahidi 1 tu kati ya 7 anayeishi nchini Marekani. Bado wengine wameambiwa kwamba Mashahidi hawamwamini Yesu. Kwa miaka mingi, watu wa Yehova wameitwa “Wakomunisti,” “majasusi wa Kimarekani,” na “watu wenye msimamo mkali.” Kwa kuwa wale wanaoambiwa hadithi hizo hawana habari kamili au hawakubali ukweli wa mambo, wanakwazika.

8. Kulingana na Matendo 17:11, watu wanapaswa kufanya nini ikiwa wanataka kuwatambua watumishi wa Yehova leo?

8 Mtu anaweza kuepukaje kukwazika? Watu wanahitaji kutafuta habari kamili. Hivyo ndivyo Luka, mwandikaji wa Injili, alivyoazimia kufanya. Alijitahidi kufuatilia “mambo yote kwa usahihi tangu mwanzo.” Alitaka wasomaji wake wajue “kikamili uhakika wa mambo” waliyosikia kumhusu Yesu. (Luka 1:1-4) Wayahudi wa Beroya ya kale walikuwa kama Luka. Waliposikia kwa mara ya kwanza habari njema kumhusu Yesu, walichunguza Maandiko ya Kiebrania ili kuhakikisha mambo waliyokuwa wakiambiwa. (Soma Matendo 17:11.) Vivyo hivyo, watu leo wanahitaji kuchunguza ukweli wa mambo. Ni lazima walinganishe mambo wanayofundishwa na watu wa Mungu na yale ambayo Maandiko yanasema. Pia, wanahitaji kujifunza historia ya watu wa Yehova katika nyakati za kisasa. Ikiwa watafanya utafiti wa kutosha, hawataruhusu ubaguzi au maneno wanayosikia yawapofushe.

(2) YESU ALIKATAA KUFANYA MIUJIZA ILI KUJIONYESHA

Watu wengi walikwazika kwa sababu Yesu alikataa kufanya ishara za kujionyesha. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 9 na 10) c

9. Ni nini kilichotokea Yesu alipokataa kuonyesha ishara kutoka mbinguni?

9 Baadhi ya watu katika siku za Yesu hawakuridhika na uwezo wake wa pekee wa kufundisha. Walitaka mengi zaidi. Walisisitiza athibitishe kwamba alikuwa Masihi kwa kuwaonyesha “ishara kutoka mbinguni.” (Mt. 16:1) Huenda walisisitiza jambo hilo kwa sababu hawakuelewa maana ya andiko la Danieli 7:13, 14. Hata hivyo, haukuwa wakati wa Yehova kutimiza unabii huo. Mambo ambayo Yesu alikuwa anafundisha yalitosha kuwathibitishia kwamba yeye ndiye aliyekuwa Masihi. Lakini alipokataa kuonyesha ishara waliyotaka, walikwazika.—Mt. 16:4.

10. Yesu alitimizaje jambo ambalo Isaya aliandika kuhusu Masihi?

10 Maandiko yanasema nini? Nabii Isaya aliandika hivi kumhusu Masihi: “Hatalia kwa sauti wala kupaza sauti yake, naye hatafanya sauti yake isikike barabarani.” (Isa. 42:1, 2) Yesu alifanya huduma yake bila kujionyesha. Hakujenga mahekalu na hakuvaa mavazi ya kidini yaliyomtofautisha na wengine au kuitwa kwa majina ya cheo ya kidini. Wakati wa kesi yake, Yesu alikataa kumpendeza Mfalme Herode kwa kufanya muujiza kwa ajili yake, ingawa maisha yake yalikuwa hatarini. (Luka 23:8-11) Yesu alifanya miujiza kadhaa, lakini kazi yake kuu ilikuwa kuhubiri habari njema. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nilikuja kwa kusudi hilo.”—Marko 1:38.

11. Baadhi ya watu leo wana mtazamo gani usio sahihi?

11 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Leo, watu wengi wanavutiwa na majengo makubwa ya ibada yaliyo na mapambo ya bei ghali, makasisi wenye majina makubwa ya vyeo, na sherehe ambazo watu wengi wamesahau kwamba maana au vyanzo vyake ni vya kipagani. Watu wanaohudhuria ibada hizo za kidini hawajifunzi mambo mengi kumhusu Mungu na makusudi yake. Wale wanaohudhuria mikutano yetu ya Kikristo wanajifunza mambo ambayo Yehova anataka tufanye na jinsi ya kuishi kulingana na mapenzi yake. Majumba yetu ya Ufalme ni safi na yanatimiza kusudi, ingawa hayajapambwa kwa gharama zinazopita kiasi. Wale wanaoongoza hawavai mavazi yanayowatofautisha na wengine; wala hawaitwi kwa majina ya vyeo. Neno la Mungu ndilo msingi wa mafundisho na imani yetu. Hata hivyo, watu wengi leo wanakwazika kwa sababu hatuna sherehe au desturi zinazosisimua na mambo tunayofundisha hayapatani na mambo wanayotaka kusikia.

12. Kama inavyofafanuliwa kwenye Waebrania 11:1, 6, tunapaswa kujengaje imani yetu?

12 Tunaweza kuepukaje kukwazika? Mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo waliokuwa wakiishi Roma: “Imani hufuata jambo lililosikiwa. Nalo jambo lililosikiwa ni kupitia neno kumhusu Kristo.” (Rom. 10:17) Hivyo, tunaimarisha imani yetu kwa kujifunza Maandiko na si kwa kushiriki katika sherehe za kidini ambazo si za Kimaandiko, hata iwe sherehe hizo zinavutia kadiri gani. Ni lazima tujenge imani yenye nguvu inayotegemea ujuzi sahihi kwa sababu “bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema.” (Soma Waebrania 11:1, 6.) Hivyo, hatuhitaji kuona ishara ya pekee kutoka mbinguni ili kuthibitisha kwamba tumeipata kweli. Kuchunguza kwa makini mafundisho ya Biblia yanayoimarisha imani, kunatosha kutusadikisha kwamba tumepata kweli na kuondoa shaka yoyote.

(3) YESU HAKUFUATA DESTURI NYINGI ZA KIYAHUDI

Watu wengi walikwazika kwa sababu Yesu alikataa baadhi ya desturi zao. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 13) d

13. Ni jambo gani lililofanya watu wengi wamkatae Yesu?

13 Katika siku za Yesu, wanafunzi wa Yohana Mbatizaji walishangaa kwa sababu wanafunzi wa Yesu hawakuwa wakifunga. Yesu alifafanua kwamba hawakuwa na sababu ya kufunga alipokuwa angali hai. (Mt. 9:14-17) Hata hivyo, Mafarisayo na wengine waliompinga Yesu walimshutumu kwa sababu hakufuata desturi zao. Walikasirika walipoona akiponya wagonjwa siku ya Sabato. (Marko 3:1-6; Yoh. 9:16) Kwa upande mmoja, walidai kwamba walishika Sabato; lakini kwa upande mwingine, walikuwa wakifanya biashara hekaluni. Viongozi hao walikasirika sana Yesu alipowashutumu kwa sababu hiyo. (Mt. 21:12, 13, 15) Na wale ambao Yesu aliwahubiria katika sinagogi huko Nazareti, walikasirika sana Yesu alipotumia mfano wa historia ya Waisraeli kuwaonyesha kwamba walikuwa na ubinafsi na hawakuwa na imani. (Luka 4:16, 25-30) Watu wengi walimkataa Yesu kwa sababu hakutenda kwa njia ambayo walitarajia.—Mt. 11:16-19.

14. Kwa nini Yesu alishutumu desturi za wanadamu ambazo hazikupatana na Maandiko?

14 Maandiko yanasema nini? Yehova alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Watu hawa hunikaribia kwa vinywa vyao nao huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali sana nami; na hofu yao kunielekea inategemea amri za wanadamu ambazo wamefundishwa.” (Isa. 29:13) Yesu alikuwa sahihi kushutumu desturi za wanadamu ambazo hazikupatana na Maandiko. Wale walioona sheria na desturi za wanadamu kuwa muhimu kuliko Maandiko walimkataa Yehova na yule aliyemtuma akiwa Masihi.

15. Leo watu wengi hawapendi mambo gani kuwahusu Mashahidi wa Yehova?

15 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Watu wengi hukasirika Mashahidi wa Yehova wanapokataa kujiunga nao ili kusherehekea desturi zisizo za Kimaandiko, kama vile siku za kuzaliwa na Krismasi. Wengine wanakasirika Mashahidi wa Yehova wanapokataa kujiunga kwenye sherehe za kitaifa au wanapokataa kufuata desturi za mazishi ambazo hazipatani na Neno la Mungu. Wale wanaokwazika kwa sababu hizo huenda kwa unyoofu wakaamini kwamba wanamwabudu Mungu kwa njia inayokubalika. Lakini hawawezi kumpendeza Yehova ikiwa wanapendelea desturi za ulimwengu huu badala ya mafundisho yaliyo wazi yanayopatikana katika Biblia.—Marko 7:7-9.

16. Kulingana na Zaburi 119:97, 113, 163-165, ni lazima tufanye nini na tuepuke nini?

16 Tunaweza kuepukaje kukwazika? Tunahitaji kuzipenda sana sheria na kanuni za Yehova. (Soma Zaburi 119:97, 113, 163-165.) Tunapompenda Yehova tutakataa desturi zozote zinazomchukiza. Hatutaruhusu kitu chochote kiwe muhimu zaidi kuliko upendo wetu kwa Yehova.

(4) YESU HAKUTATUA MATATIZO YA KISIASA KWA WAKATI HUO

Watu wengi walikwazika kwa sababu Yesu alikataa kujihusisha katika masuala ya kisiasa. Jambo hilo linaweza kuwakwazaje watu leo? (Tazama fungu la 17) e

17. Ni matarajio gani yaliyowafanya watu wengi wakwazike na kumkataa Yesu?

17 Baadhi ya watu katika siku za Yesu walitaka mabadiliko ya haraka ya kisiasa. Walitarajia kwamba Masihi angewaweka huru kutokana na utawala wenye kukandamiza wa Waroma. Lakini walipojaribu kumweka Yesu kuwa mfalme wao, alikataa. (Yoh. 6:14, 15) Wengine—kutia ndani makuhani—waliogopa kwamba Yesu angeleta mabadiliko ya kisiasa ambayo yangewakasirisha Waroma ambao walikuwa wamewapa viongozi hao wa kidini nguvu na mamlaka ya kadiri. Masuala hayo ya kisiasa yaliwafanya Wayahudi wengi wamkatae Yesu.

18. Watu wengi walipuuza unabii gani mbalimbali kumhusu Masihi?

18 Maandiko yanasema nini? Ingawa unabii mwingi ulitabiri kwamba mwishowe Masihi angekuja kuwa Shujaa mshindi, unabii mwingine ulionyesha kwamba ilikuwa lazima kwanza afe kwa ajili ya dhambi zetu. (Isa. 53:9, 12) Basi kwa nini walikuwa na matarajio yasiyo sahihi? Watu wengi katika siku za Yesu walipuuza unabii wowote ambao haukuahidi kutatua matatizo yao wakati huo.—Yoh. 6:26, 27.

19. Ni matarajio gani ambayo yamewakwaza wengi leo?

19 Je, tunaona tatizo hilo leo? Ndiyo. Watu wengi leo wanakwazika kwa sababu ya msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote inapohusu mambo ya kisiasa. Wanatarajia tupige kura kwenye uchaguzi. Hata hivyo, tunatambua kwamba kwa mtazamo wa Yehova ikiwa tutamchagua mtawala wa kibinadamu atutawale, tutakuwa tukimkataa Yeye. (1 Sam. 8:4-7) Huenda pia watu wakahisi kwamba tunapaswa kujenga shule, hospitali, na pia kutoa misaada ya kijamii. Wanakwazika kwa sababu tunaelekeza jitihada zetu katika kazi ya kuhubiri, na si kujaribu kutatua matatizo ya ulimwengu.

20. Kama inavyokaziwa na maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 7:21-23, lengo letu kuu linapaswa kuwa nini?

20 Tunaweza kuepukaje kukwazika? (Soma Mathayo 7:21-23.) Lengo letu kuu linapaswa kuwa kufanya kazi ambayo Yesu alituamuru. (Mt. 28:19, 20) Hatupaswi kamwe kukengeushwa na masuala ya kisiasa na ya kijamii ya ulimwengu huu. Tunawapenda watu na kujali matatizo yao, lakini tunajua kwamba njia bora ya kuwasaidia jirani zetu ni kwa kuwafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu na kuwasaidia wasitawishe uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.

21. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

21 Katika makala hii, tumechunguza mambo manne yaliyowafanya watu wengi wakwazike na kumkataa Yesu katika karne ya kwanza na mambo yanayoweza kuwafanya baadhi ya watu wawakatae wafuasi wa Yesu leo. Lakini je, ni mambo hayo tu tunayohitaji kuepuka? Hapana. Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo manne zaidi yanayoweza kutukwaza. Acheni tuazimie kuepuka kukwazika na kuendelea kuimarisha imani yetu!

WIMBO 56 Fanya Kweli Iwe Njia Yako ya Maisha

a Ingawa Yesu alikuwa Mwalimu mkuu zaidi aliyeishi duniani, watu wengi katika siku zake walikwazika kwa sababu yake. Kwa nini? Katika makala hii, tutachunguza sababu nne. Pia, tutaona kwa nini watu wengi leo wanakwazwa na mambo ambayo wafuasi wa kweli wa Yesu wanasema na kutenda. Jambo la muhimu zaidi, tutajifunza jinsi tunavyoweza kuepuka kukwazika ili tuendelee kumfuata Yesu.

b MAELEZO YA PICHA: Filipo anamtia moyo Nathanaeli akutane na Yesu.

c MAELEZO YA PICHA: Yesu akihubiri habari njema.

d MAELEZO YA PICHA: Yesu anamponya mwanamume aliyepooza mkono huku wapinzani wakimtazama.

e MAELEZO YA PICHA: Yesu akielekea mlimani peke yake.