MAKALA YA 39

Je, Jina Lako Liko Katika “Kitabu cha Uzima”?

Je, Jina Lako Liko Katika “Kitabu cha Uzima”?

“Kitabu cha kumbukumbu kikaandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wanaomwogopa Yehova.”​—MAL. 3:16.

WIMBO 61 Songeni Mbele, Enyi Mashahidi!

MUHTASARI a

Katika historia yote ya wanadamu, Yehova amekuwa akiongeza majina kwenye “kitabu cha uzima” (Tazama fungu la 1 na 2)

1. Kulingana na Malaki 3:16, Yehova amekuwa akiandika kitabu gani, na kina habari gani?

 KWA maelfu ya miaka, Yehova amekuwa akiandika kitabu cha pekee. Kitabu hicho kina orodha ya majina, kuanzia jina la shahidi wa kwanza mwaminifu, Abeli. b (Luka 11:50, 51) Tangu wakati wa Abeli, Yehova ameongeza majina katika kitabu hicho, na leo kina mamilioni ya majina. Katika Biblia, kitabu hicho kinaitwa “kitabu cha kumbukumbu,” “kitabu cha uzima,” na “kitabu cha kukunjwa cha uzima.” Katika makala hii, tutakiita “kitabu cha uzima.”​—Soma Malaki 3:16; Ufu. 3:5; 17:8.

2. Ni nani ambao majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima, na tunapaswa kufanya nini ili majina yetu yaandikwe katika kitabu hicho?

2 Kitabu hicho cha pekee kina majina ya wale wote wanaomwabudu Yehova kwa woga, au heshima kubwa, na wanaolipenda jina lake. Wana tumaini la kupata uzima wa milele. Leo, majina yetu yanaweza kuandikwa katika kitabu hicho ikiwa tutasitawisha uhusiano wa karibu na wa kibinafsi pamoja na Yehova kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Mwana wake, Yesu Kristo. (Yoh. 3:16, 36) Sote tungependa majina yetu yaandikwe katika kitabu hicho​—iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani.

3-4. (a) Je, tutaishi milele ikiwa sasa majina yetu yameandikwa katika kitabu cha uzima? Eleza. (b) Ni jambo gani ambalo litazungumziwa katika makala hii na ile inayofuata?

3 Je, inamaanisha kwamba wale wote ambao majina yao yameandikwa katika kitabu hicho watapata uzima wa milele? Tunapata jibu la swali hilo katika maneno ambayo Yehova alimwambia Musa kwenye andiko la Kutoka 32:33. Yehova alisema hivi: “Yeyote aliyenitendea dhambi, nitamfuta katika kitabu changu.” Basi, majina ambayo sasa yako katika kitabu hicho yanaweza kufutwa, au kuondolewa, kana kwamba mwanzoni Yehova anaandika majina hayo kwa penseli. (Ufu. 3:5, maelezo ya chini) Tunapaswa kuhakikisha kwamba majina yetu yanabaki katika kitabu hicho hadi yatakapoandikwa kwa njia ya kudumu, kana kwamba kwa wino.

4 Huenda tukajiuliza maswali fulani. Kwa mfano, Biblia inasema nini kuhusu wale ambao majina yao yameandikwa kwenye kitabu cha uzima na wale ambao majina yao hayajaandikwa katika kitabu hicho? Ni wakati gani ambapo wale ambao majina yao yatabaki katika kitabu hicho watapata uzima wa milele? Namna gani wale ambao walikufa bila kupata fursa ya kumjua Yehova? Je, majina yao yanaweza kuandikwa katika kitabu hicho? Maswali hayo yatajibiwa katika makala hii na ile inayofuata.

NI NANI AMBAO MAJINA YAO YAKO KATIKA KITABU HICHO?

5-6. (a) Kama inavyoonyeshwa kwenye Wafilipi 4:3, ni nani ambao majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima? (b) Ni wakati gani ambapo majina yao yataandikwa kwa njia ya kudumu katika kitabu cha uzima?

5 Ni nani ambao majina yao yameandikwa kwenye kitabu hicho cha mfano? Ili kujibu swali hilo, tutachunguza vikundi vitano vya watu. Kati ya vikundi hivyo, baadhi ya majina ya watu yameandikwa katika kitabu cha uzima, na mengine hayapo.

6 Kikundi cha kwanza kinafanyizwa na wale ambao wamechaguliwa ili watawale pamoja na Yesu mbinguni. Je, sasa majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima? Ndiyo. Kulingana na maneno ya mtume Paulo kwa ‘wafanyakazi wenzake’ huko Filipi, majina ya watiwa-mafuta ambao wamepewa mwaliko wa kutawala pamoja na Yesu, sasa yameandikwa katika kitabu cha uzima. (Soma Wafilipi 4:3.) Lakini ili majina yao yabaki katika kitabu hicho cha mfano, ni lazima waendelee kuwa waaminifu. Kisha baada ya kutiwa muhuri wa mwisho, iwe ni kabla ya kufa au kabla ya dhiki kuu kuanza, majina yao yataandikwa kwa njia ya kudumu katika kitabu hicho.​—Ufu. 7:3.

7. Kulingana na Ufunuo 7:16, 17, ni wakati gani ambapo majina ya umati mkubwa wa kondoo wengine yataandikwa kwa njia ya kudumu katika kitabu cha uzima?

7 Kikundi cha pili kinafanyizwa na umati mkubwa wa kondoo wengine. Je, sasa majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima? Ndiyo. Je, bado majina yao yatakuwa katika kitabu hicho baada ya kuokoka Har–Magedoni? Ndiyo. (Ufu. 7:14) Yesu alisema kwamba watu hao walio kama kondoo “watapata uzima wa milele.” (Mt. 25:46) Lakini watu hao watakaookoka Har–Magedoni hawatapata uzima wa milele papo hapo. Majina yao yataendelea kuwa katika kitabu cha uzima kana kwamba yameandikwa kwa penseli. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, Yesu “atawachunga na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.” Wale watakaotii mwongozo wa Kristo na mwishowe wahukumiwe kuwa waaminifu kwa Yehova, majina yao yataandikwa kwa njia ya kudumu katika kitabu cha uzima.​—Soma Ufunuo 7:16, 17.

8. Ni nani ambao majina yao hayajaandikwa katika kitabu cha uzima, na ni nini kitakachowapata?

8 Kikundi cha tatu kinafanyizwa na mbuzi, ambao wataangamizwa wakati wa Har–Magedoni. Majina yao hayako katika kitabu cha uzima. Yesu anasema kwamba “watakatiliwa mbali milele.” (Mt. 25:46) Paulo aliongozwa na roho kusema kwamba “watu hao watapata hukumu ya adhabu ya uharibifu wa milele.” (2 The. 1:9; 2 Pet. 2:9) Hali iko hivyo pia kwa wale wote ambao wameitendea dhambi kimakusudi roho takatifu katika historia yote ya wanadamu. Watu hawatapata uzima wa milele, badala yake watapata uharibifu wa milele. Ni wazi kwamba hawatafufuliwa. (Mt. 12:32; Marko 3:28, 29; Ebr. 6:4-6) Acheni sasa tuzungumzie vikundi viwili vya watu ambao watafufuliwa duniani.

WALE WATAKAOFUFULIWA

9. Kama inavyoonyeshwa kwenye Matendo 24:15, ni vikundi gani viwili vitakavyofufuliwa duniani, na kuna tofauti gani kati ya vikundi hivyo?

9 Biblia inazungumza kuhusu vikundi viwili vya watu watakaofufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele duniani, yaani, “waadilifu” na “wasio waadilifu.” (Soma Matendo 24:15.) “Waadilifu” ni wale waliomtumikia Yehova kwa uaminifu walipokuwa hai. Kinyume chake, “wasio waadilifu” ni wale ambao hawakumtumikia kwa uaminifu. Kwa kweli, katika visa vingi hawakutenda kwa uadilifu. Kwa kuwa vikundi vyote viwili vitafufuliwa, je, tunaweza kusema kwamba majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima? Ili kujibu swali hilo acheni tuchunguze kila kikundi.

10. Kwa nini “waadilifu” watafufuliwa, na baadhi yao watapata pendeleo gani? (Tazama pia katika toleo hili “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” kuhusu ufufuo utakaofanyika duniani.)

10 “Waadilifu” ndio wanaofanyiza kikundi cha nne. Kabla ya kufa, majina yao yalikuwa yameandikwa kwenye kitabu cha uzima. Je, majina yao yaliondolewa katika kitabu hicho walipokufa? Hapana, kwa sababu bado “wako hai” katika kumbukumbu ya Yehova. Yehova “si Mungu wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake wote wako hai.” (Luka 20:38) Hilo linamaanisha kwamba waadilifu watakapofufuliwa hapa duniani, majina yao yatapatikana yakiwa yameandikwa katika kitabu cha uzima, ingawa mwanzoni yatakuwa yameandikwa “kwa penseli.” (Luka 14:14) Bila shaka, baadhi ya watu hao watakaofufuliwa watapata pendeleo la kutumikia wakiwa “wakuu katika dunia yote.”​—Zab. 45:16.

11. “Wasio waadilifu” watahitaji kujifunza nini kabla ya majina yao kuandikwa katika kitabu cha uzima?

11 Mwishowe, fikiria kikundi cha tano, “wasio waadilifu.” Labda kwa sababu hawakujua sheria za Yehova, hawakuishi maisha ya uadilifu kabla ya kufa. Basi, majina yao hayakuandikwa katika kitabu cha uzima. Lakini Mungu atakapowafufua, watapata nafasi ili mwishowe majina yao yaandikwe katika kitabu cha uzima. Watu hao “wasio waadilifu” watahitaji kusaidiwa sana. Kabla ya kufa, baadhi yao walifanya mambo mabaya sana. Kwa hiyo, watahitaji kufundishwa jinsi ya kuishi kulingana na viwango vya Yehova vya uadilifu. Ili kutimiza uhitaji huo, Ufalme wa Mungu utasimamia kazi kubwa zaidi ya kutoa elimu katika historia yote ya wanadamu.

12. (a) Ni nani watakaowafundisha wasio waadilifu? (b) Ni nini kitakachowapata wale ambao watakataa kufuata mambo watakayojifunza?

12 Ni nani watakaowafundisha wasio waadilifu? Ni umati mkubwa na waadilifu watakaofufuliwa. Ili majina ya wasio waadilifu yaandikwe kwenye kitabu cha uzima, watahitaji kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kujiweka wakfu kwake. Yesu Kristo na wale watakaohukumu pamoja naye, watafuatilia kwa makini maendeleo ya watu hao wasio waadilifu. (Ufu. 20:4) Mtu yeyote ambaye atakataa kukubali msaada huo, ataondolewa​—hata kama atakuwa na umri wa miaka 100. (Isa. 65:20) Yehova na Yesu wanaweza kusoma mioyo na watahakikisha kwamba hakuna mtu atakayeruhusiwa kusababisha uharibifu katika dunia mpya.​—Isa. 11:9; 60:18; 65:25; Yoh. 2:25.

UFUFUO KWENYE UZIMA NA KWENYE HUKUMU

13-14. (a) Zamani, tulielewaje maneno ya Yesu kwenye Yohana 5:29? (b) Tunahitaji kutambua jambo gani kuhusu maneno hayo?

13 Yesu pia alizungumza kuhusu wale watakaofufuliwa hapa duniani. Kwa mfano, alisema: “Saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mema kwenye ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yoh. 5:28, 29) Yesu alimaanisha nini?

14 Zamani, uelewaji wetu ulikuwa kwamba maneno ya Yesu yanarejelea matendo ambayo wale watakaofufuliwa watatenda baada ya kufufuliwa; yaani, baadhi yao watafufuliwa na kutenda mambo mema na wengine watafufuliwa na kutenda mambo mabaya. Hata hivyo, ona kwamba Yesu hasemi wale ambao wametoka tu katika makaburi ya ukumbusho watatenda mambo mema au watazoea kutenda mambo maovu. Anazungumzia matukio ya wakati uliopita. Anazungumza kuhusu watu “waliotenda mema” na wale “waliozoea kutenda maovu.” Hilo linaonyesha kwamba walifanya matendo hayo kabla ya kufa. Hilo linapatana na akili, sivyo? Kwa sababu hakuna mtu atakayeruhusiwa kutenda maovu katika ulimwengu mpya. Ni lazima iwe kwamba wasio waadilifu walizoea kutenda matendo hayo maovu kabla ya kufa. Basi, tunapaswa kuelewaje maneno ya Yesu kuhusu “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu”?

15. Ni nani ambao watapata “ufufuo wa uzima,” na kwa nini?

15 Waadilifu, ambao walitenda mambo mazuri kabla ya kufa, watapata “ufufuo wa uzima” kwa sababu tayari majina yao yatakuwa yameandikwa katika kitabu cha uzima. Hilo linamaanisha kwamba ufufuo wa “wale waliotenda mema” unaofafanuliwa kwenye Yohana 5:29, ni sawa na ufufuo wa “waadilifu” unaotajwa kwenye Matendo 24:15. Uelewaji huu unapatana na maneno ya andiko la Waroma 6:7, linalosema hivi: “Yule ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” Dhambi ambazo waadilifu hao walitenda zilifutwa walipokufa, lakini rekodi yao ya uaminifu bado ipo. (Ebr. 6:10) Bila shaka, waadilifu hao ambao watafufuliwa watahitaji kuendelea kuwa waaminifu ili majina yao yabaki katika kitabu cha uzima.

16. “Ufufuo wa hukumu” unamaanisha nini?

16 Namna gani wale waliozoea kutenda maovu kabla ya kufa? Ingawa dhambi zao zilifutwa walipokufa, hawakuwa na rekodi ya uaminifu. Majina yao hayakuwa yameandikwa katika kitabu cha uzima. Basi, ufufuo wa “wale waliozoea kutenda maovu” ni sawa na ufufuo wa “wasio waadilifu” unaotajwa kwenye Matendo 24:15. Watapata “ufufuo wa hukumu.” c Wasio waadilifu watahukumiwa katika maana ya kwamba Yesu atachunguza na kupima matendo yao. (Luka 22:30) Muda utahitaji kupita kabla ya kuamua ikiwa majina yao yanastahili kuandikwa kwenye kitabu cha uzima. Ikiwa watu hao wasio waadilifu watakubali kubadili mwenendo wao mwovu wa zamani na kujiweka wakfu kwa Yehova, ndipo majina yao yatakapoandikwa kwenye kitabu cha uzima.

17-18. Wote watakaofufuliwa duniani watahitaji kufanya nini, na matendo yanayotajwa kwenye Ufunuo 20:12, 13 yanamaanisha nini?

17 Iwe zamani walikuwa waadilifu au wasio waadilifu, wale watakaofufuliwa watahitaji kutii sheria zitakazokuwa kwenye vitabu vipya vya kukunjwa ambavyo vitafunguliwa wakati wa ile miaka 1,000. Mtume Yohana alifafanua hivi mambo aliyoona kwenye maono: “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wakiwa wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme, na vitabu vya kukunjwa vikafunguliwa. Lakini kitabu kingine cha kukunjwa kikafunguliwa; hicho ni kitabu cha uzima. Wafu wakahukumiwa kutokana na yale mambo yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao.”—Ufu. 20:12, 13.

18 Wale watakaofufuliwa watahukumiwa kwa msingi wa “matendo” gani? Je, ni matendo waliyotenda kabla ya kufa? Hapana! Kumbuka kwamba dhambi zao za zamani ziliondolewa walipokufa. Basi, “matendo yao” hayawezi kuwa matendo waliyofanya katika maisha yao ya zamani. Badala yake, matendo hayo yanamaanisha jinsi watakavyotenda baada ya kufundishwa katika ulimwengu mpya. Hata wanaume waaminifu kama vile Noa, Samweli, Daudi, na Danieli watahitaji kujifunza kumhusu Yesu Kristo na kuonyesha imani katika dhabihu yake. Wasio waadilifu watahitaji kujifunza mengi hata zaidi!

19. Mwishowe, itakuwaje kwa wale watakaokataa nafasi hiyo ya pekee?

19 Mwishowe, itakuwaje kwa wale ambao watakataa nafasi hiyo ya pekee? Ufunuo 20:15 inasema: “Yeyote ambaye hakupatikana ameandikwa katika kile kitabu cha uzima alitupwa ndani ya lile ziwa la moto.” Naam, wataangamizwa kabisa milele. Basi, ni muhimu kwamba tuhakikishe jina letu limeandikwa katika kitabu cha uzima na kuendelea kubaki humo!

Ndugu akishiriki katika kazi kubwa ya kutoa elimu itakayofanywa wakati wa ile Miaka Elfu Moja (Tazama fungu la 20)

20. Ni kazi gani yenye kusisimua ambayo itafanywa wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja? (Tazama picha kwenye jalada.)

20 Kipindi cha Utawala wa Miaka Elfu Moja kitakuwa chenye kusisimua sana! Kitatia ndani kazi kubwa zaidi ya kutoa elimu ambayo imewahi kufanywa hapa duniani. Lakini pia, kitakuwa kipindi ambacho mwenendo wa waadilifu na wasio waadilifu utachunguzwa na kupimwa. (Isa. 26:9; Mdo. 17:31) Kazi hiyo ya kutoa elimu itafanywaje? Makala inayofuata itatusaidia kuelewa na kuthamini maandalizi hayo ya pekee.

WIMBO 147 Uzima wa Milele Umeahidiwa

a Makala hii itazungumzia marekebisho katika uelewaji wetu wa maneno ya Yesu yaliyoandikwa kwenye Yohana 5:28, 29 kuhusu “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu.” Tutajifunza maana ya aina hizo mbili za ufufuo na wale wanaohusika katika kila kisa.

b Kitabu hicho kilianza kuandikwa “tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu,” yaani, ulimwengu wa watu ambao wanaweza kukombolewa kutoka kwa dhambi. (Mt. 25:34; Ufu. 17:8) Basi, inaonekana kwamba jina la Abeli mwadilifu ndilo jina lililoandikwa kwanza katika kitabu cha uzima.

c Zamani, tulifafanua kwamba neno “hukumu” linalotumiwa hapa linamaanisha hukumu isiyofaa, au kupatikana na hatia. Kwa kweli, neno “hukumu” linaweza kuwa na maana hiyo. Lakini katika muktadha huu, inaonekana kwamba Yesu alitumia neno “hukumu” katika maana pana zaidi, akimaanisha kuchunguza na kupima mwenendo au kama kamusi moja ya Kigiriki inavyosema, “kuchanganua tabia.”