MAKALA YA 25

Msiwakwaze “Hawa Wadogo”

Msiwakwaze “Hawa Wadogo”

“Msimdharau mmoja wa hawa wadogo.”—MT. 18:10.

WIMBO 113 Amani Tuliyo Nayo

MUHTASARI a

1. Yehova amefanya nini kwa ajili ya kila mmoja wetu?

 YEHOVA amemvuta kila mmoja wetu kwake. (Yoh. 6:44) Hilo linamaanisha nini? Yehova alipochunguza mabilioni ya watu katika ulimwengu huu, aliona kitu fulani chenye thamani ndani yako—moyo mnyoofu ambao ungekuja kumpenda. (1 Nya. 28:9) Yehova anakujua, anakuelewa, na anakupenda. Inafariji sana kujua hilo!

2. Yesu alitoa mfano gani ili kuonyesha jinsi Yehova anavyomthamini kila mmoja wa kondoo Wake?

2 Yehova anakujali sana, na pia anawajali ndugu na dada zetu Wakristo. Ili kufafanua jambo hilo, Yesu alimlinganisha Yehova na mchungaji. Ikiwa kondoo 1 kati ya 100 anapotea, mchungaji atafanya nini? ‘Atawaacha wale 99 mlimani na kwenda kumtafuta yule aliyepotea.’ Mchungaji anapompata kondoo, hatamkasirikia kwa sababu alipotea. Atashangilia. Wazo kuu ni nini? Kila kondoo ni mwenye thamani kwa Yehova. Yesu alisema hivi: “Baba yangu aliye mbinguni hapendi hata mmoja wa hawa wadogo aangamie.”—Mt. 18:12-14.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Kwa kweli, hatungependa kamwe kumvunja moyo ndugu au dada yetu yeyote. Tunaweza kuepukaje kuwakwaza wengine? Na tunaweza kufanya nini ikiwa ndugu au dada yetu atatuumiza? Tutajibu maswali hayo katika makala hii. Lakini kwanza, acheni tujifunze mengi zaidi kuhusu “hawa wadogo” wanaorejelewa kwenye Mathayo sura ya 18.

“HAWA WADOGO” NI AKINA NANI?

4. “Hawa wadogo” ni akina nani?

4 Maneno “hawa wadogo” yanawarejelea wanafunzi wa Yesu walio na umri tofauti-tofauti. Haidhuru umri wao halisi, wao ni “kama watoto wadogo” katika maana ya kwamba wako tayari kufundishwa na Yesu. (Mt. 18:3) Ingawa wana malezi, utamaduni, maoni, na utu unaotofautiana, wote wanamwamini Kristo. Naye Kristo anawapenda sana.—Mt. 18:6; Yoh. 1:12.

5. Yehova anahisije mtu fulani anapomkwaza au kumuumiza mmoja kati ya watu Wake?

5 Wote wanaorejelewa kuwa “hawa wadogo,” ni wenye thamani kwa Yehova. Ili kuelewa jinsi Yehova anavyohisi, fikiria jinsi unavyohisi kuhusu watoto. Tunawapenda na kuwathamini sana. Tunataka kuwalinda kwa sababu hawana nguvu, uzoefu, na hekima kama ya watu wazima. Ingawa hatupendi kuona mtu yeyote akiumizwa, tunaudhika zaidi—hata kukasirika—tunapoona mtu fulani akimuumiza mtoto. Vivyo hivyo, Yehova anataka kutulinda. Naye huudhika—hata kukasirika—mtu fulani anapomkwaza au kumuumiza mmoja kati ya watu Wake!—Isa. 63:9; Marko 9:42.

6. Kulingana na 1 Wakorintho 1:26-29, ulimwengu unawaonaje wanafunzi wa Yesu?

6 Ni kwa njia gani nyingine wanafunzi wa Yesu ni “wadogo”? Ulimwengu unawaona watu gani kuwa muhimu? Matajiri, watu mashuhuri, na wenye mamlaka. Kinyume na hilo, wanafunzi wa Yesu wanaonekana kuwa watu wasio muhimu, watu “wadogo” ambao si kitu. (Soma 1 Wakorintho 1:26-29.) Lakini Yehova hawaoni kwa njia hiyo.

7. Yehova anataka tuhisije kuhusu ndugu na dada zetu?

7 Yehova anawapenda watumishi wake wote, iwe wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi au ni wapya katika kweli. Ndugu na dada zetu wote ni wenye thamani kwa Yehova, hivyo sisi pia tunapaswa kuwaona kuwa wenye thamani. Tunataka ‘kuupenda ushirika mzima wa akina ndugu,’ na si baadhi yao tu. (1 Pet. 2:17) Tunapaswa kuwa tayari kufanya yote tunayoweza ili kuwalinda na kuwatunza ndugu na dada zetu. Ikiwa tutagundua kwamba tumemuumiza au kumkasirisha ndugu au dada yetu, hatupaswi kupuuza jambo hilo na kufikiri kwamba ndugu yetu anachokozeka kirahisi na kwamba anapaswa kusamehe na kusahau. Kwa nini baadhi ya ndugu na dada wanaweza kukwazika? Labda kwa sababu ya malezi yao, baadhi ya ndugu na dada wanajiona kuwa duni kuliko wengine. Wengine ni wapya katika kweli, bado hawajajifunza jinsi ya kushughulika na hali ya kutokamilika ya wengine. Vyovyote vile, tunapaswa kufanya yote tunayoweza ili kurudisha amani. Kwa kuongezea, mtu anayekwazwa mara kwa mara na wengine anahitaji kutambua kwamba sifa hiyo si nzuri na anahitaji kuifanyia kazi. Anahitaji kufanya hivyo ili awe na amani ya akili na kwa ajili ya hali njema ya wengine.

WAONE WENGINE KUWA BORA KULIKO WEWE

8. Wanafunzi wa Yesu waliathiriwa na mtazamo gani uliokuwa umeenea?

8 Ni nini kilichomchochea Yesu azungumze kuhusu “hawa wadogo”? Wanafunzi wake walikuwa wamemuuliza swali hili: “Kwa kweli ni nani aliye mkuu zaidi katika Ufalme wa mbinguni?” (Mt. 18:1) Wakati huo, Wayahudi wengi waliona nyadhifa na vyeo kuwa jambo muhimu sana. Msomi mmoja anasema hivi: “Wanaume walitanguliza maishani kutafuta heshima, sifa, umashuhuri, staha, na kukubaliwa na watu, na walikuwa tayari kufa kwa ajili ya vitu hivyo.”

9. Wanafunzi wa Yesu walihitaji kufanya nini?

9 Yesu alijua kwamba wanafunzi wake walihitaji kujitahidi kung’oa roho ya mashindano ambayo ilikuwa imekita mizizi katika utamaduni wa Wayahudi. Aliwaambia hivi: “Yule aliye mkuu zaidi kati yenu anapaswa kuwa mdogo zaidi, na yule anayeongoza awe kama anayehudumu.” (Luka 22:26) Tunajiendesha kama “mdogo zaidi” tunapowaona “wengine kuwa bora kuliko” sisi. (Flp. 2:3) Kadiri tunavyositawisha mtazamo huo, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwetu kutowakwaza wengine.

10. Ni shauri gani la mtume Paulo tunalopaswa kuchukua kwa uzito?

10 Ndugu na dada zetu wote ni bora kuliko sisi katika njia moja au nyingine. Ni rahisi kuona hilo, ikiwa tutakazia sifa zao nzuri. Tunapaswa kuchukua kwa uzito shauri hili ambalo mtume Paulo aliwapa Wakorintho: “Ni nani anayekufanya wewe kuwa tofauti na mwingine? Kwa kweli, una nini ambacho hukupokea? Basi, ikiwa kwa kweli ulikipokea, kwa nini unajisifu kana kwamba hukukipokea?” (1 Kor. 4:7) Tunapaswa kuwa makini kutambua mwelekeo wowote wa kujikazia uangalifu sisi wenyewe, au kufikiri kwamba sisi ni bora kuliko wengine. Ikiwa ndugu hutoa hotuba zenye kusisimua au dada ana kipawa cha kuanzisha mafunzo ya Biblia, sikuzote wanapaswa kumpa utukufu Yehova.

SAMEHE “KUTOKA MOYONI”

11. Wazo kuu la mfano wa Yesu kuhusu mfalme na mtumwa ni gani?

11 Baada ya Yesu kuwaonya wafuasi wake kuhusu kuwakwaza wengine, aliwatolea mfano wa mfalme na mtumwa wake. Mfalme alifuta deni ambalo mtumwa huyo hangefaulu kulipa kamwe. Baadaye, mtumwa huyo hakuwa tayari kufuta deni la mtumwa mwenzake lililokuwa dogo zaidi. Mwishowe, mfalme alimtupa mtumwa huyo asiye na rehema gerezani. Tunapata somo gani? Yesu alisema hivi: “Baba yangu wa mbinguni atawatendea ninyi vivyo hivyo ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni.”—Mt. 18:21-35.

12. Tunawaumizaje wengine tunapokataa kuwasamehe?

12 Matendo ya mtumwa huyo hayakumwathiri yeye tu, bali na wengine pia. Kwanza, alimuumiza sana mtumwa mwenzake kwa kutomwonyesha rehema na kuamuru “atupwe gerezani mpaka alipe deni lake.” Pili, aliwaumiza watumwa wengine walioona jambo alilofanya. “Watumwa wenzake walipoona jambo hilo, wakahuzunika sana.” Vivyo hivyo, matendo yetu huwaathiri wengine. Ikiwa ndugu au dada yetu atatukosea na tukakataa kumsamehe, ni nini kitakachotokea? Kwanza, tutamuumiza kwa kukataa kumsamehe, kumwonyesha ufikirio, na upendo. Pili, tunawafanya wengine kutanikoni wakose amani wanapotambua kwamba hatuelewani na ndugu yetu.

Je, utaweka kinyongo au utasamehe kutoka moyoni? (Tazama fungu la 13 na 14) b

13. Unajifunza nini kutokana na kisa cha painia mmoja?

13 Tunapowasamehe ndugu na dada zetu, tunajinufaisha sisi wenyewe na wengine pia. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa dada painia ambaye tutamwita Crystal. Aliumizwa na dada mwingine kutanikoni. Crystal anakumbuka hivi: “Maneno yasiyo ya upendo ya dada huyo, nyakati nyingine yalinichoma kama kisu. Katika huduma, hata sikutaka tupangwe katika kikundi kimoja. Nilianza kupoteza bidii na shangwe yangu.” Crystal alifikiri kwamba alikuwa na sababu nzuri ya kukasirika. Lakini hakuweka kinyongo au kujifikiria mwenyewe na hisia zake. Kwa unyenyekevu alitumia shauri la Kimaandiko linalopatikana kwenye makala “Samehe Kutoka Katika Moyo Wako,” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1999. Crystal alimsamehe dada yake. Anasema hivi: “Sasa ninatambua kwamba sote tunajitahidi kuvaa utu mpya na kwamba Yehova anatusamehe kila siku na kwa hiari. Ninahisi kana kwamba nimetua mzigo mzito sana uliokuwa mabegani mwangu. Shangwe yangu imerudi tena.”

14. Kulingana na Mathayo 18:21, 22, inaonekana mtume Petro alikabili changamoto gani, na unajifunza nini kutokana na jibu la Yesu?

14 Tunajua kwamba tunapaswa kusamehe; kufanya hivyo ni jambo linalofaa. Lakini huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Huenda mtume Petro alihisi hivyo nyakati fulani. (Soma Mathayo 18:21, 22.) Ni nini kinachoweza kutusaidia? Kwanza, tafakari kuhusu jinsi Yehova anavyokusamehe mara nyingi. (Mt. 18:32, 33) Hatustahili msamaha wa Yehova, lakini anatusamehe kwa hiari. (Zab. 103:8-10) Wakati huohuo, “sisi pia tuna wajibu wa kupendana.” Hivyo, kuwasamehe wengine si jambo la hiari. Tuna wajibu wa kuwasamehe ndugu na dada zetu. (1 Yoh. 4:11) Pili, tafakari kile kinachotokea tunaposamehe. Tunaweza kumsaidia yule aliyetukosea, kuunganisha kutaniko, kulinda urafiki wetu na Yehova, na kupata kitulizo kwa kutua mzigo tuliokuwa tumebeba. (2 Kor. 2:7; Kol. 3:14) Mwishowe, sali kwa yule anayetuhimiza tuwasamehe wengine. Usimruhusu Shetani aharibu amani unayofurahia pamoja na waabudu wenzako. (Efe. 4:26, 27) Tunahitaji msaada wa Yehova ili tuepuke kunaswa na mtego wa Shetani.

USIRUHUSU UKWAZIKE

15. Kulingana na Wakolosai 3:13, tunaweza kufanya nini ikiwa tutaumizwa na matendo ya ndugu au dada yetu?

15 Hata hivyo, namna gani ikiwa mwamini mwenzako ametenda kwa njia inayokuumiza sana? Unapaswa kufanya nini? Jitahidi kufanya yote unayoweza ili kudumisha amani. Sali kwa Yehova kutoka moyoni. Mwombe Yehova ambariki mtu aliyekukosea na akusaidie kuona sifa nzuri ambazo ndugu au dada huyo anazo—sifa zilezile ambazo zinamfanya Yehova ampende. (Luka 6:28) Ikiwa huwezi kupuuza jambo ambalo ndugu yako amefanya, fikiria jinsi unavyoweza kuzungumza naye. Sikuzote ni bora kufikiri kwamba kamwe ndugu huyo hawezi kukuumiza kwa kukusudia. (Mt. 5:23, 24; 1 Kor. 13:7) Unapozungumza naye, wazia kwamba ana nia nzuri. Lakini namna gani ikiwa hataki kufanya amani? ‘Endelea kumvumilia.’ Usikate tamaa. (Soma Wakolosai 3:13.) Jambo la muhimu hata zaidi, usiweke kinyongo kwa sababu kinaweza kuharibu uhusiano wako pamoja na Yehova. Usiruhusu kitu chochote kikukwaze. Kwa kufanya hivyo, utathibitisha kwamba unampenda Yehova kuliko kitu kingine chochote.—Zab. 119:165.

16. Kila mmoja wetu ana wajibu gani?

16 Tunathamini pendeleo la kumtumikia Yehova kwa umoja tukiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja”! (Yoh. 10:16) Kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 165, kinasema hivi: “Ili ufaidike na umoja huo, una jukumu la kuudumisha.” Hivyo, tunahitaji ‘kujizoeza kuwaona ndugu na dada zetu kama Yehova anavyowaona.’ Machoni pa Yehova sisi sote ni “wadogo” walio na thamani. Je, hivyo ndiyo unavyowaona ndugu na dada zako? Yehova anaona na kuthamini kila kitu unachofanya ili kuwasaidia na kuwatunza.—Mt. 10:42.

17. Tumeazimia kufanya nini?

17 Tunawapenda waabudu wenzetu. Hivyo, ‘tumeazimia kutoweka kikwazo au kizuizi mbele ya ndugu’ zetu. (Rom. 14:13) Tunawaona ndugu na dada zetu kuwa bora kuliko sisi na tunataka kuwasamehe kutoka moyoni. Na tusikubali kukwazwa na wengine. Badala yake, acheni tuchague kufuatilia “mambo yanayoleta amani na mambo ya kujengana.”—Rom. 14:19.

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

a Kwa sababu ya kutokamilika, huenda tukafanya au kusema jambo linaloweza kuwaumiza ndugu na dada zetu. Tunapaswa kufanya nini hilo likitokea? Je, tutajitahidi kurudisha uhusiano wetu na ndugu na dada zetu? Je, tutakuwa tayari kuomba msamaha haraka? Au je, tunasema ikiwa wameumia hilo ni tatizo lao, si letu? Au namna gani ikiwa mara kwa mara tunakasirishwa na maneno au matendo ya wengine? Je, tunatoa kisingizio kwamba hivyo ndivyo tulivyo​—huo ndio utu wetu? Au je, tunaona njia yetu ya kushughulikia hali hiyo kuwa udhaifu ambao tunahitaji kuufanyia kazi?

b MAELEZO YA PICHA: Dada amekasirishwa na dada mwingine kutanikoni. Baada ya kusuluhisha tatizo lao faraghani, wanalisahau na wanaendelea kutumikia pamoja kwa furaha.