SOMO LA 04

Mungu Ni Nani?

Mungu Ni Nani?

Katika historia yote, wanadamu wameabudu miungu ya aina mbalimbali. Hata hivyo, Biblia inamtaja Mungu mmoja ambaye “ni mkuu kuliko miungu mingine yote.” (2 Mambo ya Nyakati 2:5) Ni Mungu gani huyo? Na kwa nini ni mkuu kuliko miungu mingine yote ambayo watu huabudu? Katika somo hili, utajifunza jinsi Mungu huyo anavyojitambulisha kwako.

1. Mungu anaitwa nani, na ni nini kinachoonyesha kwamba anataka tulijue jina lake?

Mungu anajitambulisha kwetu kupitia Biblia. Anasema: “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu.” (Soma Isaya 42:5, 8.) Jina “Yehova” limetafsiriwa kutoka katika Kiebrania na linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Yehova anataka ulijue jina lake, na ulitumie. (Kutoka 3:​15) Tunajuaje jambo hilo? Alihakikisha kwamba jina lake linapatikana zaidi ya mara 7,000 katika Biblia! a Jina Yehova ni la “Mungu wa kweli juu mbinguni na chini duniani.”​​—Kumbukumbu la Torati 4:​39.

2. Biblia inatufundisha nini kumhusu Yehova?

Biblia inasema kwamba kati ya miungu yote ambayo watu huabudu, Yehova ndiye Mungu pekee wa kweli. Kwa nini? Kuna sababu kadhaa. Yehova ndiye mwenye mamlaka yote, na yeye ndiye aliye “Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Soma Zaburi 83:18.) Yeye ndiye “Mweza-Yote,” kwa sababu ana uwezo wa kufanya chochote anachotaka kufanya. Yeye ndiye ‘aliyeumba vitu vyote,’ kutia ndani ulimwengu na kila kitu kilicho hai duniani. (Ufunuo 4:​8, 11) Yehova peke yake ndiye amekuwepo sikuzote, na ataendelea kuwepo milele.​—Zaburi 90:2.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza tofauti kati ya majina ya cheo ya Mungu na jina lake la kibinafsi. Kisha ujifunze jinsi ambavyo amekujulisha jina lake na kwa nini amefanya hivyo.

3. Mungu ana majina mengi ya cheo, lakini ana jina moja la kibinafsi

Ili kuona tofauti kati ya cheo cha mtu na jina lake la kibinafsi, onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kuna tofauti gani kati ya jina la cheo kama vile “Bwana,” na jina la kibinafsi?

Biblia inasema kwamba watu huabudu miungu mingi na mabwana wengi. Soma Zaburi 136:1-3, kisha mzungumzie swali hili:

  • “Mungu wa miungu” na “Bwana wa mabwana” ni nani?

4. Yehova anataka ujue na kulitumia jina lake

Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anataka ulijue jina lake? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Unafikiri Yehova anataka watu walijue jina lake? Kwa nini?

Yehova anataka watu walitumie jina lake. Soma Waroma 10:13, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kwa nini tunapaswa kutumia jina Yehova?

  • Wewe unahisije mtu anapokumbuka jina lako na kulitumia?

  • Unafikiri Yehova anahisije unapolitumia jina lake?

5. Yehova anataka uwe rafiki yake

Mwanamke fulani kutoka Kambodia anayeitwa Soten alisema kwamba kujua jina la Mungu kulimletea “hisia za kipekee.” Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali hili:

  • Katika video hiyo, Soten alihisije baada ya kujua jina la Mungu?

Kwa kawaida, ili mtu awe rafiki yako unapaswa kulijua jina lake. Soma Yakobo 4:8a, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yehova anataka ufanye nini?

  • Kujua na kulitumia jina la Mungu kutakusaidiaje uwe rafiki yake?

WATU FULANI HUSEMA: “Kuna Mungu mmoja tu, na unaweza kumwita jina lolote.”

  • Je, unaamini kwamba jina la Mungu ni Yehova?

  • Unaweza kutoa sababu gani ili kuonyesha kwamba Mungu anataka tulitumie jina lake?

MUHTASARI

Yehova ni jina la Mungu pekee wa kweli. Anataka tulijue na kulitumia jina hilo ili tuwe rafiki zake.

Ungejibuje?

  • Kwa nini Yehova ni tofauti na miungu mingine ambayo watu huabudu?

  • Kwa nini tunapaswa kulitumia jina la Mungu?

  • Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anataka uwe rafiki yake?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza sababu tano zenye kusadikisha zinazothibitisha kwamba kuna Mungu.

“Je, Kuna Mungu?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Chunguza kwa nini inapatana na akili kuamini kwamba Mungu amekuwepo sikuzote.

“Ni Nani Aliyemuumba Mungu?” (Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 2014)

Jifunze kwa nini tunapaswa kutumia jina la Mungu, hata kama hatujui jinsi lilivyotamkwa nyakati za kale.

“Yehova Ni Nani?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Je, tunaweza kumwita Mungu kwa jina lolote tunalopenda? Ona kwa nini tunaweza kusema kwamba ana jina moja tu la kibinafsi.

“Mungu Ana Majina Mangapi?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

a Ili kupata habari zaidi kuhusu maana ya jina la Mungu na kwa nini limeondolewa katika baadhi ya tafsiri za Biblia ona Nyongeza A4 katika Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.