SOMO LA 06

Uhai Ulianzaje?

Uhai Ulianzaje?

“[Mungu] ndiye chanzo cha uhai.” (Zaburi 36:9) Je, unaamini hivyo? Watu fulani wanafikiri kwamba uhai haukuumbwa, bali ulijitokeza wenyewe. Ikiwa hilo ni kweli, basi tuko hai kwa sababu ya tukio ambalo halikupangiwa. Lakini ikiwa Yehova ndiye aliyeumba uhai, bila shaka maisha yetu yana kusudi. a Chunguza jinsi Biblia inavyoeleza kuhusu chanzo cha uhai na kwa nini tunaweza kuamini kwamba inasema ukweli.

1. Ulimwengu ulitoka wapi?

Biblia inasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Wanasayansi wengi wanakubali kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Mungu aliumbaje ulimwengu? Alitumia ‘nguvu yake ya utendaji,’ yaani, roho yake takatifu kuumba kila kitu ulimwenguni kutia ndani nyota na sayari.​—Mwanzo 1:2.

2. Kwa nini Mungu aliumba dunia?

Yehova “hakuiumba [dunia] tu bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.” (Isaya 45:18) Aliumba dunia ikiwa mahali pazuri pa kuishi na makao ya kudumu ya wanadamu. (Soma Isaya 40:28; 42:5.) Sayansi inathibitisha kwamba dunia ni sayari ya kipekee. Dunia ndiyo sayari pekee inayoweza kuendeleza uhai wa wanadamu.

3. Ni nini kinachofanya wanadamu wawe tofauti na wanyama?

Baada ya kuumba dunia, Yehova aliumba viumbe. Kwanza, aliumba mimea na wanyama duniani. Kisha, “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake.” (Soma Mwanzo 1:​27.) Kwa nini wanadamu ni viumbe wa kipekee? Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, kwa hiyo tunaweza kuonyesha sifa zake kama vile upendo na haki. Vilevile alituumba tukiwa na uwezo wa kujifunza lugha, kufurahia vitu maridadi, na muziki. Tofauti na wanyama, tunaweza kumwabudu Muumba wetu.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza mambo yanayothibitisha kwamba uhai uliumbwa na kwamba simulizi la Biblia kuhusu uumbaji linapatana na akili. Jifunze mambo ambayo sifa za wanadamu zinatufundisha kumhusu Mungu.

4. Uhai uliumbwa

Wanadamu husifiwa wanapotengeneza vitu kwa kuiga muundo wa vitu vya asili. Basi ni nani anayepaswa kusifiwa kwa kuumba vitu vya asili? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali hili:

  • Wanadamu wamebuni vitu gani kwa kuiga muundo wa vitu vya asili?

Kila nyumba ilibuniwa na kujengwa na mtu fulani. Lakini ni nani aliyebuni na kuumba vitu vya asili? Soma Waebrania 3:4, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Wewe unavutiwa zaidi na vitu gani vya asili?

  • Je, inapatana na akili kuamini kwamba ulimwengu na kila kitu kilichomo kiliumbwa? Kwa nini?

Je, wajua?

Unaweza kupata makala na video kuhusu habari hii kwenye mfululizo huu “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” na “Maoni Kuhusu Chanzo cha Uhai.

“Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yule aliyevijenga vitu vyote ni Mungu”

5. Simulizi la Biblia kuhusu uumbaji linapatana na akili

Katika Mwanzo sura ya 1, Biblia inaeleza kuhusu chanzo cha dunia na uhai uliomo. Je, unaamini simulizi hilo, au je, ni hadithi ya kutungwa? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, Biblia inafundisha kwamba dunia na uhai uliomo uliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24?

  • Je, unafikiri simulizi la Biblia kuhusu uumbaji ni sahihi na linapatana na akili? Kwa nini?

Soma Mwanzo 1:1, kisha mzungumzie swali hili:

  • Wanasayansi wanasema kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Maoni yao yanapatanaje na jambo ambalo umesoma katika Biblia?

Baadhi ya watu hufikiri kwamba Mungu alitumia mageuzi kuumba uhai. Soma Mwanzo 1:21, 25, 27, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, Biblia inafundisha kwamba Mungu aliumba uhai wa hali ya chini akauacha ujigeuze kuwa samaki, kisha mnyama, na mwishowe kuwa mwanadamu? Au je, aliumba “aina” mbalimbali za uhai? b

6. Wanadamu ni viumbe wa kipekee wa Mungu

Sisi ni tofauti na wanyama ambao Yehova aliumba. Soma Mwanzo 1:26, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, uwezo wetu wa kuonyesha upendo na huruma unatufundisha Mungu ana sifa gani?

WATU FULANI HUSEMA: “Simulizi la Biblia kuhusu uumbaji ni hadithi ya kutungwa.”

  • Wewe una maoni gani? Kwa nini?

MUHTASARI

Yehova aliumba ulimwengu na uhai wa kila aina.

Ungejibuje?

  • Biblia inafundisha nini kuhusu chanzo cha ulimwengu?

  • Je, Mungu aliumba uhai wa hali ya chini kisha akauacha ujigeuze na kutokeza aina mbalimbali ya viumbe, au je, aliumba viumbe vyote?

  • Kwa nini wanadamu ni viumbe wa kipekee?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ona jinsi vitu vya asili vinavyothibitisha kwamba kuna Muumba.

“Vitu vya Asili Vinatufundisha Nini?” (Amkeni!, Septemba 2006)

Ona jinsi baba anavyomfafanulia mwanaye simulizi la Biblia kuhusu uumbaji.

‘Yehova Aliumba Vitu Vyote’ (2:36)

Chunguza kama utafiti wa kisayansi wa vitu vya kale unathibitisha kwamba uhai uliumbwa au ulijitokeza wenyewe.

Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai (broshua)

a Somo la 25 litazungumzia Mungu ana kusudi gani kwa wanadamu.

b Katika Biblia, neno “aina” linarejelea kundi kubwa la vitu vilivyo hai.