SOMO LA 08

Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova

Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova

Yehova anataka umjue vizuri. Kwa nini? Anatarajia kwamba kadiri unavyojifunza kuhusu sifa zake, njia zake na kusudi lake, ndivyo utakavyotamani kuwa rafiki yake. Je, wewe unaweza kuwa rafiki ya Mungu? (Soma Zaburi 25:14.) Unapaswa kufanya nini ili uwe rafiki yake? Biblia inajibu maswali hayo na inaeleza kwa nini urafiki pamoja na Yehova ndio urafiki bora zaidi kuliko urafiki mwingine wowote.

1. Yehova anakualika ufanye nini?

‘Mkaribie Mungu, naye atakukaribia.’ (Yakobo 4:8) Hilo linamaanisha nini? Yehova anakualika uwe rafiki yake. Huenda watu fulani wakafikiri kwamba ni vigumu kuwa rafiki ya Mungu kwa sababu hawawezi kumwona. Hata hivyo, katika Neno lake Biblia, Yehova ameeleza mambo yote tunayohitaji kujua kuhusu sifa zake ili tusitawishe urafiki pamoja naye. Tunaposoma ujumbe wa Mungu katika Biblia, urafiki wetu pamoja naye huzidi kukua, ingawa hatujawahi kumwona.

2. Kwa nini Yehova ndiye Rafiki bora zaidi kuliko rafiki mwingine yeyote?

Yehova anakupenda kuliko mtu mwingine yeyote. Anataka uwe na furaha na uzungumze naye wakati wowote unapohitaji msaada. Unaweza ‘kumtupia mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’ (1 Petro 5:7) Sikuzote Yehova yuko tayari kuwasaidia, kuwafariji, na kuwasikiliza rafiki zake.​—Soma Zaburi 94:18, 19.

3. Yehova anatarajia rafiki zake wafanye nini?

Yehova anawapenda watu wote, “lakini ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.” (Methali 3:32) Yehova anatarajia rafiki zake wafanye mambo anayoona kuwa mazuri na waepuke mambo mabaya. Baadhi ya watu hufikiri kwamba hawawezi kufuata kikamili viwango vya Yehova kuhusu mema na mabaya. Hata hivyo, Yehova anatuelewa vizuri. Anamkubali kila mtu anayempenda kikweli na anayefanya yote anayoweza ili kumfurahisha.​—Zaburi 147:11; Matendo 10:34, 35.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze mengi kuhusu jinsi unavyoweza kuwa rafiki ya Yehova, na utambue kwa nini yeye ni Rafiki bora zaidi kuliko rafiki mwingine yeyote.

4. Abrahamu alikuwa rafiki ya Yehova

Simulizi la Biblia kumhusu Abrahamu (anayeitwa pia Abramu) linatusaidia kuelewa jinsi tunavyoweza kuwa rafiki ya Mungu. Soma kumhusu Abrahamu katika Mwanzo 12:1-4. Kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yehova alimwambia Abrahamu afanye nini?

  • Yehova alimwahidi nini?

  • Abrahamu alitendaje baada ya kupokea maagizo ya Yehova?

5. Mambo ambayo Yehova anatarajia kutoka kwa rafiki zake

Kwa kawaida sisi hutazamia mambo fulani kutoka kwa rafiki zetu.

  • Ni mambo gani ambayo ungependa rafiki zako wakufanyie?

Soma 1 Yohana 5:3, kisha mzungumzie swali hili:

  • Yehova anatarajia nini kutoka kwa rafiki zake?

Ili kumtii Yehova, tunapaswa kubadili mwenendo na tabia zetu. Soma Isaya 48:17, 18, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini Yehova anataka rafiki zake wabadili mwenendo na tabia zao?

Rafiki mzuri hutukumbusha kufanya mambo yanayoweza kutulinda na kutunufaisha. Yehova hufanya vivyo hivyo pia kwa rafiki zake

6. Jinsi Yehova anavyowasaidia rafiki zake

Yehova huwasaidia rafiki zake kukabiliana na matatizo. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Yehova amemsaidiaje mwanamke katika video hiyo kukabiliana na mawazo na hisia zisizofaa?

Soma Isaya 41:10, 13, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yehova anaahidi kuwafanyia nini rafiki zake wote?

  • Je, unafikiri Yehova ni rafiki mzuri? Kwa nini?

Rafiki wa karibu watakusaidia unapohitaji msaada. Yehova pia atakusaidia

7. Ili tuwe rafiki za Yehova tunapaswa kuwasiliana naye

Mawasiliano huimarisha urafiki. Soma Zaburi 86:6, 11, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Tunaweza kuzungumza na Yehova kupitia njia gani?

  • Yehova huzungumza nasi kupitia njia gani?

Tunazungumza na Yehova kupitia sala; naye Yehova huzungumza nasi kupitia Biblia

WATU FULANI HUSEMA: “Haiwezekani kuwa rafiki ya Mungu.”

  • Unaweza kutumia andiko gani kuonyesha kwamba inawezekana kuwa rafiki ya Yehova?

MUHTASARI

Yehova anataka kuwa Rafiki yako, na atakusaidia uwe na uhusiano wa karibu pamoja naye.

Ungejibuje?

  • Yehova huwasaidiaje rafiki zake?

  • Kwa nini Yehova anawaagiza rafiki zake wabadili mwenendo na tabia zao?

  • Je, unafikiri ni vigumu kuwa rafiki ya Yehova? Kwa nini?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Urafiki pamoja na Mungu unaweza kuboreshaje maisha yako?

“Yehova​—Mungu Tunayepaswa Kumjua” (Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 2003)

Jifunze kwa nini mwanamke huyu anahisi kwamba urafiki wake na Yehova ulibadili maisha yake.

“Sikutaka Kufa!” (Mnara wa Mlinzi Na. 1 2017)

Wasikilize vijana wanapoeleza jinsi wanavyohisi kumhusu Yehova.

Inamaanisha Nini Kuwa Rafiki ya Mungu? (1:46)