SOMO LA 15

Yesu Ni Nani?

Yesu Ni Nani?

Yesu ni mmoja kati ya watu maarufu zaidi katika historia. Watu wengi wanajua jina lake, lakini hawajui mengi kumhusu. Na wengine wana maoni mbalimbali kumhusu Yesu. Biblia inafundisha nini kumhusu Yesu?

1. Yesu ni nani?

Yesu ni kiumbe wa roho mwenye nguvu anayeishi mbinguni. Yehova Mungu alimuumba kwanza kabla ya vitu vingine vyote. Ndiyo sababu anaitwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Wakolosai 1:15) Biblia inamwita Yesu ‘Mwana mzaliwa pekee’ wa Mungu kwa sababu Yesu peke yake ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Yehova. (Yohana 3:16) Yesu alifanya kazi kwa ukaribu na Yehova Baba yake, akimsaidia kuumba vitu vingine vyote. (Soma Methali 8:​30.) Bado Yesu ana uhusiano wa karibu na Yehova. Anatumikia kwa ushikamanifu akiwa msemaji wa Mungu, yaani, “Neno,” akiwasilisha ujumbe na maagizo ya Mungu.​—Yohana 1:14.

2. Kwa nini Yesu alikuja duniani?

Miaka elfu mbili hivi iliyopita, Yehova alitumia roho yake takatifu kuhamisha kimuujiza uhai wa Yesu kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira aliyeitwa Maria. Na kwa njia hiyo, Yesu alizaliwa akiwa mwanadamu. (Soma Luka 1:34, 35.) Yehova alimtuma Yesu duniani ili awe Masihi, au Kristo, na ili awaokoe wanadamu. a Yesu alitimiza unabii wote wa Biblia kumhusu Masihi, na hivyo ikawa rahisi kwa watu kutambua kwamba yeye “ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”​—Mathayo 16:16.

3. Yesu yuko wapi sasa?

Baada ya Yesu kufa akiwa mwanadamu, Yehova alimfufua akiwa kiumbe wa roho na kisha akarudi mbinguni. Akiwa huko, “Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi.” (Wafilipi 2:9) Sasa, Yesu ana mamlaka kubwa sana. Cheo chake ni cha pili kutoka kwa Yehova.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze Yesu ni nani hasa, na kwa nini ni muhimu sana kujifunza kumhusu.

4. Yesu si Mungu Mweza Yote

Ingawa Yesu ni kiumbe wa roho mwenye nguvu mbinguni, Biblia inafundisha kwamba anajitiisha kwa Yehova ambaye ni Mungu wake na Baba yake. Kwa nini tunasema hivyo? Onyesha VIDEO ili uone kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu tofauti kati ya cheo cha Yesu na Mungu mweza yote.

Maandiko yanayofuata yanatusaidia kuelewa uhusiano uliopo kati ya Yehova na Yesu. Soma kila andiko kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

Soma Luka 1:30-32.

  • Malaika alifafanuaje uhusiano uliopo kati ya Yesu na Yehova Mungu, “Aliye Juu Zaidi”?

Soma Mathayo 3:16, 17.

  • Yesu alipobatizwa, sauti kutoka mbinguni ilisema nini?

  • Unafikiri ilikuwa sauti ya nani?

Soma Yohana 14:28.

  • Ni nani aliye na umri mkubwa na mwenye mamlaka zaidi? Je, ni baba au mwana?

  • Yesu alisema Yehova ni Baba yake, hilo linatufundisha nini?

Soma Yohana 12:49.

  • Je, Yesu anahisi kwamba yeye na Baba yake ni mtu yuleyule? Wewe una maoni gani?

5. Ni nini kilichothibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi?

Biblia ina unabii mwingi uliowasaidia watu kumtambua Masihi, yaani, yule aliyechaguliwa na Mungu ili kuwaokoa wanadamu. Onyesha VIDEO ili uone baadhi ya unabii ambao Yesu alitimiza alipokuja duniani.

Soma unabii huu wa Biblia kisha mzungumzie maswali yanayofuata:

Soma Mika 5:2 ili uone mahali ambapo Masihi angezaliwa. b

  • Je, unabii huu ulitimia Yesu alipozaliwa?​—Mathayo 2:1.

Soma Zaburi 34:20 na Zekaria 12:10 uone mambo yaliyotabiriwa kuhusu kifo cha Masihi.

  • Je, unabii huo ulitimizwa?​—Yohana 19:33-37.

  • Je, unafikiri Yesu alipanga ili baadhi ya unabii huo utimie?

  • Hilo linakuthibitishia nini kumhusu Yesu?

6. Tunanufaika tunapojifunza kumhusu Yesu

Biblia inakazia umuhimu wa kujifunza kumhusu Yesu na jukumu lake. Soma Yohana 14:6 na 17:3, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini ni muhimu kujifunza kumhusu Yesu?

Yesu alifungua njia ya kuwa rafiki ya Mungu. Alifundisha kweli kumhusu Yehova, na kupitia kwake tunaweza kupata uzima wa milele

WATU FULANI HUSEMA: “Mashahidi wa Yehova hawamwamini Yesu.”

  • Ungemjibuje mtu anayesema hivyo?

MUHTASARI

Yesu ni kiumbe wa roho mwenye nguvu. Yeye ni Mwana wa Mungu na ndiye Masihi.

Ungejibuje?

  • Kwa nini Yesu anaitwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote”?

  • Yesu alifanya kazi gani kabla ya kuja duniani?

  • Tunajuaje kwamba Yesu ndiye Masihi?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza uone ikiwa Biblia inafundisha kwamba Mungu alikuwa Baba mzazi wa Yesu jinsi ambavyo wanadamu huzaliwa.

“Kwa Nini Yesu Anaitwa Mwana wa Mungu?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Chunguza kwa nini Biblia haiungi mkono fundisho la Utatu.

“Je, Yesu Ni Mungu?” (Mnara wa Mlinzi, Aprili 1, 2009)

Soma jinsi maisha ya mwanamke fulani yalivyobadilika alipochunguza kile ambacho Biblia inasema kumhusu Yesu.

“Mwanamke Myahudi Anaeleza Sababu Iliyomfanya Achunguze Upya Imani Yake” (Amkeni!, Mei 2013)

a Somo la 26 na 27 litazungumzia kwa nini wanadamu wanahitaji kuokolewa na jinsi Yesu anavyotuokoa.

b Ona Maelezo ya Ziada 2 kuhusu unabii uliotabiri wakati hususa ambao Yesu angekuja duniani.