SOMO LA 23

Ubatizo​—Lengo Muhimu!

Ubatizo​—Lengo Muhimu!

Yesu alifundisha kwamba ni lazima Wakristo wabatizwe. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Lakini ubatizo ni nini? Na mtu anapaswa kufanya nini ili afikie lengo hilo?

1. Ubatizo ni nini?

Neno “batiza” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “zamisha” ndani ya maji. Yesu alipobatizwa, alizamishwa ndani ya Mto Yordani na kisha ‘akatoka katika maji.’ (Marko 1:9, 10) Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli hubatizwa kwa kuzamishwa kabisa ndani ya maji.

2. Ubatizo unamaanisha nini?

Mtu anapobatizwa, anaonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Mtu anajiweka wakfu jinsi gani? Kabla ya kubatizwa, anatoa sala faraghani na kumwambia Yehova kwamba anataka kumtumikia milele. Anaahidi kwamba atamwabudu Yehova peke yake, na jambo muhimu zaidi maishani mwake litakuwa kufanya mapenzi ya Mungu. Anaamua ‘kujikana mwenyewe na kuendelea kufuata’ mafundisho na mfano wa Yesu. (Mathayo 16:24) Kujiweka wakfu na kubatizwa humwezesha mtu kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova na watu wengine wanaomwabudu Yehova.

3. Mtu anapaswa kuchukua hatua gani kabla ya kubatizwa?

Kabla ya kubatizwa, unapaswa kujifunza kumhusu Yehova na kujenga imani yenye nguvu kwake. (Soma Waebrania 11:6.) Kadiri ujuzi na imani yako inavyozidi kuongezeka, ndivyo utakavyompenda Yehova zaidi. Bila shaka, utatamani kuwaambia wengine kumhusu na kuishi kulingana na viwango vyake. (2 Timotheo 4:2; 1 Yohana 5:3) Mtu anapoanza kuishi “kwa kumstahili Yehova ili kumpendeza kikamili,” inawezekana kwamba ataamua kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.​—Wakolosai 1:9, 10. a

CHIMBA ZAIDI

Ona mambo tunayojifunza kutokana na ubatizo wa Yesu na jinsi mtu anavyoweza kujitayarisha ili kuchukua hatua hiyo muhimu.

4. Mambo tunayojifunza kutokana na ubatizo wa Yesu

Soma Mathayo 3:13-17 ili ujifunze mengi kuhusu ubatizo wa Yesu. Kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, Yesu alikuwa mtoto mchanga alipobatizwa?

  • Alibatizwa jinsi gani? Je, alinyunyiziwa maji?

Baada ya kubatizwa, Yesu alianza kufanya kazi ya pekee ambayo Mungu alimpa afanye duniani. Soma Luka 3:21-23 na Yohana 6:38, kisha mzungumzie swali hili:

  • Yesu alitanguliza kazi gani maishani baada ya kubatizwa?

5. Unaweza kufikia lengo la kubatizwa

Mwanzoni huenda ukawa na wasiwasi kuhusu kujiweka wakfu na kubatizwa. Hata hivyo, unaweza kufanya maendeleo hatua kwa hatua na mwishowe kupata ujasiri wa kufanya uamuzi huo muhimu. Ili uone baadhi ya watu waliofanya hivyo, onyesha VIDEO.

Soma Yohana 17:3 na Yakobo 1:5, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu ajitayarishe kwa ajili ya ubatizo?

  1. Tunajiweka wakfu kwa kumwambia Yehova kwamba tunataka kumtumikia milele

  2. Tunapobatizwa tunawaonyesha watazamaji kwamba tumejiweka wakfu kwa Mungu

6. Tunapobatizwa tunajiunga na familia ya Yehova

Tunapobatizwa tunajiunga na familia yenye umoja ya ulimwenguni pote. Ingawa tumetoka katika maeneo na malezi mbalimbali, sisi sote tunaamini mambo yaleyale na tunaishi kulingana na viwango vilevile vya maadili. Soma Zaburi 25:14 na 1 Petro 2:17, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mtu anapobatizwa anakuwa na uhusiano gani na Yehova na watu wengine wanaomwabudu?

WATU FULANI HUSEMA: “Mimi siko tayari kubatizwa.”

  • Ikiwa wewe unahisi hivyo, je, bado unafikiri kwamba ubatizo ni lengo muhimu?

MUHTASARI

Yesu alifundisha kwamba ni lazima Wakristo wabatizwe. Ili kufikia lengo hilo, mtu anapaswa kujenga imani yenye nguvu kwa Yehova, kuishi kulingana na viwango vyake, na kujiweka wakfu kwake.

Ungejibuje?

  • Ubatizo ni nini, na kwa nini ni muhimu kubatizwa?

  • Kuna uhusiano gani kati ya kujiweka wakfu na kubatizwa?

  • Ni hatua gani ambazo mtu anapaswa kuchukua kabla ya kujiweka wakfu na kubatizwa?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Jifunze ukweli kuhusu ubatizo.

“Ubatizo Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Chunguza hatua ambazo mtu anapaswa kuchukua ili kufikia ubatizo.

“Upendo na Uthamini Wetu kwa Yehova Hutuchochea Kubatizwa” (Mnara wa Mlinzi, Machi 2020)

Soma uone kwa nini mwanamume fulani hakuongozwa tu na hisia alipoamua kubatizwa.

“Walitaka Nijithibitishie Ukweli” (Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 2013)

Chunguza kwa nini ubatizo ni lengo muhimu na jinsi unavyoweza kujitayarisha ili ubatizwe.

“Nibatizwe?” (Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, sura ya 37)

a Ikiwa mwanzoni mtu alibatizwa katika dini nyingine, anahitaji kubatizwa tena. Kwa nini? Kwa sababu dini hiyo haikufundisha ukweli ulio katika Biblia.​—Ona Matendo 19:1-5 na Somo la 13.