SOMO LA 26

Kwa Nini Wanadamu Wanateseka na Kupatwa na Mambo Mabaya?

Kwa Nini Wanadamu Wanateseka na Kupatwa na Mambo Mabaya?

Jambo baya linapotokea watu hujiuliza, “Kwa nini jambo hili limetokea?” Tunafurahi sana kujua kwamba Biblia inajibu waziwazi swali hilo!

1. Shetani alianzishaje uovu ulimwenguni?

Shetani Ibilisi alimwasi Mungu. Shetani alitaka kuwatawala viumbe wengine, hivyo aliwashawishi wanadamu wa kwanza Adamu na Hawa wajiunge naye kuasi. Shetani alifanya hivyo alipomdanganya Hawa. (Mwanzo 3:1-5) Alimfanya afikiri kwamba Yehova alikuwa akimnyima jambo fulani zuri. Alidai kwamba wanadamu wangekuwa na furaha zaidi ikiwa hawangemtii Mungu. Shetani alisema uwongo wa kwanza kwa kumdanganya Hawa kwamba hangekufa. Hiyo ndiyo sababu Biblia inamwita Shetani kuwa “mwongo na ndiye baba ya uwongo.”​—Yohana 8:44.

2. Adamu na Hawa waliamua kufanya nini?

Yehova aliwaonyesha Adamu na Hawa ukarimu mwingi. Aliwaambia wangeweza kula matunda ya kila mti katika bustani ya Edeni isipokuwa mti mmoja. (Mwanzo 2:15-17) Hata hivyo, waliamua kula matunda ya mti waliokatazwa. Hawa alianza “kuchuma matunda ya mti huo na kula.” Baadaye, Adamu “akaanza kula.” (Mwanzo 3:6) Wote wawili hawakumtii Mungu. Kwa kuwa Adamu na Hawa walikuwa wakamilifu, walikuwa na uwezo wa kiasili wa kufanya mambo yaliyo sawa. Lakini kwa kutomtii Mungu kimakusudi, walitenda dhambi na kukataa utawala wake. Uamuzi huo uliwasababishia mateso mengi.​—Mwanzo 3:16-19.

3. Uamuzi wa Adamu na Hawa umetuathirije?

Baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi hawakuwa wakamilifu tena, hivyo wakapitisha hali ya kutokamilika kwa wazao wao wote. Biblia inasema hivi kumhusu Adamu: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote.”​—Waroma 5:12.

Kuna sababu nyingi zinazofanya tuteseke. Wakati fulani tunateseka kwa sababu ya maamuzi mabaya tunayofanya, au kwa sababu ya maamuzi mabaya ya watu wengine. Na wakati mwingine tunateseka kwa sababu tunakuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.​—Soma Mhubiri 9:11.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza sababu zinazoonyesha kwamba Mungu hasababishi uovu na kuteseka ulimwenguni leo, na jinsi anavyohisi tunapoteseka.

4. Ni nani anayefanya wanadamu wateseke?

Watu wengi wanaamini kwamba Mungu ndiye anayeutawala ulimwengu wote. Je, hilo ni kweli? Onyesha VIDEO.

Soma Yakobo 1:13 na 1 Yohana 5:19, kisha mzungumzie swali hili:

  • Je, Mungu ndiye anayesababisha uovu na kuteseka?

5. Utawala wa Shetani umekuwa na matokeo gani?

Soma Mwanzo 3:1-6, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Shetani alisema uwongo gani?​—Ona mstari wa 4 na 5.

  • Shetani alisema nini ili kudai kwamba Yehova anawanyima wanadamu jambo fulani zuri?

  • Kulingana na madai ya Shetani, je, wanadamu wanamhitaji Yehova awe Mtawala wao ili wawe na furaha?

Soma Mhubiri 8:9, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa kuwa Yehova si Mtawala wa ulimwengu huu, hali zimekuwaje?

  1. Adamu na Hawa walikuwa wakamilifu na waliishi katika Paradiso. Lakini walimsikiliza Shetani wakamwasi Yehova

  2. Baada ya Adamu na Hawa kuasi, ulimwengu ulijaa dhambi, mateso, na kifo

  3. Yehova atakomesha dhambi, mateso, na kifo. Kwa mara nyingine, wanadamu watakuwa wakamilifu na kuishi katika Paradiso

6. Yehova anajali tunapoteseka

Je, Mungu anajali tunapoteseka? Ona mambo ambayo Mfalme Daudi na mtume Petro waliandika. Soma Zaburi 31:7 na 1 Petro 5:7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Unahisije unapojua kwamba Yehova anaona na anajali tunapoteseka?

7. Mungu atakomesha mateso yote yanayowapata wanadamu

Soma Isaya 65:17 na Ufunuo 21:3, 4, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini inafariji kujua kwamba Yehova ataondoa madhara yote yanayowapata wanadamu?

Je, wajua?

Shetani aliposema uwongo wa kwanza alimchongea Yehova, yaani, alimharibia Yehova sifa kwa kudai kwamba ni Mtawala asiye na haki na upendo. Hivi karibuni, Yehova atalitakasa jina lake atakapoondoa mateso yanayowapata wanadamu. Hilo linamaanisha, atathibitisha kwamba utawala wake ndio utawala bora. Kutakaswa kwa jina la Yehova ndilo jambo muhimu zaidi ulimwenguni.​—Mathayo 6:9, 10.

WATU FULANI HUSEMA: “Kuteseka ni mpango wa Mungu.”

  • Wewe ungesemaje?

MUHTASARI

Shetani Ibilisi na wanadamu wawili wa kwanza ndio waliosababisha uovu ulio ulimwenguni. Yehova anajali sana tunapoteseka na hivi karibuni ataondoa mateso.

Ungejibuje?

  • Shetani Ibilisi alimwambia Hawa uwongo gani?

  • Uasi wa Adamu na Hawa unatuathirije sisi sote?

  • Tunajuaje kwamba Yehova anajali tunapoteseka?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Jifunze jinsi Biblia inavyofafanua maana ya dhambi.

“Dhambi Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Soma mengi kuhusu suala ambalo Shetani Ibilisi alizusha katika bustani ya Edeni.

“Kwa Nini Mungu Anaruhusu Watu Wateseke?” (Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 2014)

Chunguza majibu yenye kuridhisha ya maswali fulani magumu.

“Kwa Nini Wayahudi Wengi Waliuwawa? Kwa Nini Mungu Hakuzuia?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Ona jambo ambalo mwanamume fulani alijifunza kuhusu mateso aliyoona.

Siko Peke Yangu Tena (5:09)