SOMO LA 29

Ni Nini Hutokea Tunapokufa?

Ni Nini Hutokea Tunapokufa?

Je, umewahi kufiwa na mtu unayempenda? Katika kipindi hicho kigumu huenda ulijiuliza: ‘Ni nini hutokea tunapokufa? Je, tutawaona tena wapendwa wetu wakati ujao?’ Katika somo hili na linalofuata, tutachunguza majibu yenye kufariji yaliyo katika Biblia.

1. Ni nini hutokea tunapokufa?

Yesu alilinganisha kifo na usingizi mzito. Mtu ambaye amelala usingizi mzito hajui kinachoendelea. Kwa nini kifo kinalinganishwa na usingizi? Baada ya kufa mtu hawezi kuhisi maumivu. Hawezi kuhisi upweke hata kama aliwapenda sana marafiki na watu wa familia yake. Biblia inasema kwamba “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.”​—Soma Mhubiri 9:5.

2. Kwa nini ni muhimu kujua ukweli kuhusu kifo?

Watu wengi wanaogopa kifo, hata wanawaogopa watu waliokufa! Lakini mambo ambayo Biblia inasema kuhusu kifo yanaweza kukufariji. Yesu alisema: “Kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) Baadhi ya dini hufundisha kwamba mtu anapokufa nafsi yake huendelea kuishi, lakini Biblia haifundishi hivyo. Basi, hakuna mtu anayeteseka baada ya kufa. Pia, kwa sababu watu waliokufa hawajui jambo lolote, hawawezi kutudhuru. Hivyo, hatuhitaji kuwatuliza au kuwaabudu watu waliokufa, wala kusali kwa ajili yao.

Watu fulani hudai kwamba wana uwezo wa kuwasiliana na watu waliokufa. Lakini hilo haliwezekani. Kama tulivyojifunza, “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.” Wale wanaofikiri wanawasiliana na wapendwa wao waliokufa, inawezekana kwamba wanawasiliana na roho waovu ambao hujifanya kuwa watu waliokufa. Kwa hiyo, kujua ukweli kuhusu kifo hutulinda dhidi ya roho waovu. Yehova anatuonya kwamba tusijaribu kuwasiliana na watu waliokufa kwa sababu anajua tukiwasiliana na roho waovu tutapata madhara.​​—Soma Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu kifo na uimarishe imani yako kwa Mungu mwenye upendo, ambaye hawaadhibu watu waliokufa.

3. Jifunze ukweli kuhusu hali ya watu waliokufa

Ulimwenguni pote, watu wanaamini mambo mbalimbali kuhusu jambo linalotokea tunapokufa. Bila shaka, haiwezekani kwamba imani hizo zote ni za kweli.

  • Katika eneo lenu watu wanaamini nini kuhusu hali ya watu waliokufa?

Ili kuona jambo ambalo Biblia inafundisha, onyesha VIDEO.

Soma Mhubiri 3:20, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kulingana na andiko hili, ni nini hutokea mtu anapokufa?

  • Je, kuna sehemu yoyote ya mtu aliyekufa inayoendelea kuishi?

Biblia inatuambia kuhusu kifo cha Lazaro, aliyekuwa rafiki wa karibu wa Yesu. Soma Yohana 11:11-14, ili uone jambo ambalo Yesu alisema kuhusu hali ya Lazaro. Kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yesu alilinganisha kifo na nini?

  • Hilo linatufundisha nini kuhusu hali ya watu waliokufa?

  • Una maoni gani kuhusu jinsi Biblia inavyofafanua kifo?

4. Ni muhimu kujua ukweli kuhusu kifo

Kujua ukweli kuhusu kifo, hutusaidia tusiwaogope watu waliokufa. Soma Mhubiri 9:10, kisha mzungumzie swali hili:

  • Je, watu waliokufa wanaweza kutudhuru?

Ukijifunza ukweli ulio katika Biblia kuhusu watu waliokufa, hutaamini uwongo wa kwamba tunapaswa kuwatuliza au kuwaabudu watu waliokufa. Soma Isaya 8:19 na Ufunuo 4:11, kisha mzungumzie swali hili:

  • Unafikiri Yehova anahisije kuhusu mtu anayeabudu au kutafuta msaada kutoka kwa watu waliokufa?

Ukweli kuhusu kifo unatuweka huru kutoka kwenye desturi zisizompendeza Yehova

5. Tunapata faraja tunapojifunza ukweli kuhusu kifo

Watu wengi wamefundishwa kwamba watakapokufa wataadhibiwa kwa sababu ya makosa waliyofanya zamani. Lakini inafariji kujua kwamba hakuna mtu anayeteseka baada ya kufa, hata mtu ambaye alifanya mambo mabaya sana. Soma Waroma 6:7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kama tulivyosoma katika Biblia, mtu anapokufa anawekwa huru au anaondolewa hatia ya dhambi yake. Je, unafikiri kuna mtu aliyekufa ambaye anaendelea kuteseka kwa sababu ya makosa aliyofanya?

Tunapoendelea kujifunza mengi kumhusu Yehova, ndivyo tunavyozidi kutambua kwamba hawezi kamwe kuwatesa watu waliokufa. Soma Kumbukumbu la Torati 32:4 na 1 Yohana 4:8, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, Mungu mwenye sifa zinazotajwa kwenye maandiko hayo anaweza kuwatesa watu waliokufa?

  • Je, umefarijika kujua ukweli kuhusu kifo? Kwa nini?

WATU FULANI HUSEMA: “Ninaogopa kwamba nitakapokufa nitateseka.”

  • Unaweza kuwasomea mistari gani ya Biblia ili kuwafariji?

MUHTASARI

Mtu anapokufa, uhai wake unakoma. Watu waliokufa hawateseki wala hawawezi kuwadhuru walio hai.

Ungejibuje?

  • Ni nini hutokea tunapokufa?

  • Kwa nini ni muhimu kujua ukweli kuhusu kifo?

  • Kwa nini kujifunza ukweli kuhusu kifo kunatufariji?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ona maana halisi ya neno “nafsi” katika Biblia.

“Nafsi Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Je, Mungu huwaadhibu watu waovu katika moto wa mateso?

Je, Watu Watateswa Katika Moto wa Mateso? (3:07)

Je, tunapaswa kuwaogopa watu waliokufa?

Roho za Wafu, Je, Zaweza Kukusaidia au Kukuumiza? Je, Ziko Kweli? (broshua)

Ona jinsi mwanamume fulani alivyofarijika baada ya kujifunza ukweli kuhusu jambo linalotokea tunapokufa.

“Nilivutiwa na Majibu ya Biblia Yaliyo Wazi na Yanayoeleweka” (Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 2015)