SOMO LA 31

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu ndio ujumbe muhimu zaidi katika Biblia. Yehova atatumia Ufalme huo kutimiza kusudi lake la mwanzoni la kuifanya dunia iwe paradiso. Ufalme huo ni nini? Tunajuaje kwamba umeanza kutawala? Ufalme huo umetimiza mambo gani? Na utatimiza mambo gani wakati ujao? Maswali hayo yatajibiwa katika somo hili na masomo mawili yanayofuata.

1. Ufalme wa Mungu ni nini, na Mfalme wake ni nani?

Ufalme huo ni serikali iliyoanzishwa na Yehova Mungu mwenyewe. Mfalme wa Ufalme huo ni Yesu Kristo, na anatawala kutoka mbinguni. (Mathayo 4:17; Yohana 18:36) Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Atatawala akiwa Mfalme . . . milele.” (Luka 1:32, 33) Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu atatawala watu wote duniani.

2. Ni nani wanaotawala pamoja na Yesu?

Yesu anatawala pamoja na wengine. “Watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa . . . watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10) Ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Kristo? Tangu Yesu alipokuja duniani, mamilioni ya watu wamekuwa wafuasi wake. Lakini watu 144,000 ndio tu wanaoenda mbinguni kutawala pamoja na Yesu. (Soma Ufunuo 14:1-4.) Wakristo wengine wote walio duniani watakuwa raia wa Ufalme huo.​—Zaburi 37:29.

3. Kwa nini Ufalme wa Mungu ni bora kuliko serikali za wanadamu?

Ingawa watawala wa serikali za wanadamu wanajitahidi kufanya mambo mazuri, hawana uwezo wa kufanya mambo yote wanayotaka. Baada ya kipindi chao cha kutawala kwisha, huenda watawala wengine wabinafsi wakaanza kutawala na hawawajali raia wao. Lakini kuhusu Yesu Mtawala wa Ufalme wa Mungu, hakuna mtawala mwingine atakayechukua nafasi yake. Mungu “[ameusimamisha] ufalme ambao hautaangamizwa kamwe.” (Danieli 2:44) Yesu atatawala dunia yote, na hatakuwa na ubaguzi. Yesu ni mwenye upendo, fadhili, na haki, naye atawafundisha watu kuwatendea wengine kwa njia hiyohiyo, yaani, kwa upendo, fadhili, na haki.​—Soma Isaya 11:9.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza uone kwa nini Ufalme wa Mungu ni serikali bora kuliko serikali zote za wanadamu.

4. Serikali yenye nguvu itaitawala dunia yote

Yesu Kristo ana nguvu nyingi sana za kutawala kuliko mtawala yeyote katika historia. Soma Mathayo 28:18, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini Yesu ana mamlaka kubwa zaidi kuliko mtawala yeyote wa serikali za wanadamu?

Serikali za wanadamu hubadilika-badilika, na kila serikali hutawala sehemu fulani ya dunia. Namna gani Ufalme wa Mungu? Soma Danieli 7:14, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kwa nini inafurahisha kujua kwamba Ufalme wa Mungu “hautaangamizwa”?

  • Kwa nini tunafurahi kujua kwamba utaitawala dunia yote?

5. Ni lazima serikali za wanadamu ziondolewe

Kwa nini ni lazima Ufalme wa Mungu uondoe serikali za wanadamu? Onyesha video, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Utawala wa serikali za wanadamu umekuwa na matokeo gani?

Soma Mhubiri 8:9, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, unafikiri Ufalme wa Mungu unapaswa kuondoa serikali za wanadamu? Kwa nini?

6. Watawala wa Ufalme wa Mungu wanaelewa hali yetu

Kwa kuwa Mfalme wetu, Yesu, aliwahi kuwa mwanadamu, anaweza ‘kuusikitikia udhaifu wetu.’ (Waebrania 4:15) Wanaume na wanawake waaminifu 144,000 ambao watatawala pamoja na Yesu wamechaguliwa na Yehova “kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.”​—Ufunuo 5:9.

  • Je, unafarijika kujua kwamba Yesu na watawala wenzake wanaelewa hali za wanadamu? Kwa nini?

Yehova amewachagua wanaume na wanawake kutoka katika malezi mbalimbali watawale pamoja na Yesu

7. Sheria za Ufalme wa Mungu ni bora zaidi

Serikali huweka sheria ambazo zimekusudiwa kuwanufaisha na kuwalinda raia wake. Ufalme wa Mungu pia una sheria ambazo zinapaswa kufuatwa na raia wake. Soma 1 Wakorintho 6:9-11, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Unafikiri ulimwengu utakuwaje kila mtu atakapofuata sheria za Mungu? a

  • Je, unafikiri Yehova ana haki ya kuwawekea sheria raia wa Ufalme wake? Kwa nini?

  • Ni nini kinachoonyesha kwamba watu ambao hawafuati sheria hizo wanaweza kubadilika?​—Ona mstari wa 11.

Serikali huweka sheria ili kuwalinda na kuwanufaisha raia wake. Ufalme wa Mungu una sheria bora zinazowalinda na kuwanufaisha raia wake

HUENDA MTU AKAULIZA: “Ufalme wa Mungu ni nini?”

  • Unawezaje kujibu swali hilo?

MUHTASARI

Ufalme wa Mungu ni serikali halisi iliyo mbinguni ambayo itaitawala dunia yote.

Ungejibuje?

  • Watawala wa Ufalme wa Mungu ni nani?

  • Kwa nini Ufalme wa Mungu ni bora kuliko serikali zote za wanadamu?

  • Yehova anatarajia raia wa Ufalme wake wafanye mambo gani?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza uone Yesu alisema utawala wa Mungu utatawala kutokea wapi.

“Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanachagua kuwa washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu badala ya serikali za wanadamu?

Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu (1:43)

Chunguza jinsi Biblia inavyofafanua wale 144,000 ambao wamechaguliwa na Yehova kutawala pamoja na Yesu.

“Ni Nani Wanaoenda Mbinguni?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Ni nini kilichomsadikishia mwanamke aliyekuwa gerezani kwamba Mungu peke yake ndiye anayeweza kuleta ulimwengu wenye haki?

“Jinsi Nilivyopata Suluhisho la Ukosefu wa Haki” (Amkeni!, Novemba 2011)

a Baadhi ya sheria hizo zitazungumziwa katika Sehemu ya 3.