SOMO LA 37

Maoni ya Biblia Kuhusu Pesa na Kazi

Maoni ya Biblia Kuhusu Pesa na Kazi

Je, umewahi kulemewa na mahangaiko kuhusu kazi au pesa? Huenda ikawa vigumu kushughulikia mahitaji yetu na wakati huohuo kumtolea Yehova ibada anayostahili. Biblia inatupatia ushauri unaoweza kutusaidia.

1. Biblia inasema nini kuhusu kazi?

Mungu anataka tufurahie kazi yetu. Biblia inasema hivi: “Hakuna jambo bora analoweza kufanya mtu kuliko . . . kufurahia kazi yake ngumu.” (Mhubiri 2:24) Yehova ni mfanyakazi mwenye bidii. Tunapomwiga kwa kufanya kazi kwa bidii, tunamfurahisha na tunaridhika.

Kufanya kazi ni muhimu. Lakini hatupaswi kamwe kuruhusu kazi iwe muhimu kuliko ibada yetu kwa Yehova. (Yohana 6:​27) Yehova anatuahidi kwamba tukimtanguliza, atatuandalia mahitaji yetu ya kimwili.

2. Biblia inasema nini kuhusu pesa?

Biblia inasema ‘pesa ni ulinzi,’ lakini pia inatuonya kwamba pesa peke yake haziwezi kutuletea furaha. (Mhubiri 7:12) Basi tunatiwa moyo tusipende pesa bali ‘turidhike na vitu tulivyo navyo.’ (Soma Waebrania 13:5.) Tunaporidhika na vitu tulivyo navyo, tunaepuka mahangaiko ya kutafuta vitu vingi zaidi. Tunaepuka madeni yasiyo ya lazima. (Methali 22:7) Na tunaepuka hatari ya kucheza kamari au kunaswa na njia za kupata utajiri wa haraka.

3. Tunawezaje kutumia pesa zetu kwa ukarimu?

Yehova ni Mungu mkarimu na tunamwiga tunapokuwa “wakarimu, tayari kushiriki vitu na wengine.” (1 Timotheo 6:18) Tunaweza kutumia pesa zetu kwa ukarimu kwa kutoa michango katika kutaniko na kuwasaidia watu wengine wanaohitaji msaada, hasa waabudu wenzetu. Yehova anapendezwa hasa na nia yetu ya kutoa, bali si kiasi tunachotoa. Tunapotoa kwa ukarimu kutoka moyoni, tunakuwa na furaha na tunamfurahisha Yehova.​—Soma Matendo 20:35.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze manufaa ya kuwa na mtazamo uliosawazika kuhusu kazi na jinsi ya kuridhika.

4. Mheshimu Yehova kupitia mazoea yako ya kufanya kazi

Urafiki wetu na Yehova unapaswa kutuchochea kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu kazi. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, ulifurahia nini kuhusu mtazamo wa Jason na mwenendo wake kazini?

  • Jason alifanya nini ili kuwa na usawaziko kuhusu kazi?

Soma Wakolosai 3:23, 24, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini ni muhimu kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu kazi?

Kufanya kazi ni muhimu. Lakini hatupaswi kamwe kuruhusu kazi iwe muhimu kuliko ibada yetu kwa Yehova

5. Tunanufaika tunaporidhika

Watu wengi hujitahidi kutafuta pesa nyingi iwezekanavyo. Lakini Biblia inatoa ushauri tofauti. Soma 1 Timotheo 6:6-8, kisha mzungumzie swali hili:

  • Biblia inatutia moyo tufanye nini?

Tunaweza kuwa na furaha hata tukiwa na vitu vichache sana. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Ingawa familia hizo hazina pesa nyingi, kwa nini wana furaha?

Namna gani ikiwa tuna vitu vingi na bado tunatamani kupata vingi zaidi? Yesu alitoa mfano unaoonyesha hatari ya kufanya hivyo. Soma Luka 12:15-21, kisha mzungumzie swali hili:

  • Umejifunza nini kutokana na mfano wa Yesu?​—Ona mstari wa 15.

Soma na ulinganishe Methali 10:22 na 1 Timotheo 6:10. Kisha mzungumzie maswali haya:

  • Unafikiri ni jambo gani lililo muhimu zaidi? Kuwa rafiki ya Yehova, au kuwa na pesa nyingi sana? Kwa nini?

  • Ni matatizo gani yanayosababishwa na kutafuta pesa nyingi zaidi?

6. Yehova atatuandalia mahitaji yetu

Inapokuwa vigumu kupata kazi au pesa, tunapata nafasi ya kuonyesha kama kweli tunamtegemea Yehova. Onyesha VIDEO ili kuona jinsi tunavyoweza kukabiliana na matatizo ya kifedha, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, ndugu huyo alikabili changamoto gani?

  • Alifanya nini ili kukabiliana na changamoto hizo?

Soma Mathayo 6:25-34, kisha mzungumzie swali hili:

  • Yehova amewaahidi nini wale wanaomtanguliza?

WATU FULANI HUSEMA: “Lazima nifanye kazi kwa bidii ili kuiandalia familia yangu. Siwezi kuhudhuria mikutano ya kutaniko kila juma.”

  • Ni andiko gani linalokuthibitishia kwamba kutanguliza ibada yako kwa Yehova ndio uamuzi bora?

MUHTASARI

Tunahitaji kazi na pesa lakini mambo hayo hayapaswi kamwe kutuzuia kumtumikia Yehova.

Ungejibuje?

  • Ni nini kinachoweza kukusaidia uwe na usawaziko kuhusu kazi?

  • Kuridhika kunaweza kukunufaishaje?

  • Unaweza kuonyeshaje kwamba unaamini ahadi ya Yehova ya kuwaandalia mahitaji watu wake?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza uone kama Biblia inafundisha kwamba ni vibaya kuwa na pesa.

“Je, Pesa Ndio Chanzo cha Uovu Wote?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Jifunze jinsi tunavyoweza kutumia pesa zetu kwa njia inayomfurahisha Mungu.

“Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Je, kucheza kamari kuna madhara yoyote?

“Maoni ya Biblia​—Kucheza Kamari” (Amkeni!, Machi 2015)

Ona jambo lililomchochea mtu aliyekuwa mwizi na mcheza-kamari abadili maisha yake.

“Nilipenda Sana Mashindano ya Farasi” (Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 2011)