SOMO LA 39

Maoni ya Mungu Kuhusu Damu

Maoni ya Mungu Kuhusu Damu

Damu ni muhimu sana. Bila damu hatuwezi kuendelea kuwa hai. Akiwa Muumba wetu, Mungu ana haki ya kuweka sheria kuhusu damu. Ametoa maagizo gani kuhusu damu? Je, tunaweza kula damu au kutiwa mishipani? Na unawezaje kufanya maamuzi mazuri kuhusu damu?

1. Yehova ana maoni gani kuhusu damu?

Nyakati za kale, Yehova aliwaambia hivi waabudu wake: “Uhai wa kila kiumbe umo katika damu yake.” (Mambo ya Walawi 17:14) Kulingana na maoni ya Yehova, damu inawakilisha uhai. Kwa kuwa uhai ni zawadi takatifu kutoka kwa Mungu, basi pia damu ni takatifu.

2. Mungu anakataza matumizi gani ya damu?

Kabla ya Ukristo, Yehova aliwaamuru waabudu wake wasile damu. (Soma Mwanzo 9:4 na Mambo ya Walawi 17:10.) Baadaye, kupitia baraza linaloongoza aliwaagiza Wakristo ‘waendelee kujiepusha na damu.’​—Soma Matendo 15:28, 29.

Kujiepusha na damu kunamaanisha nini? Ikiwa daktari angekuambia ujiepushe na pombe, ungeacha kunywa pombe. Hata hivyo, je, ungekula chakula kilichochanganywa na pombe, au ungekubali kutiwa pombe mishipani? Bila shaka, hungekubali. Vivyo hivyo, amri ya Mungu kwamba tujiepushe na damu inamaanisha hatupaswi kula au kunywa damu, wala kula nyama ya mnyama ambaye hajatolewa damu. Wala hatupaswi kula chakula ambacho kimechanganywa na damu.

Namna gani kutumia damu katika matibabu? Baadhi ya matibabu yanavunja sheria za Mungu moja kwa moja. Matibabu hayo yanatia ndani kutiwa damu mishipani. Iwe ni damu nzima au sehemu kuu za damu, yaani, chembe nyekundu, chembe nyeupe, vigandisha-damu, na plazima. Kuhusu matibabu fulani, huenda isionekane wazi kama yanavunja sheria ya Mungu au la. Baadhi ya matibabu hayo yanahusisha kutumia visehemu vilivyotolewa kwenye mojawapo ya sehemu kuu za damu. Na matibabu mengine yanahusisha matumizi ya damu ya mgonjwa mwenyewe. Tunapofikiria matibabu hayo, kila mmoja wetu anapaswa kufanya uamuzi wake mwenyewe. a​—Wagalatia 6:5.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi ya kufanya maamuzi kuhusu matibabu yanayohusisha damu.

3. Fanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova kuhusu matibabu

Unawezaje kufanya maamuzi ya matibabu yanayopatana na maoni ya Mungu kuhusu damu? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie umuhimu wa kufuata hatua zinazoonyeshwa hapa.

  • Sali ili upate hekima.​—Yakobo 1:5

  • Fanya utafiti kuhusu kanuni za Biblia na jinsi ya kuzitumia.​—Methali 13:16.

  • Chunguza matibabu mbalimbali yanayopatikana katika eneo lenu.

  • Amua matibabu ambayo huwezi kamwe kuyakubali.

  • Hakikisha kwamba utabaki na dhamiri safi baada ya kufanya uamuzi.​—Matendo 24:16. b

  • Tambua kwamba hakuna mtu anayepaswa kukufanyia uamuzi kuhusu mambo yanayohusisha dhamiri, iwe ni mwenzi wako wa ndoa, mzee wa kutaniko, au mwalimu wako wa Biblia.​—Waroma 14:12.

  • Andika uamuzi wako.

4. Mashahidi wa Yehova hutafuta matibabu bora

Inawezekana kutii sheria ya Mungu kuhusu damu na wakati huohuo kupata matibabu bora yasiyohusisha damu. Onyesha VIDEO.

Soma Tito 3:2, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini tunapaswa kuzungumza na madaktari kwa heshima na upole?

Matibabu yasiyokubalika

Mkristo atajifanyia uamuzi

A. Plazima ya damu

Visehemu vya plazima

B. Chembe nyeupe

Visehemu vya chembe nyeupe

C. Vigandisha-damu

Visehemu vya vigandisha-damu

D. Chembe nyekundu

Visehemu vya chembe nyekundu

 5. Matibabu yanayohusisha visehemu vya damu

Damu ina sehemu kuu nne​—chembe nyekundu, chembe nyeupe, vigandisha-damu, na plazima. Sehemu hizo zina sehemu nyingine ndogo zaidi zinazoitwa visehemu vya damu. c Baadhi ya visehemu hivyo huongezwa katika dawa zinazotumiwa kutibu magonjwa au kuzuia kuvuja kwa damu.

Inapohusu visehemu vya damu, kila Mkristo anapaswa kujifanyia uamuzi wake mwenyewe unaotegemea dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Huenda baadhi ya Wakristo wakakataa matibabu au mbinu za matibabu zinazohusisha visehemu vya damu. Na wengine wanaweza kuhisi kwamba dhamiri zao zinawaruhusu kukubali visehemu vya damu.

Unapofanya maamuzi yako, fikiria swali hili:

  • Ninawezaje kumweleza daktari sababu yangu ya kukubali au kukataa matumizi ya visehemu fulani vya damu?

HUENDA MTU AKAULIZA: “Kuna ubaya gani kuongezwa damu mwilini?”

  • Wewe una maoni gani?

MUHTASARI

Yehova anataka tuione damu kuwa takatifu.

Ungejibuje?

  • Kwa nini Yehova anaiona damu kuwa takatifu?

  • Tunajuaje kwamba amri ya Mungu ya kujiepusha na damu inahusisha kuepuka kutiwa damu mishipani?

  • Unawezaje kufanya maamuzi mazuri kuhusu matibabu yanayohusisha damu?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Unapaswa kufikiria mambo gani unapofanya maamuzi ya matibabu yanayohusisha damu yako mwenyewe?

“Maswali Kutoka kwa Wasomaji” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 2000)

Unapaswa kuzingatia mambo gani unapoamua ikiwa utakubali visehemu vya damu?

“Maswali Kutoka kwa Wasomaji” (Mnara wa Mlinzi, Juni 15, 2004)

Ni nini kilichomfanya daktari fulani aamini kwamba maoni ya Yehova kuhusu damu yanafaa?

“Nilikubali Maoni ya Mungu Kuhusu Damu” (Amkeni!, Desemba 8, 2003)

Jifunze jinsi wazee walio kwenye Halmashauri za Uhusiano na Hospitali wanavyowasaidia ndugu na dada zao.

Yehova Huwategemeza Wagonjwa (10:23)

a Ona Somo la 35, “Jinsi ya Kufanya Maamuzi Mazuri.”

b Ona  jambo kuu la 5, “Matibabu Yanayohusisha Visehemu vya Damu” na Maelezo ya Ziada 3, “Matibabu Yanayohusisha Damu.”

c Baadhi ya madaktari huona sehemu nne kuu za damu kuwa visehemu vya damu. Kwa hiyo, unapaswa kuhakikisha daktari anaelewa uamuzi wako kwamba hutakubali kutiwa mishipani damu nzima, chembe nyekundu, chembe nyeupe, vigandisha-damu, au plazima.