SOMO LA 40

Tunawezaje Kuwa Safi Machoni pa Mungu?

Tunawezaje Kuwa Safi Machoni pa Mungu?

Wazia mama anayemtayarisha mtoto wake mdogo ili aende shuleni. Anahakikisha kwamba mtoto ameoga na nguo zake ni safi. Kufanya hivyo kunamsaidia mtoto wake awe na afya nzuri na watu wengine wanaona kwamba wazazi wake wanamtunza vizuri. Vivyo hivyo, Baba yetu mwenye upendo Yehova, anataka tuwe safi kimwili na kiadili. Tunapokuwa safi, tunanufaika na tunamletea utukufu.

1. Tunawezaje kuwa safi kimwili?

Yehova anatuambia hivi: “Lazima muwe watakatifu.” (1 Petro 1:16) Kuwa watakatifu kunahusisha kuwa safi kimwili na kiadili. Tunaweza kuwa safi kimwili kwa kuoga kwa ukawaida na kudumisha nguo, nyumba, na magari yetu yakiwa safi. Pia, tunaweza kusaidia kufanya usafi katika Jumba letu la Ufalme. Tunapodumisha usafi wa kimwili tunamletea Yehova utukufu.​—2 Wakorintho 6:3, 4.

2. Ili tuwe safi, tunapaswa kuepuka mazoea gani?

Biblia inatuhimiza “tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Hivyo, tunajitahidi kuepuka jambo lolote linaloweza kuchafua mwili au akili zetu. Mawazo yetu yanapaswa kumfurahisha Yehova, basi tunajitahidi kabisa kuepuka mawazo yasiyofaa. (Zaburi 104:34) Pia, tunajitahidi kuepuka maneno machafu.​—Soma Wakolosai 3:8.

Ni nini kingine kinachoweza kutuchafua kimwili au kiadili? Kuna vitu vinavyoweza kuchafua mwili wetu. Kwa hiyo, tunaepuka kuvuta sigara, kutumia tumbaku, kutafuna miraa au mirungi, na kutumia dawa za kulevya. Tunapoepuka vitu hivyo, tunakuwa na afya bora na tunaonyesha kwamba tunaheshimu zawadi ya uhai. Pia, tunajitahidi kuwa na maadili safi kwa kuepuka mazoea machafu kama vile kupiga punyeto na kutazama ponografia. (Zaburi 119:37; Waefeso 5:5) Inaweza kuwa vigumu kushinda mazoea hayo, lakini Yehova anaweza kutusaidia kuyashinda.​—Soma Isaya 41:13.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi tunavyoweza kumheshimu Yehova kwa kuwa safi kimwili, na jinsi tunavyoweza kushinda mazoea machafu.

3. Usafi wa kimwili unamtukuza Yehova

Tunaweza kuelewa maoni ya Yehova kuhusu usafi kwa kuchunguza amri alizowapa Waisraeli wa kale. Soma Kutoka 19:10 na 30:17-19, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kulingana na mistari hii, Yehova ana maoni gani kuhusu usafi wa kimwili?

  • Ni mazoea gani yatakayokusaidia kudumisha usafi wa kimwili?

Tunahitaji muda na jitihada ili kudumisha usafi wa kimwili. Hata hivyo, tunaweza kudumisha usafi mahali popote tunapoishi iwe sisi ni maskini au matajiri. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Watu tunaowahubiria wanawezaje kumheshimu Yehova ikiwa tunatumia vifaa safi na nadhifu?

4. Shinda mazoea mabaya

Yehova anaweza kutusaidia kushinda zoea lolote baya

Ikiwa wewe ni mraibu wa kuvuta sigara au kutumia dawa za kulevya, huenda unaelewa jinsi ilivyo vigumu kushinda mazoea hayo. Ni nini ambacho kitakusaidia? Fikiria madhara unayopata kutokana na mazoea hayo. Soma Mathayo 22:37-39, kisha mzungumzie jinsi kuvuta sigara au kutumia dawa za kulevya kunavyoathiri . . .

  • urafiki wa mtu na Yehova.

  • familia ya mtu huyo na watu wanaomzunguka.

Chukua hatua ambazo zitakusaidia kushinda mazoea mabaya. a Onyesha VIDEO.

Soma Wafilipi 4:13, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kuwa na mazoea mazuri ya kusali, kujifunza Biblia, na kuhudhuria mikutano kunawezaje kumsaidia mtu apate nguvu za kushinda mazoea mabaya?

5. Jitahidi kushinda mawazo na mazoea machafu

Soma Wakolosai 3:5, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Tunajuaje kwamba kutazama ponografia, kutuma ujumbe au picha za ngono, na kupiga punyeto ni mazoea machafu machoni pa Yehova?

  • Je, inawezekana kufuata sheria za Yehova kuhusu usafi wa maadili? Kwa nini?

Jifunze jinsi ya kushinda mawazo machafu. Onyesha VIDEO.

Yesu alitoa mfano unaoonyesha kwamba tunapaswa kuchukua hatua thabiti ili tuendelee kudumisha maadili safi. Soma Mathayo 5:29, 30, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ingawa Yesu hakumaanisha tunapaswa kujisababishia majeraha ya kimwili, alionyesha kwamba tunapaswa kuchukua hatua fulani. Mtu anapaswa kuchukua hatua gani thabiti ili kuepuka mawazo machafu? b

Ikiwa unapambana ili kushinda mawazo machafu, Yehova anathamini jitihada zako. Soma Zaburi 103:13, 14, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ikiwa unapambana na zoea chafu, andiko hili linawezaje kukusaidia uendelee kupambana?

Usife moyo, endelea kupambana!

Huenda ukajiambia hivi, ‘Nimeshindwa, hakuna haja ya kuendelea kupambana.’ Lakini fikiria jambo hili: Mkimbiaji anapoanguka haimaanishi kwamba hawezi kuendelea na mbio hizo, pia haimaanishi kwamba anapaswa kurudi nyuma na kuanza tena. Vivyo hivyo, hata unapolemewa na kurudia zoea hilo, haimaanishi kwamba huwezi kulishinda. Wala haimaanishi kwamba jitihada ulizofanya ni za bure. Ni jambo la kawaida kujikwaa. Lakini usife moyo! Kwa msaada wa Yehova, unaweza kushinda zoea baya.

WATU FULANI HUSEMA: “Mimi ni mraibu. Siwezi kuacha.”

  • Unaweza kutumia andiko gani kumsaidia mtu huyo aone kwamba Yehova anaweza kumsaidia aache zoea baya?

MUHTASARI

Tunamfurahisha Yehova tunapodumisha mwili, mawazo, na mwenendo wetu ukiwa safi.

Ungejibuje?

  • Kwa nini ni muhimu sana kudumisha usafi?

  • Unawezaje kudumisha usafi wa kimwili?

  • Unawezaje kudumisha mawazo na mwenendo wako ukiwa safi?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ni mambo gani rahisi unayoweza kufanya ili kudumisha usafi wa kimwili hata kama huna vitu vingi vya kimwili?

Usafi na Afya​—Kunawa Mikono (3:01)

Ona hatua unazoweza kuchukua ili uache kuvuta sigara.

“Jinsi ya Kuacha Kuvuta Sigara” (Amkeni!, Mei 2010)

Chunguza madhara ya kutazama ponografia.

“Ponografia​—Je, Ina Madhara?” (Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 2013)

Ona jinsi mwanamume fulani alivyoshinda zoea la kutazama ponografia.

“Nilishindwa Mara Nyingi Kabla ya Kushinda” (Mnara wa Mlinzi Na. 4 2016)

a Gazeti lenye kichwa “Jinsi ya Kuacha Kuvuta Sigara,” lililo kwenye sehemu ya Chunguza Zaidi katika somo hili, linaeleza hatua ambazo mtu anapaswa kuchukua ili kushinda uraibu.

b Ili kupata msaada wa kushinda zoea la kupiga punyeto, ona “Ninaweza Kushinda Jinsi Gani Mazoea ya Kupiga Punyeto?” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1, sura ya 25.